RUMAFRICA Magazine

RUMAFRICA FASHION

RUMAFRICA FASHION

DALILI HIZI ZITAKUONYESHA UNA TATIZO LA KIAFYA.


Kawaida mwili ukiwa umepungukiwa aina yoyote ya kirutubisho (ingredients), huonesha dalili kabla ya kujitokeza kwa ugonjwa. Bahati mbaya sana, watu wengi hawana uelewa wa dalili hizo. Katika makala haya, nakutajia dalili chache miongoni mwa dalili hizo.

Midomo Kukauka

Midomo huakisi afya ya mwili na hali ya maji katika mwili mzima. Kama una maji ya kutosha mwilini, basi hata midomo yako itakuwa laini na yenye unyevu. Unapokuwa na upungufu wa maji, ngozi huwa kavu. Kwa wale akina dada ambao hulazimika kulainisha midomo yao kila wakati kwa kutumia ‘lip sticks’, wajue kwamba wana upungufu wa maji mwilini.
Dalili nyingine…

Kuumwa kichwa, kukosa haja ndogo kwa muda mrefu, kukojoa mkojo wa njano-nyeusi au mkojo wenye harufu kali, ngozi kavu na unapoiminya ngozi ya nyuma ya kiganja inachelewa kunyooka, nazo ni dalili kwamba mwili una upungufu wa maji.

Suluhisho 

Kunywa maji ya kutosha kulingana na uzito wa kazi unazozifanya. Kiwango cha chini ni angalau lita moja ya maji safi na salama, hakikisha umekunywa maji hata kama husikii kiu. Vile vile ulaji wa matunda na unywaji wa juisi zitokanazo na matunda au mboga mboga, huweza kuondoa upungufu wa maji mwilini.

Kukosa Haja Kubwa

Kitendo cha kukaa zaidi ya siku moja bila kupata haja kubwa ni dalili ya wazi ya ukosefu wa kamba lishe (fibre) mwilini. Kwa kawaida binadamu anatakiwa kupata choo kikubwa kila siku kilicho laini na kingi. Iwapo hupati choo kila siku na ukipata unapata kigumu, tena kidogo, jua una matatizo!

Haja kubwa ni muhimu kwa sababu ndiyo inayosafisha tumbo, uchafu unapokaa tumboni kwa muda mrefu, sumu zilizomo kwenye haja kubwa hurejea mwilini na husababisha matatizo mengi ya kiafya, kuanzia magonjwa ya uvimbe, moyo na hata ubongo. Sumu huvuruga pia mtiririko wa homoni mwilini na hudhoofisha kinga ya mwili.

Suluhisho

Kula kwa wingi matunda mbalimbali, mboga za majani na vyakula vitokanavyo na nafaka zisizokobolewa, kama vile ugali wa dona, mtama, ulezi, n.k. Ulaji wa vyakula hivyo bora, siyo tu kutaondoa tatizo la ukosefu wa haja kubwa, bali vitakulinda pia dhidi ya magonjwa ya kisukari, presha, ugonjwa wa moyo na mengine mengi.

Vidonda Pembeni ya Mdomo

Utafiti umeonesha kwamba kupasuka kwa midomo na kutokea kwa vidonda pembeni ya midomo, huwa ni dalili moja wapo ya upungufu wa vitamini B mwilini na mara nyingi huwatokea watu wanaopenda kunywa kilevi kupita kiasi, kula vyakula vya kwenye makopo (processed foods) na kula sukari kwa wingi.

Suluhisho

Suluhisho ni kula vyakula vyenye kuongeza vitamin B kwa wingi. Miongoni mwa vyakula vyenye kiwango kingi cha vitamin B ni pamoja na kiini cha mayai ya kienyeji, viazi vitamu, nyama ya ng’ombe na ya kuku, maini na vyakula vitokanavyo na nafaka isiyokobolewa.

Ingawa unaweza pia kula vidonge lishe vya vitamin B ili kuondoa upungufu huo, lakini tahadhari lazima ichukuliwe na ina shauriwa kula vyakula vya kuongeza vitamini hiyo zaidi kuliko vidonge.