RUMAFRICA Magazine

RUMAFRICA FASHION

RUMAFRICA FASHION

ETI KWELI MAKAHABA, MATEJA WAMPONZA MCHUNGAJI GWAJIMA KUHAMISHA KANISA LAKE?


WAANDISHI WETU/Amani
NI msala! Kupigwa notisi ya kutakiwa kuhamisha kanisa kwa Mchungaji Kiongozi wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Josephat Gwajima kumeelezwa kusababishwa na baadhi ya makahaba, wavuta bangi na wengineo, Amani limeambiwa.


Mchungaji Kiongozi wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, Josephat Gwajima.

Mapema wiki iliyopita, Gwajima amepewa notisi na Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) ikimtaka kuhamisha kanisa lake kwenye Viwanja vya Tanganyika Packers, Kawe jijini Dar ifikapo Machi 9, mwaka huu.

Taarifa zilizodakwa na gazeti hili zinasema kuwa, barua mbili za NHC zilipelekwa kwa makanisa mawili likiwemo la Ngurumo ya Upako la Nabii George David ‘Geor Dave’ (Amani lina nakala).
Amani lilifika kwenye viwanja hivyo mwanzoni mwa wiki hii na kuzungumza na wenyeji wa eneo hilo ambao walisema hata wao wanasikia mchungaji huyo anatakiwa kuondoka eneo hilo lakini kwa ajili ya kupisha ujenzi wa nyumba za NHC.

Katika Ofisi ya Serikali ya Mtaa wa Mzimuni, Amani lilizungumza na mwenyekiti wake, Hassan Faraji Nganyani ambapo alikiri kupata kopi ya barua hiyo.

“Ni kweli ndugu waandishi kopi ya barua kutoka Shirika la Nyumba la Taifa tumepata, inawataka viongozi wa makanisa hayo mawili kuhama ifikikapo Machi 9, mwaka huu,” alisema kiongozi huyo.

Kiongozi huyo alikwenda mbele zaidi kwa kusema kuwa, kuhamisha makanisa hayo ili kujenga nyumba za shirika ni sahihi lakini tatizo jingine ni kwamba, siku ambazo waumini hao hawakeshi kanisani hapo, kuna makundi ya watu hufika eneo hilo na kufanya ukahaba, wengine kutupa vichanga baada ya kutoa mimba achilia mbali wahuni wanaovuta bangi na mateja mbalimbali ‘wabwia unga’.


Mzee mmoja ambaye alisema ni mstaafu wa serikali alisema kuwa, alishapeleka maombi kwenye shirika la nyumba akitaka eneo hilo lidhibitiwe baada ya baadhi ya watu, ukiacha makanisa kulitumia vibaya.
“Ni kweli siku kukiwa hakuna ibada, wahuni, wavuta bangi na watumia madawa ya kulevya wanageuza maskani yao. Nadhani NHC walizingatia pia maombi yangu na ya wengine,” alisema mstaafu huyo.

Waandishi walifakiwa kuongea na baadhi ya watu wanaoabudu katika Kanisa la Gwajima ambapo walisema eneo hilo lilikuwa limezoeleka kwa kila mtu aliyekuwa akiabudu hapo.Baadhi yao walisema uwanja huo ulikuwa unatosheleza umati uliokuwa ukifika kusikia Neno la Mungu lakini baada ya kupata notisi hawajui watapata wapi kiwanja kikubwa kama hicho.

Juhudi za kumpata Mchungaji Gwajima hazikufua dafu baada ya simu yake kuita muda mrefu bila kupokelewa. Amani lilipofika kanisani kwake ilidaiwa yuko safarini.

Mchungaji Gwajima alihamia katika viwanja hivyo mwaka 2008 akitokea Ubungo Chai Bora, Dar ambako kulionekana kutokidhi idadi ya watu.Nabii Geor Dave naye alipotafutwa na Amani kwa njia ya simu hakupatikana hewani hadi gazeti linakwenda mitamboni.