RUMAFRICA Magazine

RUMAFRICA FASHION

RUMAFRICA FASHION

KUTOIELEWA SHERIA YA MAKOSA YA MTANDAO KUTAWAPONZA WENGI


Tecno, Huawei na simu zingine za smartphone zenye bei chee zimewafanya watu wengi kuweza kufaidi ukuaji wa teknolojia. Lakini pia uwepo wa simu hizo, usingeweza kukamilika pasipo makampuni za mitandao ya simu hapa nchini kuboresha miundombinu ya internet.

Kwa sasa kila mwananchi, hata wale wa vijijini wana access na internet. Hadi sasa kwa mujibu wa mamlaka ya mawasiliano nchini, TCRA zaidi ya watanzania milioni 17 wanatumia internet. Ndio maana kuna ongezeko kubwa la matumizi ya mitandao ya kijamii hususan Facebook, Instagram na WhatsApp. Ni WhatsApp kutokana na umuhimu wake imetokea kuwa mtandao unaotumiwa na wabongo wengi.

Huko kuna makundi ambayo watu huchat, hutumiana video na picha kutaarifiana na mara nyingi kujifurahisha. Lakini pia ongezeko la matumizi ya simu, internet na mitandao ya kijamii imefanya kuwepo na matumizi mabaya na hivyo kupelekea kuanzishwa kwa sheria ya makosa ya mtandao.

Lakini bahati mbaya ni kuwa pamoja na Watanzania wengi kujua kuwa sheria hii inafanya kazi, hawajui ni makosa gani hasa yanayoangaliwa na yana adhabu gani. Ndio maana tukio lililotokea wiki hii huko Dakawa wilayani Mvomero, Morogoro la msichana aliyedhalilishwa kimapenzi na wanaume wawili na kumrekodi kisha kusambaza picha na video zake limewaponza wengi.

Ni kwasababu pamoja na kwamba watu hawa wanaodaiwa kuwa ex na mwingine mpenzi wa sasa wa binti huyo walitenda kosa la ubakaji, walikuwa hawajui kuwa kwa kumrekodi na kusambaza video na picha zake walikuwa wanazishika sharubu za sheria hii.

Kwa akili yake, Zuberi Thabiti, mpenzi wa msichana huyo aliamini kuwa kwa kumrekodi binti huyo akifanyiwa ukatili huo atakuwa amelipiza kisasi kwa usaliti anaodaiwa kufanyiwa baada ya mpenzi wake kutembea na dereva wake na maisha yataendelea kama kawaida.

Lakini kuna kundi jingine la watu ambalo limeponzwa na kutokujua kuwa kusambaza picha au video za aina hiyo ni kosa kisheria. Tayari polisi wanawashikilia watu 9 wengine (tofauti na wawili waliohusika kwenye tukio) kwa kusambaza picha hizo. Hawa wamevunja sheria ya makosa ya mtandao kifungu namba nne, kifungu kidogo (1) (a): Kifungu hicho kinasema:

14.-(1) Mtu hatachapisha au kusababisha
kuchapishwa kupitia katika mfumo wa kompyuta-
(a) ponografia; au
(b) ponografia yoyote iliyo ya kiasherati au chafu.

Sheria ya makosa ya mtandao imeweka adhabu kali zaidi katika mambo ya ponografia:

(2) Mtu atakayekiuka kifungu kidogo cha (1)
atakuwa ametenda kosa na akitiwa hatiani, atawajibika, iwapo ni uchapishaji kuhusiana na-
(a) ponografia, kulipa faini isiyopungua shilingi
milioni ishirini au kutumikia kifungo kwa
kipindi kisichopungua miaka saba au vyote kwa
pamoja; au
(b) ponografia iliyo ya kiasherati au chafu, kulipa
faini isiyopungua shilingi milioni thelathini au
kutumikia kifungo kwa kipindi kisichopungua
miaka kumi au vyote kwa pamoja.


Kwahiyo pasipokujua, watu wengi watajikuta wanafungwa ama kulipa faini kwa kusambaza video za matusi kwenye makundi yao WhatsApp wakitarajia kupongezwa kwa kuchangamsha ‘genge.’

Na Ponografia ni sehemu moja tu ya makosa ya mtandao. Makosa mengine ambayo Watanzania wanapaswa kujiepusha nayo ni pamoja na:

5. Kubaki katika mfumo wa kompyuta kinyume cha sheria.
6. Kuingilia mawasiliano kinyume cha sheria.
7. Kuingilia data kinyume cha sheria.
8. Ujasusi data.
9. Kuingilia mfumo kinyume cha sheria.
10. Kifaa kisicho halali.
11. Kughushi kunakohusiana na masuala ya kompyuta.
12. Udanganyifu unaohusiana na kompyuta.
13. Ponografia za watoto.
14. Ponografia.
15. Makosa yanayohusiana na utambuzi.
16. Kutoa taarifa za uongo.
17. Ubaguzi.
18. Matusi ya kibaguzi.
19. Mauaji ya kimbari na makosa dhidi ya binadamu.
20. Ujumbe unaotumwa bila ridhaa.
21. Ufichuaji wa taarifa za upelelezi
22. Kuzuia upelelezi.
23. Unyanyasaji kwa kupitia mtandao.
24. Ukiukaji wa haki bunifu.
25. Wakosaji wakuu.
26. Jaribio la kufanya uhalifu.
27. Kula njama ya kutenda kosa.
28. Ulinzi wa miundombinu muhimu ya TEHAMA.
29. Makosa yanayohusu miundombinu muhimu ya TEHAMA