RUMAFRICA Magazine

RUMAFRICA FASHION

RUMAFRICA FASHION

PETER MABULA : ROHO, AKILI NA MWILI WAKO UNAVILISHA NINI KILA SIKU?


Na Mtumishi Peter Mabula.

BWANA YESU atukuzwe ndugu yangu.
Karibu tujifunze Neno la MUNGU.
Leo nazungumzia maeneo ambayo yanatakiwa kulishwa au kujazwa vitu fulani ambavyo vinaweza kuwa ni vibaya au vuzuri.

Wagalatia 6:7 "Msidanganyike, MUNGU Hadhihakiwi; Kwa Kuwa Chochote Apandacho Mtu,ndicho Atakachovuna."

Ndugu, Unayo Maeneo matatu(3) Ya Kuyalisha. 

Maeneo Yako Ya Kulisha Ni Roho, Akili Na Mwili. 
Kile upandacho ndicho utakachovuna.
Ukipanda dhambi utavuna mabaya na hata unaweza kuvuna jehanamu kama hutatubu na kumrudia BWANA YESU.
Ukipanda mema utavuna baraka.
Ukilipanda ndani yako neno la KRISTO lazima utatoka na ushindi. BWANA YESU anawatafuta watu kama hao wanaopanda Neno lake ndani yao na kuishi maisha matakatifu. 
Kile unachopanda lazima tu kiote na kustawi na kuzaa matunda, hayo matunda yanaweza kuwa mabaya au mazuri.

Yakobo 1:14-15 '' Halafu ile tamaa ikiisha kuchukua mimba huzaa dhambi, na ile dhambi ikiisha kukomaa huzaa mauti. Ndugu zangu wapenzi, msidanganyike. '' 

-Huu ni mfano mmojawapo ya vile ambavyo mwanadamu anaweza kuvipanda ndani yake na kuzaa mabaya. ukipanda tamaa mbaya ndani yako, hiyo tamaa inaweza kuzaa mtoto aitwae dhambi na hiyo dhambi ikikomaa inaweza kuzaa mauti. mauti hapa inawakilisha uharibifu, mateso, jehanamu na kila jambo ambalo limekuja kinyume na mpango wa MUNGU kwako. Tamaa mbaya ni kitu kilichopandwa ndani yako na kimeota na kutoa mmea ulitwao dhambi na dhambi ikikua huzaa uharibifu.
Ndugu yangu, ni vizuri sana kushughulikia shina kabla ya kutaka kushughulikia matawi ambayo hata yakitoka bado yanaweza kuota tena, ndio maana ujumbe huu umekuja leo ili kukusaidia ujue jinsi ya kujinasua na mabaya au dhambi inayokusumbua kwa muda mrefu. msaada ni huu '' Jaza Neno la MUNGU katika moyo wako na liishi neno la MUNGU utafanikiwa''
Hapo juu kuna sehemu tatu ambavyo wanadamu hupanda. Kuna vitu unaweza kuvipanda rohoni mwako na vikatoa matokeo kwako, kuna vitu unaweza kuvipanda kwenye akili yako au kwa jina jingine kwenye nafsi yako na vitatoa majibu kwako, na kuna vitu unaweza kuvipanda kwenye mwili navyo vikatoa majibu. tahadhari ni kwamba je unapanda nini? je unapanda mabaya au mazuri? je unapanda utakatifu na laana? je unapanda mbingu au kuzimu? je unapanda baraka au hasara.
Kila siku nafsi yako unailisha nini?
Kila siku mwili wako unaujaza nini?
Kila siku roho yako unailisha nini?
BWANA YESU siku akirudi atakuja kuhukumu walio hai wote na wafu wote. wakati mwingine unatenda mabaya kwa sababu umekubali kulisha mabaya roho yako, nafsi yako na mwili wako.
Mithali 1:7 '' Kumcha BWANA ni chanzo cha maarifa, Bali wapumbavu hudharau hekima na adabu. ''

-Andiko hili lina siri kubwa sana. Kumcha BWANA ndio chanzo cha maarifa sahihi na elimu sahihi na akili sahihi.
Kama unamcha BWANA hakika utajaza roho yako mambo ya MUNGU na hiyo kukusaidia kukaa mbali na dhambi.
Kama una mcha BWANA lazima ujitenge na mabaya yote. 

=Unacholisha Roho Yako Kama Ni Kizuri Utavuna Faida Na Kama Ni Kibaya Utavuna Mabaya. 
Ndugu yangu, je rohoni mwako umejaza nini?
Hata katika kutafuta mchumba ili awe mke mwema/mme mwema wako lazima uangalie je ndani yake yuko YESU au yuko shetani? Je rohoni mwake amejaza ufalme wa MUNGU au amejaza ufalme wa giza?
Kile unachopanda rohoni mwako ndicho utakachovuna.
BWANA YESU anasema 
''Basi kila asikiaye hayo maneno yangu, na kuyafanya, atafananishwa na mtu mwenye akili, aliyejenga nyumba yake juu ya mwamba;-Mathayo 7:24''

-Ukijaza roho yako neno la MUNGU na ukalitendea kazi hakika utakuwa heri.
-Ukipanda neno hai la MUNGU ndani yako linaweza kukupa uzima. 

Ukiilisha roho yako kila siku neno la MUNGU na Maombi hakika utashinda dhambi na vishawishi vyote vibaya.
kuna watu hutunza taarifa mbaya tu rohoni mwao. ndugu ni lini utatunza taarifa nzuri ndani yako?. taarifa nzuri ni Wokovu wa KRISTO.

Mithali 16:20-21 ''Atakayelitafakari neno atapata mema; Na kila amwaminiye BWANA ana heri. Aliye na hekima moyoni ataitwa mwenye busara; Utamu wa maneno huongeza elimu.''

-Je una hekima hekima moyoni mwako?
-Utakua na hekima kama tu umejaza mambo ya MUNGU katika roho yako. 

=Akili Yako Pia Inatakiwa Ijazwe Vitu Vizuri. Ukijaza Kwenye Akili Yako Neno La MUNGU Itakuwa Ni Heri Kwako Maana Utajaza Ufahamu Mzuri Wa Ki-MUNGU. Lakini Kama Akili Yako Ukiijaza Mabaya Ni Kwa Hasara Yako Mwenyewe.
Kuna watu kwenye akili zao wamejaza vitu vibaya ambavyo vimewashinda kuviacha hata kama wanatamani kuacha. kuna vijana wengi leo simu zao wamejaza video za ngono na kupelekea kila siku wanaota ndoto za uzinzi tu. Hawataki ndoto hizo chafu ila hawajajua kwamba ndoto hizo chafu zinakuja kwao kila siku katika hali isiyo ya kawaida kwa sababu kila siku wanazilisha nafsi zao picha za uzinifu. watu hao ndani yako kumejaa dhambi na sio utakatifu.
Ndugu, kujaza kwako mabaya akilini mwako kutakufanya uonekane huna akili hata moja mbele ya waliojaza mambo mazuri akilini mwao.
Wagalatia waliitwa hawana akili kwa sababu walijaza vitu visivyosahihi katika akili zao.
Wagalatia 3:1-4 ''Enyi Wagalatia msio na akili, ni nani aliyewaloga, ninyi ambao YESU KRISTO aliwekwa wazi mbele ya macho yenu ya kuwa amesulibiwa? Nataka kujifunza neno hili moja kwenu. Je! Mlipokea ROHO kwa matendo ya sheria, au kwa kusikia kunakotokana na imani? Je! Mmekuwa wajinga namna hii? Baada ya kuanza katika ROHO, mnataka kukamilishwa sasa katika mwili? Mmepatikana na mateso makubwa namna hii bure? Ikiwa ni bure kweli.'' 

-Je akili yako umejaza nini? 
-Kuna watu kila siku wanajaza nafsi zao mawazo mabaya ambayo wamejikuta wakiyaishi hata kama hawapendi, kumbe tatizo ni kile ambacho wanalisha akili zao kila siku ndicho kinawatesa. 
ndugu yangu, ndio maana ujumbe huu umekuja kwako ili kuanzia leo akili yako uijaze ibada, uijaze utakatifu na uijaze injili ya KRISTO.
Kuna watu wamepanda nafsini mwao nguo fupi tu ndio maana kila siku wanavaa vimini mitaani, hata wakizomewa bado hawajawahi kushtuka kwamba wakifanyacho hakifai bali ndio kwanza wameongoza na kuacha matiti nje. chanzo ni kile walichojaza kwenye akili zao. akili zao zimewaelekeza hivi '' Nguo za heshima zinatakiwa zivaliwe mbele za wakwe tu na wazazi''. 
hicho ni matokeo ya kile wanacholisha nafsi zao. ili wabadilike wanatakiwa kubadilika kwanza kwenye akili yao ambayo imewapotosha.
Kuna watu ndani yao wamejaza miungu na kumwacha MUNGU aliye hai ambaye anapatikana katika KRISTO YESU pekee.
Hawa inahitajika neema ya MUNGU ya kuwabadilisha roho zao, nafsi zao na miili yao ndipo wataitambue kweli inayoweka huru watu. kweli inayoweka huru ni KRISTO YESU pekee(Yohana 8:36)
Kuna ndugu ndani yao wamejaza miziki ya kidunia mioyoni mwao kiasi kwamba hata wamefeli masomo yao maana ndani ya akili zao hawakujaza kile walichofundishwa, bali walijaza bongo fleva. hiyo ni mifano michache tu lakini ukweli ni kwamba kunahitajika mabadiliko makubwa katika jamii yote, na mabadiliko hayo yatakuja tu pale ambapo ufahamu utabadilika na kuanza kujaza Neno la MUNGU la uzima. 

Kuna Watu Akili Zao Wamejaza Miziki Ya Kidunia, Watu Kama Hao Hata Ukiwaalika Kwenye Ibada Au Mkesha Kanisani Lazima Watoe Udhuru. Ni Kwa Sababu Akili Zao Wamejaza Mambo Mabaya. Ukijaza Kwenye Akili Yako Soka Sidhani Kama Unaweza Kuchagua Kwenda Kwenye Mkesha Wa Maombi Badala Ya Kwenda Kwenye Mpira kama vyote hivyo viwili vitakuwa vinafanyika muda mmoja.
Hayo Ni Matokeo Ya Akili Yako Kuijaza Yasiyotakiwa. Lakini Akili Yako Ukiijaza Neno La MUNGU Ni Lazima Utatamani Mambo Ya Ki-MUNGU. 
Biblia inatoa angalizo kwamba 
'' Vitu vyote ni safi kwa hao walio safi; lakini hakuna kilicho safi kwao walio wanajisi, wasioamini; bali akili zao zimekuwa najisi, na nia zao pia. Wanakiri ya kwamba wanamjua MUNGU, bali kwa matendo yao wanamkana; ni wenye machukizo, waasi, wala kwa kila tendo jema hawafai. -Tito 1:15-16 '' 

=Kile Unacholisha Mwili Pia Kina Faida au hasara Yake. 
Yohana 3:6 '' Kilichozaliwa kwa mwili ni mwili; na kilichozaliwa kwa ROHO ni roho. '' 

-Kumbe mwili huzaa na kilichozaliwa na mwili ni mwili.
-Mwili uliojaa uzinzi huleta matokeo mabaya kimwili lakini kiroho ndio kuna matokeo mabaya zaidi. Mwili ulijazaa dhambi huleta matokeo mabaya. kumbe hata mwili unatakiwa ujazwe vitu vizuri na sio vibaya, sizungmzii kujaza chakula cha kimwili mfano chpsi mayai bali nazungumzia hali ya kiroho katika mwili wako.

1 Kor3:3 '' kwa maana hata sasa ninyi ni watu wa tabia ya mwilini. Maana, ikiwa kwenu kuna husuda na fitina, je! Si watu wa tabia ya mwilini ninyi; tena mnaenenda kwa jinsi ya kibinadamu? ''

-Tabia ya mwili ni matokeo ya kujijaza mambo yasiyo sahihi.
Ni muhimu sana kujaza ndani yako mambo ya MUNGU na kuyashika.
Kuna watu wanatamani wakue kiroho lakini imeshindikana maana ndani yako wamejaza mambo yasiyofaa.
Hata wanaokua kiroho ukiwatazama kiuchunguzi utagundua kwamba kila siku ndani yao wanapanda vitu vya ki-MUNGU. Wanapanda maombi, kulisoma na kulitafakari Neno la MUNGU na kujitoa kwa ajili ya KRISTO.
Ndugu, yale unayolisha roho yako kila siku ndio unayoyaishi. yale unayolisha nafsi yako kila siku hayo ndio unayoyaishi au utakayoyaishi na yale unayopanda katika mwili wako hayo ndio utakayoyaishi.
Mithali 12:20 ''Hila imo mioyoni mwao wafikirio uovu; Bali wafanyao mashauri ya amani, kwao kuna furaha. '' 

-Ndugu,Naamini umejifunza na utachukua hatua njema ya kumpokea BWANA YESU kama hujaokoka ili awe BWANA na MWOKOZI wako tangu leo na utaanza kuishi maisha matakatifu
KAMA UNATAKA KUTUBU RUDIA MANENO HAYA KISHA TAFUTA KANISA LA KIROHO UKAJIUNGE NA KUANZA KUISHI MAISHA MATAKATIFU.
''BABA katika jina la YESU KRISTO Niko mbele zako mimi mwenye dhambi, lakini leo nimetambua kosa langu na naomba unisamehe dhambi zangu zote, nisamehe dhambi ninazozikumbuka na pia zile ambazo sizikumbuki. futa jina langu katika kitabu cha hukumu na uliandike jina langu katika kitabu cha uzima. Neno lako katika Warumi sura ya 10 Mstari wa 9 na wa 10 Neno lako linasema ''Kwa sababu, ukimkiri YESU kwa kinywa chako ya kuwa ni BWANA, na kuamini moyoni mwako ya kuwa MUNGU alimfufua katika wafu, utaokoka. Kwa maana kwa moyo mtu huamini hata kupata haki, na kwa kinywa hukiri hata kupata wokovu '' . BWANA YESU mimi nimekuamini leo na hivyo naamini sasa napokea wokovu wako na hakika nimeokoka. Kuanzia leo Naufunga ukurasa wa dhambi na ninaufungua ukurasa wa matendo mema na matakatifu. BWANA nipe ROHO wako Mtakatifu ili aniwezeshe kushinda dhambi na anasa zote za dunia. Kuanzia leo mimi nimeokoka na ni mtoto wa MUNGU mwenye haki zote. ninafuta laana zote na kila roho ya shetani inayonifuatilia naiharibu kwa jina la YESU KRISTO kama neno la MUNGU linavyosema katika Yeremia sura ya kwanza mstari wa 10. BWANA YESU nakushukuru sana kwa kuniokoa. Yote haya kwa imani nimepokea na niko tayari sasa kwa ROHO MTAKATIFU kunitumia. Katika jina la YESU KRISTO nimeomba na kupokea .
Amen.''
Kama umetubu toba ya kweli hakika wewe kuanzia sasa ni mshindi na ni shujaa. Kwa sasa naishia hapo, MUNGU akitupa nafasi tutajifunza tena siku nyingine. ulishindwa kumpokea BWANA YESU nafasi yako bado ipo na muda wa kumpokea ni leo wala sio kesho, amua leo na atakuandika jina lako katika kitabu cha uzima na utaanza kuukulia wokovu kwa mafundisho kanisani. MUNGU ana makusudi kabisa na wewe, hataki upotelee motoni anataka uende uzimani aliko KRISTO BWANA. MUNGU akubariki sana . 
Ni mimi ndugu yako Peter  Mabula