RUMAFRICA Magazine

RUMAFRICA FASHION

RUMAFRICA FASHION

UPENDO PENEZA: TAMASHA LA PASAKA LITAKEMEA MAUAJI

Na Mwandishi Wetu


Mhe. Peneza. ©Miwani Asilia Blog

Mbunge wa viti maalum wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) Upendo Peneza ameelezea uamuzi wa kupelekwa Tamasha la Pasaka mkonani Geita kuwa mzuri, kwani mkoa huo umekithiri kwa mauaji ya vikongwe na watu wenye ulemavu hivyo ni ishara kubwa ya kuelekea kukombolewa.

Peneza amesema kuwa anaamini watu wakimpenda Mungu wataacha kufanya mauaji ya vikongwe na watu wenye ulemavu wa ngozi pamoja na mauaji ya watu kwa ujumla, kwani mkoa huo unaongoza kwa mauaji ya aina hii.

Alisema Tamasha hilo ni msaada mkubwa kwa mkoa huo kwani litahamasisha na kupinga mauaji huku akisisitiza kuwa kampuni ya Msama ambayo inasifika kusaidia jamii anaiomba pia iwafikie hata watoto wa mitaani wa mkoa wa Geita.

“Tunamshukuru Msama na kamati yake kwani Tamasha linaweza kuwa msaada mkubwa kwa mkoa wetu mauaji yamezidi si kwa walemavu wa ngozi na vikongwe hata watu wa kawaida wanauwawa kwa mapanga na vitu vingine” alisema Peneza.

Alitolea mfano wa mauaji ya aliyekuwa Mwenyekiti wa mkoa wa Chadema, Alfonce Mawazo aliyeuwawa kwa kukatwakatwa mapanga hivyo kupitia tamasha la pasaka litawaasa waache mauaji.

“Kupitia hili Tamasha naamini wataacha vitendo hivyo kwa sababu Mungu anasema tusiue, mpende mwenzio, kwa hiyo mimi nadhani tamasha hili liwe la kihistoria kwa ajili ya kuwataka na kumrudia mungu,” anasema.

Peneza alisema asiwe Msama tu hata asasi, kampuni na wadau mbalimbali wajitokeze kupinga mauaji kwani hilo ni janga la kitaifa.

Comments