RUMAFRICA Magazine

RUMAFRICA FASHION

RUMAFRICA FASHION

RIPOTI KUTOKA MPEKUZI HURU BLOG: MCHUNGAJI RWAKATARE KUWATOA WAFUNGWA WENGIINE 43 GEREZANI KWA KUWALIPIA FAINI ZAO


Mchungaji Kiongozi wa Kanisa la Assemblies of God (Mlima wa Moto), Getrude Rwakatare amesema ataendelea na mpango wake wa kuwanusuru wafungwa wanaotumikia adhabu magerezani kwa kuwalipia faini ili warejee uraiani.

Akizungumza na waandishi wa habari jana Dar es Salaam, alisema katika awamu ya pili ameamua kuwalipia wafungwa 43 waliopo katika magereza ya Mkoa wa Dodoma.

“Kampeni hii ya kuwalipia faini kati ya Sh 50,000 hadi 200,000 wafungwa waliopo magerezani imetupa moyo na Watanzania wengi wameguswa na hata kutupongeza. Kutokana na hali hii kanisa letu sasa limefanya hivyo tena na safari hii tunaelekea mkoani Dodoma,” alisema.

Mchungaji Rwakatare alisema kesho watawatoa wafungwa hao mkoani Dodoma ambapo vigezo walivyoangalia ni wanawake wanaonyonyesha, wagonjwa na wazee.

“Nasi tunatimiza maandiko ya Mungu katika kufanya hivi na kuunga mkono juhudi za Mwenyekiti wa Parole, Augustino Mrema,” alisema Mchungaji Rwakatare.

Alisema kutokana na makosa mbalimbali ya faini waliohukumiwa nayo wafungwa hayo, kanisa lao limetoa Sh milioni 6.8 kwa ajili ya kulipia faini hizo.

Awali Rwakatare kupitia kanisa lake, aliwalipia wafungwa 78 katika magereza matatu ya Keko, Segerea na Ukonga ya jijini Dar es Salaam na kuachiwa huru baada ya kulipa faini ya Sh milioni 25 zilizochangwa na waumini wa kanisa hilo.

CHAMZO: MPEKUZI HURU