RUMAFRICA Magazine

RUMAFRICA FASHION

RUMAFRICA FASHION

KIFO CHENYE UTATA CHA KIGOGO MSTAAFU JESHI LA MAGEREZA UCHUNGUZI WAANZA

 
Dodoma: Naibu Kamishna mstaafu wa Magereza nchini (DCP), Luhusa Chiza (62) amefariki dunia katika mazingira ya utata kwenye Hoteli ya Kitemba mjini Dodoma. 

Kwa mujibu wa mashuhuda tukio hilo, mwili wa Chiza uligunduliwa juzi mchana na mmoja wa wahudumu wa hoteli hiyo alipotaka kufanya usafi. 



Taarifa zaidi kutoka ndani ya hoteli hiyo iliyopo Barabara ya Sita katikati ya mji, zilidai Chiza aliingia Novemba 15 usiku na msichana ambaye alitoroka baadaye. 

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, Lazaro Mambosasa alisema mwili wa Chiza ulikutwa ukiwa na damu puani na kwamba, aliingia chumbani akiwa na msichana ambaye wanamtafuta. 

Alisema kamishna huyo alifika mjini hapa akitokea jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kukagua viwanja vyake na kwamba, alikuwa akielekea mkoani Kigoma. 



Meneja wa Hoteli ya Kitemba, Crispin Daniel alisema mteja huyo aliingia Novemba 15.

“Mhudumu alikuja kuniambia kuna mteja hajisikii vizuri chumbani, anatapika si kwamba alifariki dunia akiwa hapa. Ingekuwa hivyo usingekuta hivi,” alisema. 

Alisema baada ya kupokea maelezo hayo, alipiga simu polisi na walifika na kumchukua na hafahamu kilichoendelea. 

“Watu wanasema alifia hapa kwa sababu waliona polisi wamejaa, ukweli alitoka akiwa anaumwa ndicho ninachofahamu,” alisema. 

Kaimu Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Dodoma, Dk Caroline Damian alithibitisha kupokewa kwa mwili huo juzi mchana. 

“Tayari tumeshamfanyia postmortem (uchunguzi) na tumechukuwa sampuli ya chakula, kwa ajili ya kupeleka kwa Mkemia Mkuu wa Serikali,” alisema. 

Mkuu wa Magereza Mkoa wa Dodoma, Antonio Kilumbi alisema mwili wa ofisa huyo ulisafirishwa jana kwenda Wilaya ya Kasulu mkoani Kigoma kwa mazishi.



“Alikuwa akitokea Dar es Salaam kuchunguza afya yake maana anapressure (shinikizo la damu) na alishawahi kuzimia mara nyingi tu,” alisema Kilumbi.