RUMAFRICA Magazine

RUMAFRICA FASHION

RUMAFRICA FASHION

SI KUFA JUMAPILI WATU WASHANGAA MAITI IMEFUNGUA MACHO-MEJA JENERALI ASEMA




Meja Jenerali Mstaafu wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), Benjamin Noah Msuya (enzi akiwa kazini).


Oscar Ndauka, RISASI JUMAMOSI

DAR ES SALAAM: Kweli haya ni maajabu ya Mungu! Meja Jenerali Mstaafu wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), Benjamin Noah Msuya (74), ameanika kwamba, alifariki dunia na mipango ya mazishi ikafanywa lakini siku nne baadaye alifufuka, hapa anasimulia alichokiona baada ya kifo, fuatana na Risasi Jumamosi.

Akiwa na familia yake wakati akiugua.

AZUNGUMZA NA RISASI NYUMBANI KWAKE, DAR
Akizungumza na gazeti hili Machi 16, mwaka huu, nyumbani kwake, Kunduchi Beach jijini Dar es Salaam, Msuya ambaye mwaka 1979 aliongoza majeshi ya Tanzania kuingia Uganda kwa mara ya kwanza, alisema kifo chake hicho kilitokana na ugonjwa wa saratani (kansa).

MSIKIE MWENYEWE
“Awali ya yote, mimi kwa sasa ni Meja Jenerali Mstaafu. Lakini katika utumishi wangu, ndiye niliyeingiza majeshi nchini Uganda mwaka 1979 na kumwangusha mtawala wa mabavu, Idi Amini Dada (sasa marehemu).”

Meja Jenerali Msuya akiwa hospitali.

KUMBE ALIITAWALA UGANDA KWA SIKU 3
“Baada ya Amini kukimbia, nilikuwa mtawala kwa siku tatu nikimsubiri aliyetakiwa kuwa rais wa mpito, Yusuf Kironde Lule. Lakini sikuondoka Uganda, nikaja kusimamia kuingia madarakani kwa Rais Godfrey Lukongwa Binaisa. Lule alitawala kwa siku 68 tu.”

TATIZO LA UGONJWA WAKE
Akizungumza huku mkewe, Deborah Msuya akimwangalia kwa umakini, meja jenerali huyo alisema alianza kusumbuliwa na ugonjwa huo akiwa jijini Dar, Desemba, 2010 kwa kutoka uvimbe shingoni upande wa kulia. Alihangaika kwenye hospitali mbalimbali, ikiwemo ya taifa, Muhimbili bila mafanikio wala kuutambua ugonjwa.
Cheti cha kifo chake iliyothibitishwa na madaktari

WAZO LA KWENDA UINGEREZA
“Baada ya kubaini hali yangu inazidi kuwa mbaya na hospitali nchini zimeshindwa kubaini tatizo, nilikwenda Makao Makuu ya Jeshi (Upanga) kuonana na Mkuu wa Majeshi, Jenerali Davis Mwamunyange kutaka msaada wa kwenda kutibiwa nchini Uingereza.
“Sikumkuta, nikakaa ofisini kwake kumsubiri hadi alipofika, nikamwelezea. Mwamunyange alionesha kutoarifiwa kuhusu kuumwa kwangu. Lakini alianza hapohapo kutoa msaada kwa kumwita aliyekuwa Mnadhimu wa Jeshi, Luteni Jenerali Abraham Shimbo (sasa ni balozi nchini China) na kuweka kikao cha kujadili safari ya mimi kwenda kutibiwa Uingereza.”

SAFARI YA UINGEREZA
“Julai 3, mwaka huo mimi na mke wangu, tulisafiri kwenda Uingereza ambako tulipokelewa pia na mwambata wa jeshi, Brigedia Jenerali Pelegreen Mrope. Yeye aliniandalia siku iliyofuata kuonana na daktari wa London Clinic aitwaye Dk. Sheaves.”


VIPIMO VYACHUKULIWA
“Siku niliyokwenda, nilichukuliwa vipimo mbalimbali kama X-Ray, Ultra Sound na MRI (Magnetic Resonance Imaging). Lengo lilikuwa ni kubaini tatizo linalonisumbua. Wenzetu kule wako mbali sana kwa utaalam wa afya.”

Meja Jenerali Mstaafu, Benjamin Noah Msuya alivyo sasa.

MAJIBU YATOKA
“Ilikuwa Julai 25, mwaka huo ambapo majibu ya vipimo yalitoka. Hapo ni baada ya kuangaliwa kwa ustadi na Dk. Sheaves na daktari wa kliniki nyingine, anaitwa Dk. Peters wa Hospitali ya London Bridge.
“Vipimo vilionesha nina kansa. Hivyo nikakabidhiwa kwa mtaalam mmoja kwa ajili ya matibabu. Lakini pia nikawa natumia dawa mbalimbali.

ACHUKULIWA NA MTOTO WAKE, AFARIKI DUNIA
“Kuna siku, mtoto wangu anaishi kule anaitwa Bisala au Bis alikuja kunichukua hotelini nikaenda kwake kwenye Mji wa Birmingham ambako siku chache baadaye hali haikuwa nzuri, nikapelekwa kwenye Hospitali ya Heartland ambako Agosti 6, nilifariki dunia. Madaktari walithibitisha na kutoa hati ya kifo.”

NDUGU WAKAA KIKAO CHA MAZISHI, MAJIRANI WALIA
“Tayari mke wangu, wanangu wote na ndugu wengine walishapewa taarifa kwamba mimi nimefariki dunia. Hapa nyumbani, Tanzania, kuna jirani yangu aliposikia alikuja mbio hapa nyumbani huku analia.”

ALIKWENDA WAPI?
“Ndipo kwa siku nne nikapitia kwenye mazito. Mimi kwamba nilikufa sijui, bali nilijikuta nimeingia kwenye maeneo mawili. Niliingia mbinguni na pia niliingia kuzimu. Huko kuzimu kila nikikumbuka naogopa sana. Nilikuta watu maelfu kwa maelfu wakiwa kwenye ziwa la moto. Walikuwa wakilia kwa kuomboleza.
“Midomo na macho yao vilitoa moto. Kila sehemu ya mwili ilitoka moto. Nilipata bahati ya kumsikia Mungu akinena nami juu ya yale niliyokuwa nayaona kuzimu na mbinguni na kuniambia niwatangazie wanadamu wote.
“Mungu aliniambia niwaambie wanadamu kwamba hakuna hukumu. Wengi wanadhani kuna hukumu lakini ukweli ni kwamba hakuna hukumu bali kuna…”

KUTOKA KWA MHARIRI
Habari hii ni ndefu, aliyoyaona Meja Jenerali Msuya ni mengi sana na marefu. Amezungumza mengi na yaliyoandikwa hapa ni machache, ni kama kugusia tu.
Sasa mkasa mzima utaanza kutoka kwenye Gazeti la Risasi, Jumatano ijayo na kuendelea kwenye gazeti hili, Jumamosi ijayo.
Tunaahidi kuuandika mkasa huu wa kweli unaosimuliwa na mtu mzito kama yeye mpaka mwisho bila kubakiza neno hata moja, usikose- Oscar Ndauka, Mhariri Kiongozi Magazeti Pendwa, Global Publishers.

Msikie Meja Jenerali Mstaafu, Benjamin Noah Msuya


Comments