RUMAFRICA Magazine

RUMAFRICA FASHION

RUMAFRICA FASHION

MSAIDIZI WA ASKOFU GWAJIMA ATOA TAMKO KALI.



Waumini wa Kanisa la Ufufuo na Uzima, jana walisali bila kuwapo kwa Askofu wao,Josephat Gwajima ambaye anatafutwa na Jeshi la Polisi.

Mara nyingi Jumapili, Gwajima ndiye amekuwa akiongoza ibada katika kanisa hilo lililopo Ubungo Kibo, lakini jana iliongozwa na mchungaji Edward Adriano ambaye hata hivyo, hakueleza chochote kuhusu alipo askofu huyo.

Askofu Gwajima anatafutwa na polisi baada ya kusambaa kwa sauti inayosikika kama yake akitaka Rais mstaafu, Jakaya Kikwete afikishwe mahakamani kwa yote yaliyofanyika wakati wa utawala wake.

Jana, Kamanda wa Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Simon Sirro alisema suala la Askofu Gwajima atalizungumza leo.

Alhamisi iliyopita Polisi walizingira nyumbani kwa Gwajima kwa saa saba, wakitaka kumkamata bila mafanikio.

Kamanda Sirro alisema wanamtafuta askofu huyo ili athibitishe kama maneno yenye uchochezi, yanayosambaa kwenye mitandao ni ya kwake.

Ulinzi kanisani
Ulinzi katika kanisa hilo jana uliimarishwa na vijana waliovaa vizibao vya njano, vilivyoandikwa polisi jamii tii sheria bila shuruti. Idadi ya vijana hao wanaokadiriwa kufika 40, walikuwa wengi kuliko Jumapili nyingine zilizopita.

Licha ya kutokuwapo kwa askofu huyo kanisani hapo, waumini walijaa na wengine kukosa viti huku wengine wakionekana kusimama nje ya kanisa hilo.

Kauli ya Msaidizi wa Gwajima
Msaidizi wa Askofu Gwajima, Yekonia Bihagaze, kupitia ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa Facebook, alisema juzi kuwa taratibu, sheria na kanuni zinapaswa kufuatwa kumkamata kiongozi wao.

"Kanisa la Ufufuo Na Uzima ni makini, tulivu na halikurupuki kwenye maamuzi yake. Na nchi haiongozwi mitandaoni, kama serikali inamtaka mtu ziko taratibu, sheria kanuni za kuzifuata," sehemu ya taarifa ya Mchungaji Bihagaze ilisomeka."Kwa sasa kila mmoja anaona nchi inapiga hatua kimaendeleo, ni vema wananchi sasa tukaachana na propaganda kama hizi, ni vema tukaweka shabaha yetu moja kushirikiana na Rais tulijenge taifa Letu. Taifa hili si mali ya mtu mmoja, ni mali yetu sote kwa manufaa yetu na vizazi vingine vitavyokuja.

"Adui wa Rais wetu awe adui yetu sote. Siasa zitakuja tu baadaye ila kwa sasa nchi itulie, watu tuchape kazi, tulipe kodi kwa sababu kuna Rais mwenye nia ya kuipeleka mbele.""Hakuna duniani Taifa linaloweza kuendelea pasipo wananchi kushirikiana bega kwa bega na kiongozi wao."