RUMAFRICA Magazine

RUMAFRICA FASHION

RUMAFRICA FASHION

TMA YATAHADHARISHA NCHI KUKUMBWA NA UKAME


DAR ES SALAAM: Mamlaka ya Hali ya Hewa Nchini (TMA) – imeendelea kuwataka Wakulima kufuatilia kwa ukaribu Taarifa za hali ya hewa pamoja na kuzingatia maelekezo ya wataalamu wa kilimo.

Hatua hiyo inatokana na uwepo wa dalili za upungufu wa mvua katika mwezi Novemba kwenye maeneo mengi nchini jambo ambalo linaweza kuathiri uzalishaji katika kilimo.

Hayo yamebainishwa jana Jijini Dar es salaam na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Hali ya Hewa Nchini Dkt. Agnes Kijazi alipokuwa akizungumza na Waandishi wa Habari ambapo alisema hadi sasa bado kuna viashiria vingi vya upungufu wa mvua ikiwa ni pamoja na kupungua kwa Joto katika eneo la kati la Bahari ya Pasifiki kitendo ambacho kinafahamika kama LANINA.

Alibainisha kuwa hali hiyo inapojitokeza husababisha ukame hivyo kwa wakulima kuzingatia maelekezo ya wataalam wa kilimo kwa kulima mazao ya muda mfupi na yanayostahamili ukame.

Dkt. Kijazi aliongeza kuwa Mamlaka hiyo imekuwa ikifuatilia kwa ukaribu mienendo ya ya unyevunyevu katika maeneo mbalimbali nchini pamoja na Joto katika Bahari ya Hindi ambapo imebainika kuwa hali ya unyevunyevu inaendelea kupungua katika maeneo mbalimbali nchini huku Joto katika Bahari ya Hindi ikionekana kuendelea kupungua mambo ambayo ni dalili za upungufu wa mvua na ukame.

Aidha Dkt. Kijazi alizungumzia tatizo la kutokea kwa mvua za mawe katika baadhi ya maeneo nchini ambapo alibainisha kuwa tatizo hilo linasababishwa na mabadiliko ya hali ya hewa ambayo hupelekea kutokea kwa aina ya mawingu inayofahamika kama mawingu ng’amba hivyo suala hilo halina sababu za kuhusianishwa na Imani za kishirikina kama ambavyo baadhi ya watu wamekua wakidhania.