RUMAFRICA Magazine

RUMAFRICA FASHION

RUMAFRICA FASHION

GONDWE AKAMATA MALORI SABA YAKISAFIRISHA MADINI USIKU!

Handeni, Tanga;

Mkuu wa Wilaya ya Handeni mkoani Tanga, Godwin Gondwe amekamata malori saba yakisafirisha madini ya chuma aina dolomite yanayotumika kutengeneza saruji.

Gondwe amesema kati ya malori saba walifanikiwa kukamata matano, huku mawili madereva wakiwahi kutoroka. “Malori hayo yalikuwa yanatokea Kata ya Mgambo, yanakochimbwa madini hayo,” amesema.

Kufuatia hatua hiyo, Gondwe ametangaza kupiga marufuku usafirishaji madini usiku.

“Tulipokamata magari hayo, kwanza tuliwauliza kama wamelipa kodi na kama wamelipa watuonyeshe stakabadhi,” amesema.

Alisema madini yanapo safirishwa nje ya wilaya mfanyabiashara anatakiwa kuilipa Serikali Kuu asilimia tatu na halmashauri inatakiwa kulipwa asilimia 0.3 ya mauzo.

Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya hiyo, William Makufwe amesema wamekuwa wakipoteza mapato kupitia wafanyabiashara wanaokwepa kulipa kodi.

Makufwe amesema wameanza kukusanya kodi kwa kutumia wataalamu wao na kuachana na mawakala, ambao walikuwa wanawasilisha fedha kidogo.

Meneja wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) wilaya za Handeni na Kilindi, Charles Kamuhanda alisema kumekuwa na changamoto ya ulipaji kodi kutoka kwa wafanyabiashara.