RUMAFRICA Magazine

RUMAFRICA FASHION

RUMAFRICA FASHION

MASWALI 10 TATA KIFO CHA MTIKILA!

Na Waandishi Wetu
BASI tena! Kifo cha ajali ya gari cha aliyekuwa Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia (DP) na Kiongozi wa Kanisa la Full Salvation, Mchungaji Christopher Mtikila kimewaacha wananchi na majonzi makubwa lakini nyuma yake, Uwazi limebaini maswali 10 tata kuhusu ajali hiyo.
Aliyekuwa Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia (DP) na Kiongozi wa Kanisa la Full Salvation, Mchungaji Christopher Mtikila enzi za uhai wake.

Ajali hiyo ilitokea saa kumi na mbili asubuhi ya Jumapili iliyopita, eneo la Msolwa, Chalinze wilayani Bagamoyo, Pwani ambapo gari aina ya Toyota Corolla lenye namba za usajili T 189 AGM lilipoteza mwelekeo na kuingia bondeni. Mtikila alipoteza maisha papohapo huku watu watatu, akiwemo dereva wa gari hilo wakinusurika.

WALIOKUWEMO
Mbali na Mtikila watu hao watatu ni dereva George Ponela, Ali Mohamed (msaidizi wa dereva) na Mchungaji Patrick Mgaya ambaye anatajwa kuwa msaidizi wa marehemu Mtikila.Hata hivyo, baadhi ya watu waliozungumza na Gazeti la Uwazi juzi, nje ya Hosptali Teule ya Rufaa Mkoa wa Pwani, Tumbi walionesha kuwa na maswali kumi yenye utata juu ya ajali hiyo na kifo cha Mtikila.

SWALI LA KWANZA
Swali la kwanza lenye utata ni gari hilo kufika bondeni kwa kubiringika lakini mwonekano wake hautoi picha kwamba limebondeka kutokana na kulala na kuinuka mpaka lilipofika mwisho.


Mchungaji Patrick Mgaya aliyekuwa na aliyekuwa na marehemu wakati wa ajali
.

“Unajua kwa kawaida, gari likibiringika kutoka juu kwenda chini lazima litabondekabondeka. Nadhani mliona lile gari la yule msanii marehemu Sharo Milionea (aliyepata ajali, Muheza,Tanga). Pia mliona gari la marehemu Chacha Wangwe (aliyepata ajali Kongwa, Dodoma),” alisema mkazi mmoja Kibaha, Pwani.

SWALI LA PILI
Akaendelea: “Mimi nimeona picha ya marehemu halafu nimesikia maelezo ya mmoja wa waliokuwemo, eti marehemu alilaliwa na gari. Hivi mwili unaolaliwa na gari unakuwa vile jamani? Labda lakini, mimi si mtaalam sana wa miili ya ajali. Lakini naamini angekuwa na majeraha ya kukandamizwa.”

SWALI LA TATU
Naye muuguzi mmoja wa Hospitali ya Tumbi alishangazwa na dereva ambaye anashikiliwa na polisi na msaidizi wake kutoka salama kwenye ajali hiyo ya gari kubiringika.“Watu wengine sijui ni bahati au nini? Gari libiringike vile halafu utoke salama, inawezekana kweli? Au kwa sababu kila mtu ana siku yake ya kufa aliyopangiwa na Mungu,” alisema muuguzi huyo.

SWALI LA NNE
Uwazi lilizungumza na Mchungaji Mgaya, nje ya hospitali hiyo. Yeye kaumia kidogo kwenye paji la uso.
Kwa upande wake alisema: “Gari lililopata ajali lilikuwa la kukodi. Mtikila alikodi kutoka Dar kwenda Njombe na kurudi Dar. Wakati wa kurudi ndiyo tukapata ajali.”Lakini chanzo kingine cha jijini Dar kilipozungumza na Uwazi na kutajiwa aina ya gari, kilisema: “Hilo gari litakuwa la Mchungaj Patrick Mgaya.”

SWALI LA TANO
Mtu mmoja aliyejitaja kwa jina la Mike, alizungumza na Uwazi nje ya Ofisi za Global Publishers juzi mchana na kusema kuwa, Jumamosi usiku alimpigia simu Mtikila kwa mazungumzo yao, Mtikila akasema yupo Dar.
“Sasa kusikia eti kafariki dunia akitokea Njombe nimeshangaa sana. Kwa nini aliniambia yupo Dar wakati mimi si adui yake wa kunikwepesha ukweli?” alihoji Mike.


Ali Mohamed miongoni mwa wahanga wa ajali hiyo.

SWALI LA SITA

Kwa mujibu wa Mchungaji Patrick, wakati wanarudi, dereva wa gari hilo alikuwa akienda mwendo wa kasi mpaka Mtikila akawa na kazi ya kumwambia mara kwa mara, ‘we bwana mdogo punguza mwendo, utaleta matatizo bwana.’ Alikuwa akipunguza kisha anaongeza tena na Mtikila naye alikuwa akirudia tena kumsema.
Swali hapa ni kwa nini dereva alikuwa akipenda kuongeza mwendo licha ya kutahadharishwa? Kama Mtikila alikodi gari hilo si ndiye alikuwa bosi! Kwa nini dereva alikuwa hataki kumsikiliza bosi wake?


SWALI LA SABA
Eneo la Msolwa lina watu au wanakijiji. Mara nyingi inapotokea ajali, wanakijiji hujitokeza kwa wingi kushuhudia. Kwa nini wanakijiji wa Msolwa hawakujitokeza? Picha za eneo la ajali hakuna inayomwonesha mwanakijiji hata mmoja.

SWALI LA NANE
Namba za gari kuwa A (AGM) linazua maswali kwamba ni kweli lilikuwa na uwezo wa kutoka Dar hadi Njombe na kurudi Dar? Kwa tarakimu za sasa za magari ni D. Kwa hiyo A ni magari ya muda mrefu, 2007.

SWALI LA TISA
Mwili wa Mtikila ulikutwa umelala, shati alilovaa siku hiyo ni jeupe! Kama gari lilibiringikia bondeni, kwa nini shati lisichafuke?

SWALI LA KUMI
Pia wananchi walioona picha za mwili wa Mtikila wanahoji kwa nini mwili usiwe na majeraha, mchanga au vumbi?

KWA MUJIBU WA MCHUNGAJI MGAYA

Akizungumzia ajali hiyo kwa undani, Mchungaji Patrick Mgaya alisema:

“Tulikuwa tukitoka Njombe katika mkutano wa kisiasa. Tulipofika Msolwa, Pwani leo (juzi) alfajiri kama saa 11:45 tukiwa katika gari dogo tukapata ajali mbaya sana iliyosababishia kifo cha Mtikila, nasi tukawa tumepata majeraha.
“Ninachokijua ni kwamba, dereva wetu, George Ponela ambaye tulipewa katika gari hilo tulilolikodi alikuwa akiendesha kwa mwendo mkali hadi spidi mita 140 tukawa tunamkataza.
“Marehemu alikuwa akimkataza mara kwa mara, akawa anapunguza mwendo wakati fulani lakini akawa anarudia katika hali hiyo ya kuongeza.”



ILIVYOKUWA “Marehemu aliona ni jambo la hatari kwani linaweza kusababisha mauti lakini dereva hakumsikiliza. Tulipofika Msolwa, tukaona lori limesimama mbele yetu, dereva wetu akawa analipita. Ghafla akaona lori lingine mbele yake, ikabidi atoke nje ya barabara.

“Kusema kweli ile ajali nilishaiona kwa macho. Nikaamua kushika kiti cha marehemu na cha dereva maana nilikaa siti ya nyuma na msaidizi wa dereva. Wakati gari linapinduka, wenzangu wote walirushwa nje.
“Baada ya gari kutulia, nilitoka nje nikawaona wenzangu wakimtafuta Mtikila. Baadaye tulimwona chini ya gari, amelaliwa.”

NENO LA MWISHO LA MTIKILA
“Tulishirikiana kumtoa. Tulimkuta hajakata roho. Nikamuita mchungaji… mchungaji…mchungaji Mtikila. Neno aliloniambia la mwisho ni ‘BASI’. Akakata roho. Taarifa ikatolewa polisi tukachukuliwa na kuletwa hapa Tumbi.”

KUHUSU DEREVA
“Dereva anashikiliwa na polisi lakini sisi wawili tunapata matibabu hapa na Mtikila ndo’ hivyo katuacha na yupo mochwari. Kwa kweli mwendo kasi ulichangia na sijui ni kwa nini yule dereva alikuwa akikaidi amri ya Mtikila wakati gari lile lilikodishwa na yeye ni dereva tu siyo mwenye gari.”

Habari imeandaliwa na Makongoro Oging’, Issa Mnally na Haruni Sanchawa.

Comments