RUMAFRICA Magazine

RUMAFRICA FASHION

RUMAFRICA FASHION

SOMO: UNDANI WA MAOMBI (13) - MCHUNGAJI GASPER MADUMLA






05. MIFANO YA WAOMBAJI WALIOFANIKIWA KATIKA MAOMBI.

Biblia imewataja waombaji wengi waliofanikiwa katika maombi yao,wote hawa wanatufundisha leo kwamba Mungu husikia maombi ya mwombaji. Wapo wengi ambao ni waombaji wazuri waliotajwa kwenye biblia,lakini leo nataka tuwatizame kwa ufupi waombaji saba akiwemo Yesu mwenyewe ingawa Yeye alikuwa Mungu. 

Tukianza kumuangalia Bwana Yesu,Yeye mwanzilishi wa imani yetu,alikuwa ni mwombaji aliyefanikiwa katika maombi yake,hali alikuwa Mungu. Tazama vyote vilikuwa katika uweza wake lakini hakuona fahali kuchukuliana navyo bali bado alidumu kuomba,hii ina maana kwamba Yesu,amefanyika kielelezo kwetu kutufundisha sisi namna ya kuishi kimaombi.

Bwana Yesu~Aomba zaidi ya mara tatu kwa siku,naye alifanikiwa katika maombi yake naye amekuwa kielelezo kwetu sisi na kwa kanisa la leo. Kabla ya kutenda chochote Yesu alizungumza na Mungu aliyemtuma kwanza,hata pale alipotaka kuwachagua mitume ilimbidi aombe,biblia inasema;

“Ikawa siku zile aliondoka akaenda mlimani ili kuomba, akakesha usiku kucha katika kumwomba Mungu.Hata kulipokuwa mchana aliwaita wanafunzi wake; akachagua kumi na wawili miongoni mwao, ambao aliwaita Mitume;” Luka 6:12-13.

Najifunza kwamba nami yanipasa kuomba kabla ya kufanya chochote kile. Nisifanye kwa matakwa yangu,bali kwa Bwana;soma pia Mathayo 14: 13,Mathayo 26:44,Marko 1:35,Luka 3:21,Luka 9:28 N.K

Ibrahimu.

Awali ya yote,biblia inamtaja Ibrahimu kama mtu aliyekuwa akimtumikia Bwana Mungu hata tangu ujana wake kipindi akiwa Harani( Yoshua 24:2-3). Mtu huyu alikuwa ni mwombaji endelevu aliyefanikiwa kwa maana waweza ona kila Mungu alipozungumza naye,alijenga madhabahu. Na moja ya kazi ya madhabahu ni kukutana na Mungu kwa njia ya maombi.

Ninampenda Ibrahimu jinsi alivyokaza katika imani na Mungu wake,tazama alipokaza kuomba kwa habari ya rehema juu ya Sodoma na Gomora( Mwanzo 18:23-33). Lutu na wanawe waliokolewa na ule moto si kwa sababu ya kuwa mwenye haki tu,bali kwa sababu ya maombi ya Ibrahimu kwa Mungu. Mwenye haki akaachwa,muovu akaangamizwa

Danieli.

Biblia inamuelezea Danieli kama muombaji aliyefanikiwa katika maombi yake,aliomba mara tatu kila siku (Danieli 6:10).Kilichomuokoa Danieli asiangamizwe na wabaya wake ni maombi aliyokuwa akiyafanya kwa maana alimtumikia Mungu daima naye Mungu akamuokoa kutoka katika tundu la simba wakali,tena aliokolewa katika tanuru ya moto (Danieli 3:23-26).

Kitu kimoja ninachokipenda kwa Danieli ni ile roho ya umoja katika maombi ( Danieli 2:17) ambayo leo wengi tumeikosa. Kuna kipindi huwezi kuomba mwenyewe yakupasa muwe pamoja na wenzako wenye shirika moja na wewe,kwa maana wawili ni wawili tu. Jifunze vile alivyofanikiwa Danieli aliposhirikiana na akina Hanania,Mishaeli na Azaria wenzake nao wakafanikiwa juu ya maombi yao.

Daudi.

Mara nyingi Daudi alikuwa akiwasilina na Bwana Mungu. Daudi alikuwa na moyo umpendezao Bwana,atakayeyafanya mapenzi yake yote (Matendo 13:22) Lakini pia soma Zab hii;“ Ee BWANA, uyasikilize maneno yangu,Ukuangalie kutafakari kwangu.Uisikie sauti ya kilio changu,Ee Mfalme wangu na Mungu wangu,Kwa maana Wewe ndiwe nikuombaye.“Zab.5:1-2

Eliya~“Eliya alikuwa mwanadamu mwenye tabia moja na sisi, akaomba kwa bidii mvua isinyeshe, na mvua haikunyesha juu ya nchi muda wa miaka mitatu na miezi sita.” Yakobo 5:17

Hana mkewe Elkana ( mama yake Samweli)~ Huyu alidumu katika maombi,hatimaye tunayaona matunda yake,Mungu akamjibu kwa kumpa mtoto mwanaume,Samweli (1 Samweli 1:12)

Paulo mtume~ Alifanikiwa sana katika maombi, ndio maana huduma yake ilikuwa kubwa kupita maelezo,biblia inasema: “ Ndugu zangu, nitakayo sana moyoni mwangu, na dua yangu nimwombayo Mungu, ni kwa ajili yao, ili waokolewe.”Warumi 10:1 

Kumbuka ukiwa moambaji mzuri,basi Mungu hujidhihirisha katika maombi yako, “ Ikawa babaake Publio alikuwa hawezi homa na kuhara damu. Paulo akaingia kwake, akaomba, akaweka mikono yake juu yake, na kumpoza.” Matendo 28:8

Tunajifunza nini kuhusu watu hawa wote waliokuwa waombaji?

~ Yapo mengi tunayoweza kujifunza,lakini kubwa zaidi tunajifunza kwamba Mungu hakuwaacha wale wote waliodumu kuomba daima…

Nipigie sasa kwa maombezi kwa +255 655 111 149,+255 684 033 334 au +255 762 414 446. 

ITAENDELEA…

Mchungaji G.Madumla.

Beroya bible fellowship church(Kimara,Dar,TZ)

UBARIKIWE.