RUMAFRICA Magazine

RUMAFRICA FASHION

RUMAFRICA FASHION

MATATIZO YANAYOTOKEA KWA WANADOA KUACHANA. DO NOT MISS SEMINA YA NDOA 30.08.2014 SINZA - DAR

Shalom watu wa Mungu.
Leo nataka kuongea kuhusu athari ambazo huachiliwa katika ulimwengu wa roho pale wanandoa wanapoachana. Kwanza tuangalie ndoa huanzaje!
Ni desturi ya ndoa karibu zote za kikristo zinapokuwa zinafungwa wanandoa huapishwa madhabahuni kwa kulazimishwa kusema:- “Nitakuwa nawe kwa shida na raha, mpaka kifo kitakapotutenganisha”

Hiki ni kiapo kizito sana. Japo watu wengi huapa pasipo kutafakari maneno yaliyomo ndani yake, lakini pia hawatafakari mustakabali na mwenendo wa ndoa yenyewe kwa siku za baadae ukizingatia kuwa unayeoana naye ni binadamu anayeweza kugeuka wakati wowote.

Unapoapa madhabahuni maana yake umemtaka Mungu awe shahidi na msimamizi wa hicho unachokiapia!
Kama ukisema nitakuwa pamoja na mtu huyu katika mizengwe na mapungufu yake yote wala hakuna zengwe lolote la kututenganisha isipokuwa kifo peke yake. Maana yake maneno haya ni kwamba umemhakikishia mungu kwamba kila iitwayo siku atakuona ukiwa umeambatana na mwenzi wako, na kama ikitokea akakuona uko peke yako maana yake umeachana na mwenzi wako basi Mungu ajuwe kuwa kifo kimekwisha fanya kazi yake ya kuwatenganisha.

Mimi nadhani waliotunga hiki kiapo walirejea lile andiko lisemalo “aliowaunganisha Mungu mwanadamu asiwatenganishe”

Mimi nadhani watu waliotunga kiapo hiki hawakuyachunguza maandiko kwa kina! Maana biblia ile ile inasema “Yeyote amwachaye mkewe na kuoa mwingine azini, isipokuwa ni kwa makosa ya uasherati”

Sasa shida inakuja pale wanandoa anapomfumania mwenziwe. Ndipo sasa wanaanza kuangalia andiko linalosema “amwachaye mkewe na kuoa mwingine azini, isipokuwa ni kwa makosa ya uasherati” hivyo moja kwa moja mtu huyu hujiona kuwa na haki zote za kuachana na mwenziwe.

Anasahau kama kule nyuma aliapa akisema hakuna chochote kinachoweza kumwachanisha na mwenziwe isipokuwa kifo!

Hivyo basi, wanandoa hawa wakishaachana moja kwa moja kwa wakati huo huo katika ulimwengu wa roho mauti inafunguliwa mlango kwao. Kuwa makini sana mtu wa Mungu usiingie kwenye maagano ambayo huyafahamu maana yake.

Bwana atusaidie sana.

Comments