RUMAFRICA Magazine

RUMAFRICA FASHION

RUMAFRICA FASHION

WAPINZANI KENYA WAMKUBALI JPM

Rais Dkt. John Pombe Magufuli.

Utendaji kazi wa Serikali ya awamu ya tano chini ya Rais Dkt. John Pombe Magufuli umetajwa kuwa sababu ya Rais Magufuli kupata umaarufu pamoja na kusifiwa na wananchi wengi wa nchi jirani hususani nchini Kenya.

Mwenyekiti wa Chama cha upinzani cha Labour Part of Kenya (LPK), Ababu Namwamba amesema kuwa, kilichompa umaarufu Rais Magufuli ni harakati zake za kupambana na ufisadi sambamba na kupunguza gharama za matumizi ya umma.

“Rais Magufuli anasifa fulani kule Kenya, mfano kumekuwa na harakati za kupambana na ufisadi, kupunguza gharama za shughuli za umma, hilo ndilo lililompa umaarufu, jina lake si geni masikioni mwa Wakenya. Swali, je haya mambo tunayoona katika vyombo vya habari ni porojo au kweli? Au yanabadili hali ya maisha ya wananchi wake?”

“Kenya tungependa kuona katika takwimu hali ya maisha imebadilika Tanzania, huduma za kijamii kama maji, afya na elimu zimeimarika. Pia ufisadi unapungua, lakini hadi sasa hatujaweza pata takwimu zinazoonyesha hayo mambo yanabadilika.”

Namwamba amesema ufisadi ni jambo la kupambana nalo, ambapo amemshauri Rais Magufuli kuendeleza vita hiyo ili ukuaji wa uchumi wa nchi uende sambamba na ukuaji wa uchumi wa wananchi na si kwa watu wachache.

“Ushauri wangu kutoka Kenya ni kuwa, siasa za nchi hizi mbili zinakaribiana sana, ila katika mashindano ya kisiasa tofauti iliyopo na ambayo nilipenda muitilie maanani ni kukwepa ukabilia, kutofanya siasa za kikabila na viongozi kutofanya makabila kama mtaji wa kisiasa, Kenya wanasiasa wamesababisha ubaguzi na kuleta suala la ukabila na nisingependa kuliona hili Tanzania, bali tulete siasa za sera, dhana, zitakazoleta huduma bora za kijamii,” amesema.