RUMAFRICA Magazine

RUMAFRICA FASHION

RUMAFRICA FASHION

WATOTO WALIWA NA FUNZA BABA KUDAI NI DHAMBI KUUA KIUMBE CHOCHOTE


WAUMINI wa Kanisa la Holy Ghost Tebernacle katika Kaunti ya Murang’a Alhamisi walimvamia mshirika mwenzao waliyemshitumu kwa kuwatesa watoto wake na uvamizi wa funza kwa 'kukataa' kuwatafutia huduma za kimatibabu.

Washirika hao kutoka eneo la Kiamaihwa katika Kaunti ndogo ya Kigumo walidai kuwa muumini huyo wa kiume alikuwa akitii itikadi kali ambazo hupinga mauaji ya kiumbe chochote kilicho hai, wakiitaja kama “iliyopitwa na wakati”.

Pasta Joseph Mwaura wa Kanisa hilo aliambia Swahilihub kwa njia ya simu kuwa “watoto wawili wa muumini huyo wake walikuwa wamevamiwa na funza kila sehemu ya mwili na wakitembea ungedhani walikuwa wakicheza mchezo wa kuigiza uliohitaji wahusika kutembea kana kwamba wanacheza densi na kujikunakuna!”
“Baada ya kupata habari hizo, waumini wenzangu wakiwa zaidi ya 100 walimvamia muumini huyo alipowakataza kutekeleza uokoaji huo wa watoto wake na kisha wakamwamurisha awatoe watoto hao nje watolewe funza,” akasema.

Alisema kuwa watoto hao wote wakiwa ni wa kiume wa kati ya miaka 10 na 13 walikuwa wamevamiwa na wadudu hao na ikabainika kuwa hata hawakuwa wakienda shule.

“Waumini hao walikataa katakata kumsikiza baba watoto hao akisema kuwa walikuwa wakimtakia laana kutoka kwa Maulana ikiwa angewakubalia waue funza hao!"
Aliongeza kuwa aliteta vikali kuwa imani yake haingemruhusu kuua kiumbe yeyote aliyeumbwa na Mungu, akiongeza kuwa funza hao walikuwa wametumwa kukaa katika 'hekalu' - yaani miili ya wanawe.

Funza kutumwa
“Alituambia kuwa wadudu hao wametumwa ndani ya miili ya watoto wake na hakuna vile angeweza kupingana na tukio la kiroho. Alishikilia kuwa Mungu angewaamrisha watoke kutoka miili ya wanake atakapoamua kufanya hivyo,” akasema Pasta Mwaura.

Baba huyo alidaiwa kubishana kuwa imani ya waumini hao waliomvamia kwake ilifaa kuwa ya kulisha watu kiroho wala sio kutibu magonjwa au kutekeleza uokoaji wa watu kutoka na ukarimu wao kwa viumbe wa Mungu.

“Alitulaumu kwa kupotosha waumini kuwa madawa ya kizungu ni suluhu kwa magonjwa, akiyataja kama uchawi wa Kizungu!,” akateta Pasta Mwaura.

Aidha, bwana huyo alisisitiza kuwa hakuna mahali ndani ya Biblia ambapo Yesu alionekana akitafuta matibabu hospitalini.

Hata hivyo, ubishi wake haukumfaa kwa lolote kwa kuwa waumini hao walifanikiwa kuwaokoa watoto hao ambapo waliwatoa funza hao na hatimaye wakapakwa dawa ya kutibu vidonda.

“Aidha, waokoaji hao waliwapeleka watoto hao hadi hospitalini kwa matibabu zaidi ambapo walipewa dawa zaidi ya kupulizia nyumba yao
ili kuuwa wadudu wanaosababisha uvamizi wa funza,” akasema pasta Mwaura.

Alisema kuwa kuanzia Jumatatu ijayo watoto hao watasajiliwa shuleni na ambapo wamemuomba chifu wa eneo hilo kumwandama baba huyo ili atimize hilo.

“Wakati umefika kwa waumini wa Kikristo kutupilia mbali itikadi ambazo zimewasababishia ujinga, magonjwa na umasikini,” akasem