RUMAFRICA Magazine

RUMAFRICA FASHION

RUMAFRICA FASHION

HILLARY CLINTON AFUTA ZIARA BAADA YA KUUGUA



NEW YORK, MAREKANI

MGOMBEA urais wa Chama cha Democratic nchini Marekani, Hillary Clinton, amefuta mkutano wake wa kampeni katika Jimbo la California, baada ya kuugua kichomi.

Clinton amechukua hatua hiyo baada ya kugundulika anaugua ugonjwa huo wa mapafu, ambao pia hujulikana kama nimonia.

Dalili zake ni pamoja na kukohoa, homa, uchovu, baridi na kutatizika wakati wa kupumua.

Juzi Jumapili Clinton alilazimika kuondoka mapema kutoka kwenye hafla ya kuwakumbuka waathirika wa shambulio la kigaidi la Septemba 11 jijini New York.

Hafla hiyo ilikuwa ya kuadhimisha miaka 15 tangu kutokea kwa shambulio hilo lililosababisha vifo vya karibu watu 2,900.

Saa chache baadaye, madaktari wake walisema alikuwa amegunduliwa kuwa anaugua ugonjwa wa kichomi siku mbili awali na kwamba alipewa dawa na kushauriwa kupumzika.

Baada ya kuondoka kwenye hafla hiyo, ambapo video zilionesha Clinton akisaidiwa kutembea, alipelekwa nyumbani kwa binti yake, Chelsea, jirani na eneo la tukio.

Maofisa wake walisema alikuwa amezidiwa na joto mwilini.

Alitokea baadaye na kuwaambia wanahabari: “Najihisi vyema kabisa. Ni siku nzuri hapa New York.”

Baada ya hapo alielekea nyumbani kwake Chappaqua, New York.

Daktari wake, Lisa Bardack, alisema mgombea huyo amekuwa akitatizwa na kikohozi ambacho kinahusiana na mzio.

Clinton alikuwa amepangiwa kuelekea California jana kwa ziara ya siku mbili, ambapo miongoni mwa mambo mengine angehudhuria mikutano ya kuchangisha fedha na pia kutoa hotuba kuhusu uchumi.

Viongozi wa Chama cha Republican tayari wameanza kuibua maswali kuhusu uwezo wake kiafya wa kuhudumu kama amiri jeshi mkuu.

CREDIT: MTANZANIA