RUMAFRICA Magazine

RUMAFRICA FASHION

RUMAFRICA FASHION

UMUHIMU WA CHANJO KWA WATOTO

Mtoto akipewa chanjo ya Polio
Shirikisha

Mamilioni ya watoto wa chini ya umri wa miaka mitano wamepewa chanjo katika wiki ya mwisho ya mwezi Aprili kote duniani.
Kenya imekamilisha wiki moja ya Chanjo ya kitaifa kwa watoto ambayo kulingana na shirika la afya duniani W.H.O. Chanjo hiyo inatolewa katika wiki ya mwisho ya mwezi Aprili. Wiki ya mwisho ya mwezi Aprili imeshuhudia mamillioni ya watoto kote duniani wakipokea chanjo dhidi ya magonjwa mbali mbali, yanayoathiri watoto.

Wiki hii ya chanjo inatambuliwa na shirika la Umoja wa Mataifa kwa ajili ya watoto-UNICEF. Shirika la afya duniani-W.H.O. linakadiria kuwa watoto wachanga million 22 hawapati chanjo inayostahili, ambapo zaidi ya million 1.5 walio na umri chini ya miaka 5 hufariki kutokana na magonjwa yanayoweza kuzuiwa kupitia chanjo.

Chanjo ina tiba ya kuaminika, na wataalamu wanasema inaweza kuzuia vifo kati ya million 2 na million 3 kila mwaka. Lakini ripoti ya takwimu za UNICEF inasema kwa kifupi mtoto mmoja kati ya 5 hajapokea chanjo, hasa katika mataifa yanayokabiliwa na changamoto nyingi au mgogoro wa kisiasa.

Utafiti unaonyesha kuwa watoto kutoka familia zenye kipato cha juu, au matajiri, wanapata huduma bora za matibabu, pamoja na chanjo na dawa nyingine za kutibu magonjwa. Serikali ya Kenya inajaribu kuondoa au kupunguza tofauti hiyo ya kitabaka, kwa kuhakikisha kila mtoto anapata huduma bora.

Shirika la UNICEF linasisitiza kuwa kila nchi inahitaji mchango wa kisiasa katika kusambaza huduma za chanjo kwa watoto wengi, hasa katika familia maskini na sehemu kame zaidi.

Huko Kenya kampeni hiyo imefanikishwa kupitia mashirika ya kijamii na Vyombo vya habari, ili kusaidia kuondoa jamii nyingi kutoka mila na tamaduni potofu ambazo hukataa au kupuuza manufaa ya Chanjo.

Kenya imo katika hatua za mwanzo za mfumo mpya wa serikali za ugatuzi, ambazo zimepewa jukumu pia la kuboresha elimu na afya kwa kila mwananchi.
Chanjo kwa kila mtoto aliye na umri chini ya miaka mitano ni kati ya mikakati hiyo, ambapo maudhui kuu ya mwaka huu ni kuhamasisha kina mama umuhimu wa kuwapa watoto wao Chanjo.

Kongamano la kimataifa kuhusu chanjo pia limekuwa likiendelea Abu Dhabi, ambako shinikizo limetolewa kwa wahusika kushauriana na wanaotengeneza dawa za chanjo, kupunguza gharama kubwa iliyopo ili kuwafikia wasio na uwezo duniani.