RUMAFRICA Magazine

RUMAFRICA FASHION

RUMAFRICA FASHION

ANZA NA FIKIRA KWANZA KAMA UNATAKA MAFANIKIO.

Ni muda sasa hapa nchini kila mtu amekuwa akizungumzia juu ya neno mabadiliko na kweli tumeona mabadiliko katika Nyanja mbalimbali za maisha yetu, iwe zile za upashanaji habari, usafiri, huduma za afya, kilimo n.k. lakini katika mabadiliko yote haya kuna kitu ambacho unatakiwa kukijua nacho ni fikira.
Kama unataka mafanikio ya kweli na umeamua kufanya mabadiliko basi anza na mabadiliko ya akili,sababu moja kwa nini ngozi nyeupe ilitutawala kirahisi sisi ngozi nyeusi au waafrika, ni kwasababu wazungu walipokuja kitu cha kwanza walianza kuzibadili fikira zetu na kutufanya tuanze kuwaona wao ni bora kuliko sisi, hivyo sisi tukawa tunaona raha sana kuwatumikia wao na hatimae wakatutumia mpaka wakafanikiwa kwa kiwango walichokuwa wanakihitaji na sisi tukawa masikini. Lakini yote hii ni kutokana na fikira zetu kubadilishwa.


Mtu anae oa au kuolewa kama anataka ndoa yake iwe yenye mafanikio na imara na bora ni lazima abadili fikira zake kutoka kule alikokuwa yaani alikuwa sio mke au mume wa mtu na sasa ni mke au mume wa mtu. Lakini hapa pamekuwa na utata na udanganyifu mkubwa kwa kuwa sio wote wanaobadili fikira ndio maana huko nyuma nilishawahi kusema kuwa ukitaka kufanikiwa basi hakikisha kuwa akili na mwili wako vinaenda sawa au sambamba. Hivyo kama unaoa au unaolewa basi hakikisha kuwa unabadili fikira za kutoka kule ulikokuwa na kuwa kwenye ndoa.

Mabosi wengi sana wamekuwa wikwalaumu wafanyakazi juu ya utendaji kazi wao, na wengine huenda mbali zaidi na kuwafukuza au kuwasimamisha kazi wafanyakazi wao pindi wanapoonekana wamekwenda kinyume na maagizo ya viongozi hao. Na hii hutokea mara nyingi pale bosi anapoleta utaratibu mpya. Lakini mabosi hawa wanasahau kitu kimoja ambacho ni fikira za wafanyakazi, wamezibadili vipi ili wafanyakazi hawa waendane na mifumo mipya. Kama wewe ni bosi na unataka mabadiliko katika kampuni au ofisi yako anza kwa kuwaandaa wafanyakazi wako kifikira kwanza.

Watu wengi saizi tumekuwa tukishabikia tu kila tunalo liona bila kujali jambo lile linaweza kutuathiri vipi au kutunufaisha vipi na ndio maana hatuko tayari kubadili fikira na hata kama tukionekana tumefanya mabadiliko lakini mabadiliko haya huonekana ni kama hayana tija kwa kuwa tunafanya mabadiliko nje na ndani tunakuacha. Mfano leo hii kila mtu anashabikia kauli mbiu ya hapa kazi tu lakini muulize yeye anafanya kazi gani?, utashangaa kumsikia hana kazi yoyote, mtu kama huyu unakuta amebadilika nje lakini sio ndani na hapa ndipo matatizo huanza. Anza na fikira kama unataka mafanikio.

Fikira ndio kila kitu katika maisha ya binadamu aliyegundua simu kama njia ya mawasiliano, alibadili fikira zake kutoka kule kwenye barua na kutafuta njia ya aina nyingine ambayo ni simu. Kama leo hii unataka kupata mafanikio ya ukweli basi hakikisha kuwa fikira zako umezibadili kutoka katika yale uliyokuwa unayawaza mwanzo na kwenda kwingine.

Watu wengi hupata mafanikio lakini baada ya muda mfupi mafanikio hayo hupotea. Ulishawahi kujiuliza ni kwanini?. Sababu zinaweza kuwa nyingi sana lakini na hii nayokupatia inaweza kuingia katika hizo sababu zako, sababu nayokupa ni kwa kuwa waliyapata mafanikio wakati bado wanafikira za kimasikini hivyo wameshindwa kukaa katika mafanikio kwa kuwa bado wanawaza umasikini maana ndiko fikira zao ziliko.

Mabadiliko ya kweli huanza na fikira hata kama utapewa nini, hata upewe kila kitu lakini kama hujabadili fikira zako sahau kuhusu mafanikio. Kwahiyo kitu cha kwanza katika kuelekea mafanikio ni kubadili fikira zako ziwe zimekaa kimafanikio mafanikio na ndio hapo utaanza kuyaona mafanikio na kuishi kanuni za mafanikio. Fikira sio kitu cha kupuuzia hata siku moja na kama utapuuzia basi utakuwa ni mtu wa kupanda na kushuka na hauta eleweka upo upande upi.
Fikira ndio kila kitu katika maisha ya mwanadamu, kila kitu unachokiona leo hii ni matokeo ya fikira zilizofanywa na watu. Kama unataka kufanikiwa basi hakikisha fikira zako ziwe zinaendana na mafanikio na sio kuwa sehemu ambayo hueleweki.