RUMAFRICA Magazine

RUMAFRICA FASHION

RUMAFRICA FASHION

BENKI KUU YATOA TAMKO WANAONUNUA SARAFU YA 500


Gavana wa Benki kuu, Benno Ndulu.

Stori: Hashim Aziz, UWAZI
Dar es Salaam: Kumekuwepo na madai ya muda mrefu mitaani kwamba sarafu za Sh. 500 zina madini yanayotumika kutengenezea vito vya thamani na kwamba hazipatikani kwa wingi kwenye mzunguko wa fedha kwa sababu kuna watu wanazinunua na kuzikusanya kwa ajili ya kazi hiyo, Uwazi limechimba ili kubaini ukweli wa madai hayo.

Uwazi lilianzia mitaani ambapo lilifanya mahojiano na wananchi wa maeneo mbalimbali nchini kutaka kujua kuhusu uelewa wao juu ya sarafu hiyo mpya.
Sarafu ya shilingi mia 500

“Nasikia zina madini yanayotumika kutengeneza mikufu na pete. Hapa mtaani kwetu nasikia kuna mtu anazinunua kwa wingi, ukiwa na sarafu moja, anakupa noti ya shilingi elfu moja mpaka elfu mbili,” alisema Jamal Mponji.

Wananchi wengine walioendelea kuhojiwa, walionesha kuwahi kusikia uvumi kwamba sarafu hizo zina madini na kukutana na baadhi ya watu waliokuwa wakizitafuta kwa lengo la kuzinunua kwa wingi.
Uwazi halikuishia hapo, lilifanya mahojiano na masonara kadhaa ambao ndiyo wanaotajwa zaidi kununua sarafu hizo, kuziyeyusha na kutengenezea vito vya thamani.

“Hata mimi huwa nasikiasikia lakini sijawahi kushuhudia kwa macho, mimi hapa huwa nanunua dhahabu na madini mengine, wakati mwingine nanunua vito na kuviyeyusha lakini sijawahi kutumia sarafu ya shilingi mia tano,” Ravji Singh, mfanyabiashara mwenye asili ya Kihindi anayeshughulika na kazi ya sonara, aliliambia Uwazi.

Baada ya kusikia kutoka kwa wananchi na masonara, gazeti hili lilifunga safari mpaka Makao Makuu ya Benki Kuu ya Tanzania (B.o.T) jijini Dar es Salaam ambayo kimsingi ndiyo yenye dhamana ya kutoa na kusambaza fedha zote za Tanzania.

Mwandishi wetu alikutana na jopo la wataalamu wa fedha wa benki hiyo, wakiongozwa na Mkurugenzi wa Huduma za Kibenki (Director of Banking), Marcian Kobello na kutoa ufafanuzi wa kina kuhusu madai hayo.
Mkurugenzi Kobello, alikiri kuyajua madai hayo lakini akaeleza kwamba huo ni uzushi wa mitaani ambao hauna ukweli wowote.

“Nawasahangaa watu wanaonunua sarafu za 500 kwa madai kwamba zina madini yanayoweza kutumika kutengenezea vito vya thamani. Kitaalamu, sarafu hiyo imetengenezwa kwa vitu viwili, chuma (steel) ambayo ni asilimia 94 na Nikeli (Nickel), asilimia 6. Huu mng’ao ambao ndiyo unaowachanganya wengi, ni madini ya Nickel na yamepakwa kidogo tu juu ya chuma.

“Hii ni sarafu ya kwanza kwa Tanzania kuwa na alama za usalama (security features), ukiitazama vizuri hapa (huku akionesha) kwenye hii alama inayosomeka 500, ukiigeuza kwa pembe fulani, utaona maandishi yanabadilika na kusomeka BOT.

“Bado naendelea kusisitiza kwamba hakuna madini yoyote kwenye sarafu hii yanayoweza kutumika kutengenezea vito vya thamani.

“Kinachosababisha zisipatikane kwa wingi mtaani, ni mazoea waliyonayo Watanzania zinapoingia fedha mpya kwenye mzunguko. Wengi hawapo comfortable (hawana raha) kuzitumia kwa sababu ya upya wake, wengine wanasingizia kwamba ni nzito kubeba.

“Lakini niwatoe wasiwasi wananchi, wazitumie kwa wingi ili wazizoee,” alisema.

Comments