RUMAFRICA Magazine

RUMAFRICA FASHION

RUMAFRICA FASHION

AFYA YAKO: UMUHIMU WA KUPIMA AFYA- 3

Je Kuna umuhimu gani wa kupima afya mara kwa mara?
Watu wengi huenda kupata huduma ya afya pale wanapokuwa hawajisikii vizuri au wana tatizo la kiafya linalowasumbua. Kuna magonjwa makubwa ambayo hayaonyeshi dalili zozote hadi pale yanapokuwa yameshaenea au yameleta athari kubwa mwilini, hata kusababisha kifo ghafla. Magonjwa haya ni pamoja na ugonjwa wa moyo, shinikizo kubwa la damu, kisukari, saratani n.k Kuwa na utaratibu wa kupima afya yako mara kwa mara kwani kuna manufaa yafuatayo:-

1. Ugonjwa unaweza kugundulika mapema na hivyo kuweza kutibika.

2. Kugundua kama uko katka hatari ya kupata au una viashiria hatarishi (risk factors) vya magonjwa sugu. Kwa mfano unaweza kugundulika kuwa una lehemu nyingi mwilini au shinikizo la damu limepanda. Viashiria hivi visipogundulika mapema na kudhibitiwa vinaweza kusababasha mtu kupata magonjwa ya moyo.

3. Ni fursa nzuri kuweza pia kujadili na kumwambia daktari yale matatizo madogo madogo ambayo ulikuwa huoni umuhimu wa kwenda hospitali lakini huathiri afya na maisha. Wakati huo unaweza kupata ushauri unaotakiwa na kuboresha afya na maisha yako.

Je, kwa kawaida ni mara ngapi natakiwa kupika afya yangu na vipimo gani hifanyika?

Inashauriwa kupima afya yako angalau mara moja kwa mwaka. Hata hivyo, kama mtu ana viashiria hatarishi vya kupata magonjwa sugu mtaalam wa afya atamshauri ni mara ngapi apime afya yake.

Kuna mambo ambayo ni muhimu katika umri wowote ni mengine ni muhimu zaidi katika umri mkubwa. Kupima afya hutegemea umri na jinsi. Ni vyema kumuuliza daktari wako kuhusu vipimo unavyotakiwa kufanyiwa. Viafuatavyo ni baadhi tu ya vipimo muhimu:-


1. Sukari; Aina hii ya kipimo inatakiwa kufanyika kila baada ya miaka miwili hadi mitatu kwa mwaka mwenye umri wa miaka 40 au zaidi inashauriwa kufanya vipimo mara kwa mara.


2. Lehemu: Inashauriwa kipimo hiki kifanyike baada ya miaka miwili hadi mitatu kwa watu wenye umri wa miaka 40 au zaidi inashauriwa kufanya vipimo mara kwa mara.


3. Shinikizo la Damu: Kipimo hiki kinahitajika kufanyika kila mara unapokwenda hospitali. Hata hivyo, inashauriwa kufanyiwa kipimo hiki zaidi ya mara mbili kwa mwaka.


4. Moyo: Watu wenye umri zaidi ya miaka 40 wanashauriwa kufanya kipimo hiki mara kwa mara.


5. Uzito wa Mwili: Kipimo hiki hakina wakati maalum; hata hivyo unatakiwa ufuatilie uzito wako zaidi ya mara mbili kwa mwaka.


6. Saratani ya Matiti: Wanawake wanashauriwa kwenda hospitali kufanyiwa uchunguzi wa matiti kwa njia ya x-ray (mammogram). Mara nyingi wataalam wa afya wanashauri mwanawake aliye na umri wa miaka kati ya 20-30 afanyiwe kipimo hiki kila baada ya miaka mitatu na yule mwenye umri wa miaka 40 na zaidi afanyiwe kipimo hiki kila mwaka. Vile vile mwanamke yeyote mwenye umri kuanzia miaka 20 anatakiwa kujua na kujichunguza matiti yake mwenyewe kila mwezi.

Kipimo cha Uzito

7. Shingo ya Kizazi: Wanawake kuanzia miaka 20 na kuendelea wanashauriwa kufanyiwa vipimo vya pap-smear au Visual Inspection of Acetic Acid (VIA) ili kuchunguzwa hali ya saratani kila baada ya miaka mitatu.

8. Tezi ya Kiume: kwa wanaume chini ya umri wa miaki 40 mara nyingi inashauriwa kufanyiwa kipimo kila baada ya miaka miwili au zaidi.Kwa wanaume walio na umri zaidi ya miaka 40 inashauriwa wafanye kipimo hiki kila mwaka.

9. Utumbo Mpana: Inashauriwa kufanyiwa vipimoutumbo mpana kila baada ya miaka mitano kwa watu wenye umri wa miaka 50 na zaidi.

10. Kizazi: Mara nyingi aina hii ya saratani haifanyiwi uchunguzi wa kawaida ila tu kwa wale wanawake wenye historia ya ugonjwa huu katika familia. Hata hivyo mwanamke akiona anatokwa na damu nyingi kuliko kawaida wakati wa hedhi, basi amuone daktari mapema kwa ushauri.