RUMAFRICA Magazine

RUMAFRICA FASHION

RUMAFRICA FASHION

SUKWELI KUHUSU MAJI YA SUMU MGODINI

Mwananchi alivyobabuka kichwa na miguu.

Na Igenga Mtatiro,Uwazi
MARA: Sakata la maji machafu yanayodaiwa yana sumu kutoka mgodi wa dhahabu wa North Mara (Nyamongo) uliopo Wilaya ya Tarime, mkoani Mara, limeshika kasi baada ya Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo kuamua kuchukua sampuli za maji hayo na kuzipeleka kufanyiwa uchunguzi wa kimaabara katika nchi za Ujeruman, Ufaransa na Ubelgiji ili ukweli ubainike.
Prof. Muhongo alisema hayo hivi karibuni alipokuwa ziarani Tarime na akaongeza kuwa amefikisha taarifa za utata wa afya za wananchi hao kwa waziri wa afya ili kuchukua hatua za kuendesha uchunguzi wa afya za wakazi wa maeneo hayo.

Hatua ya Waziri Muhongo imekuja baada ya kukataa taarifa ya kamati yake iliyotolewa na Baraza la Usimamizi na Uhifadhi wa Mazingira (NEMC) katika kikao chake na wananchi wilayani hapa.
Kukataa kwake kulitokana na kushinikizwa na wananchi na mbunge wao John Heche wa Jimbo la Tarime Vijijini aliposema kuwa taarifa ya Wizara ya Mazingira na Muungano chini ya ofisi ya makamu wa rais, inasema kuwa maji yana sumu ambayo haikutajwa ni ya aina gani.

Mtoto alivyobabuka

“Mimi niliambiwa na Naibu Waziri wa Mazingira na Muungano, Luhaga Mpina kuwa ripoti yao ipo tayari na kilichokuwa kikisubiriwa ni karatasi ya watu wa TBS na kwamba maji hayo siyo salama na uchunguzi wa sempo hizo ulithibitishwa na mkemia mkuu wa serikali,’’ alisema Heche.
Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo akizungumza na waathirika wa tukio hilo.

Heche alifikia hatua hiyo baada ya kumuona Waziri Muhongo akiunda tena kamati ya watu 27 ili uchunguzi ufanyike upya na kamati hiyo ilikuwa inachunguza matatizo ya wananchi na mgodi katika vijiji vinavyozunguka mgodi huo iliyofanya kazi yake hiyo kwa mwezi mmoja tangu Februari 22 hadi Machi 22 na kukabidhi taarifa Machi 23, 2016.
Mama akitoa ushuhuda

Prof Muhongo alichukua hatua ya kuagiza uchunguzi ufanyike tena kwa usimamizi wa kamati yake hiyo baada ya kuona hali siyo shwari kwa kutoamini taarifa iliyotolewa katika kikao cha Julai 18, Mwaka 2016 na NEMC wilayani Tarime.

Mashaka yake hayo yalitokana na kujitokeza mama na mtoto wake aliyejulikana kwa jina la Ayubu Daniel wa miezi minane akiwa amebabuka ngozi kwa madai kuwa ni kutokana na kuathiriwa na maji ya sumu yanayotiririka kijijini hapo kutoka mgodin
Mama wa mtoto huyo, Neema Daniel mkazi wa Matongo alisema: “Mimi baada ya mtoto wangu kupatwa na hali hii, nilikwenda na kuonana na viongozi wa mgodi, ili wanisaidie matibabu, sikuweza kupata msaada wowote nimeendelea kuhangaika wakati sina hela,’’ alisema.
Hata hivyo, Msemaji wa Mgodi huo, Fatuma Msumi alijitokeza mbele ya kikao hicho na kukiri kuwa mama huyo alifika mgodini hapo mara baada ya mtoto wake kuugua akiomba msaada wa fedha za matibabu ambapo kampuni ilikubali kumsaidia lakini tatizo lake halikusababishwa na maji machafu.
Naye Boazy Range kutoka Kijiji cha Matongo alionesha madhara aliyoyapata kichwani na mikononi, baada ya kuoga maji hayo katika makazi yao.

Kwa utata huo licha ya Prof Muhongo kusema kuwa anachukua sampuli ya maji hayo maeneo yanayotiliwa shaka, alisema kwa usimamizi wa kamati yake hiyo, sampuli zake atapewa Mbunge John Heche naye apeleke kuchunguzwa maabara yoyote ile ili naye apate majibu yake na zoezi kama hilo afanye Mkuu wa Wilaya ya Tarime, Glorious Luoga.

Waziri Muhongo alichukua uamauzi huo baada ya taarifa ya NEMC iliyosomwa na Peres Joshua kutoka makao makuu ya ofisi hizo jijini Dar es Salaam kukataliwa na wananchi.
Licha ya wananchi wengi kujitokeza, walidai maji hayo huua mifugo ya wakazi wa Kijiji cha Matongo. Wananchi wa eneo hilo walidai kuwa sampuli ya maji hayo waliipeleka maabara ya Nairobi, Kenya na majibu yakatoka Machi 20, 2015 yaliyobaini kuwa yana sumu na hayafai kwa matumizi ya mifugo na binadamu.