RUMAFRICA Magazine

RUMAFRICA FASHION

RUMAFRICA FASHION

09.10.2016: MCH. ELIZABETH LUCAS WA KANISA LA MLIMA WA MOTO AFUNDISHA JUU YA ROHO MTAKATIFU SIKU YA JUMAPILI


Mch. Elizabeth wa Mlima wa Moto Mikocheni “B” kwa Bishop Dr. Gertrude Rwakatare siku ya Jumapili 09.10.2016 aliweza kufundisha mengi katika kipindi cha Sunday School, lakini sisi tumechukua sehemu tu ya mafundisho yake ili ubarikiwe, alikuwa na haya ya kusema, “Tusome Yohana 8:31-32 Basi Yesu akawambia wale Wayahudi walio mwamini, Ninyi mkikaa katika Neno langu mmekuwa wanafunzi wangu kwelikweli. 
Tena mtaifahamu kweli, nayo kweli itawaweka huru”. Tunafundisha kweli ya Mungu. Kweli ni Neno la Mungu, pasipo Roho Mtakatifu, huwezi ukarijua Neno la Mungu, huwezi ukarifahamu hata ukiwa ukisoma unaona ni gumu kuelewa maana yake ni nini. Ukienda kwenye Agano la Kale unakuta, majina ni mengi mengi unmashindwa hata kuelewa unachosoma, lakini Neno la Mungu linasema, “Tazama ya kale yamepita tumekuwa wapya”. 

Siku ya leo muhitaji sana Roho mtakatifu akae ndani yako ili aumbe maisha mapya, ili akupatanishe na Mungu, ili akuongeze siku za kuishi, ili utembee na Bwana, ili uwe mshindi katika ulimwengu huu. Tembea na Roho wa Mungu usikubali kuchakachuliwa wokovu wako mwambie Roho “Fanya kiota ndani yangu”, unajua kiota kikikaa ndani ya moyo, Roho mtakatifu anarusha teke, saa zote ni kuishi maisha matakatifu. Ndani ya moyo wa mwanadamu Roho mtakatifu ni wa muhimu. Hili kanisa la Bwana ili lijae nguvu za Mungu ni lazima tuzae Roho mtakatifu, sema Roho mtakatifu nina kuhitaji kaa ndani yangu

Wapendwa, ukitembea na Roho wa Mungu, hata kama itakuja misukosuko ya jinsi gani wewe utatoka mshindi. Mungu akikaa ndani yako hatakama mtu alikuwa anakuvizia Roho wa Mungu atakwambia, “Usipite eneo hili”, Roho wa Mungu atakuamsha usiku kukwambia, “Kunajeshi linakuja kukuvamia amka anza kukemea, anza kupiga vita”, kwa maana Roho wa Mungu akikaa ndani yetu anaona yote ambayo sisi hatuoni kwa jinsi ya mwilini, na kwajinsi hiyo wachawi wanatuogopa wanasema, ”Sisi ni wachawi”. maana yake wanaona tumevunjavunja, tumeharibu, tumebomoa kazi zao si kwa nguvu ya mwili, si nguvu ya damu, si nguvu ya mwili yenzye uzito wa kilo mia, bali kinacho bomoa na kuharibu kazi za ibilisi ni nguvu ya Roho inayo kaa ndani yako. 

Nataka leo uipokee hiyo nguvu ya Roho uweze kuwa mtu fulani ambaye ukipita mtaani wanasema, “Hakika wokovu upo, hakika yupo Mungu atendaye.” Watu wanaokufuatilia waseme, “Huyu hawezekani sijui amempata mganga wapi?” Sisi tuliokoka mganga wetu ni Roho Mtakatifu. Ulimwengu watu mtaani, ofisini watakushangaa, na wakitaka kukuwekea kitu kibaya ili kikuangamize wanapigwa shoti, mikono yao inapigwa ganzi, vile vibaya wanavyotaka vije kwako vinaanguka chini, maana pale unapoingia asubuhi ofisini unamkabizi Roho mtakatifu kiti chako

Kila siku unatakiwa kumkadhii Roho mtakatifu meza yako ya ofisini, ofisi yako yote usiingie kichwa kichwa ofisini, kwenye biashara yako, mwambie Roho Mtakatifu, “Kamata biashara yangu na yoyote anayekuja akiwa na nia mbaya akutane na moto umteketeze, umuangamize, yoyote mwenye nia mbaya asisogee eneo lako la kazi au biashara, nampofusha katika ulimwengu wa Roho, ninampiga upofu anapotaka kuniletea mabaya macho yake yasione”, umwambie, ‘Roho Mtakatifu yeye ndiye mtetezi mkuu”, ambaye Mungu ndiye ametuachia siku ya leo. 
Mtamani Roho Mtakatifu wewe huwezi vita, vita vyetu sisi ni katika ulimwengu wa Roho. Wana wa Israel walipo kuwa safarini walikutana na vikwazo vingi, mataifa mengi walikuwa wanawapinga, lakini hakikubadilika kitu. Safari hii tunayoiendea kunavikwazo vingi njiani lakini Roho Mtakatifu akiwa pamoja nasi tutapita ndiyo maana Paul anasema, “Mimi ninayaweza mambo yote katika yeye anitiie nguvu”. Wewe pita pamoja na Roho Mtakatifu yeye ndiyo msaada wako, yeye ndiye anajua hatima ya maisha yako, hakuna kitakacho kutesa, hakuna kitakacho kushinda Roho wa Mungu akiwa katikati yako. Roho wa Mungu akiwa katikati yako kila kitu kinawezekana na atakuongoza katika njia sahihi. 

Tumejifunza habari za Roho Mtakatifu ya kwamba, Roho mtakatifu ni nafsi katika utatu wa Mungu. Mungu ni mmoja anayetenda kazi katika nafsi tatu. Huwezi ukambagua Roho Mtakatifu, Yesu Kristo , Baba ukamuweka pembeni, kwani hawa ni wamoja wanatenda kazi kwa umoja tunaona hata katika ubatizo wanabatizwa katika jina la Baba na la Mwana na la Roho mtakatifu. Mungu hutenda kazi katika umoja unaitwa ni Utatu Mtakatifu. Maandiko yanasema katika 1Yohana 5:8, “Kwa kuwa wako watatu washuhudiao mbinguni , Baba na Neno na Roho mtakatifu na watatu hawa ni umoja”. 

Kanisa la Bwana tunahitaji kuwa na Umoja, tunahitaji kushirikiana, tushikamane maana maandiko ya Bwana yanasema, Yesu akasema, “Baba nawaombea hawa ninapo ondoka, wakawe na umoja kama mimi na wewe Baba tulivyo na umoja”, nalo kanisa liwe na umoja ili tuweze kushinda, tusiweke mianya ndani ya kanisa, lazima tuwe na umoja kama Baba na Mwana na Roho Mtakatifu walivyo na umoja, tusiweke ubaguzi katikati yetu tupendane sisi kwa sisi, tuinuane sisi kwa sisi, tutiane moyo sisi kwa sisi hata watu wa dunia wanatamani maisha wa watu wa Mungu. Pasipo Roho wa Mungu huwezi ukalisoma neno la Mungu akalielewa, huwezi ukaomba kwa muda mrefu maana watu wengine wanasema kuna karama watu wengine wanasema, “Wamepata karama ya maombi” lakini mimi sijawahi kuona karama ya maombi ni Neema tu

Kuna baadhi ya watu wanaweza kuomba masaa kadhaa, wanapiga magoti wanaomba lakini kwa kawaida Roho Mtakatifu ndo anayetuwezesha katika kuomba, yeye ndiyo anatutia nguvu katika maombi. Ukikaa ukatulia Kwake Roho Mtakatifu atakuwezesha hata kama ulikuwa unaomba kwa dakika 10 utakuta unasogea kwa viwango vya Mungu kwa sababu Roho wa Mungu yupo ndani yako atakuwezesha kuomba hata kwa saa moja kwa sababu tunaenda naye hatua kwa hatua. Pia pasipo Roho Mtakatifu huwezi kuwa na upendo wa Kimungu ndani yako. Roho Mtakatifu anatuumba, anatutengeneza na hata upendo ni hivyo hivyo. Roho Mtakatifu akiwa ndani yetu anaumba upendo wa Kimungu ndani yetu tunapendana tunawapenda watu wote.