RUMAFRICA Magazine

RUMAFRICA FASHION

RUMAFRICA FASHION

HII FUNGA MWAKA YA 2016! KUTANA NA FAMILIA INAYOISHI MAKABURINI DAR

Dar es Salaam: Unaweza kudhani ni simulizi ya mambo ya kusadikika, lakini ni ukweli mtupu, suala hili linatokea katika ulimwengu huu, tena katika Mitaa ya Ubungo-Maziwa jijini hapa, ambapo familia ya Rasta Magoda na Amina Robert inaishi katika eneo la makaburi yanayolizunguka eneo hilo, yapata miaka saba sasa.


Katika makala haya, waandishi wa Uwazi, Boniphace Ngumije, Ally Katalambula na Meckion Mathiew wanakuletea historia, sababu ya familia hiyo kuishi katika eneo hilo, mauzauza na mambo mengine mengi ambayo familia hiyo imeweza kushuhudia kwa muda wote huo wa miaka saba ikiwa hapo baada ya kuitembelea katika makazi yao hayo.

Rasta Magoda akiwa na mwanaye.

Akizungumza na Uwazi kwa kujiachia, Rasta Magoda ambaye ni baba wa familia hiyo anasema kuwa alianza kuishi hapo mwaka 2009 baada ya kupata ajali ya gari iliyomsababisha kuwa mlemavu wa mguu na kushindwa kufanya shughuli kubwa za kujipatia kipato zaidi ya kazi ndogondogo.

“Si kwamba ninapenda kuishi mahali hapa (Makaburi ya UFI yaliyopo Ubungo-Maziwa, Dar) mimi na familia yangu. Lakini hii ni baada ya kupata ulemavu na kujikuta siwezi kufanya kila kitu kwa ajili ya kujipatia kipato.

“Kipindi cha nyuma nilikuwa dereva wa magari lakini mwaka 2006, nilipata ajali. Nilipopona, mwaka 2009 katika namna ya kujitafutia kipato niliamua kuhamia katika eneo hili,” anasema Rasta Magoda.

Mwandishi: Kwani wewe ni mwenyeji wa wapi?

Rasta Magoda: Tanga.

Mwandishi: Kipindi unaanza kuishi hapa katika eneo hili la makaburi hukuwa unaogopa?

Mke wa Rasta Magoda akiwa na wanaye.

Rasta Magoda: Hapana, kwanza unatakiwa kufahamu kuwa wakati ninaanza kuishi hapa, haya makaburi hayakuwepo (yalikuwepo lakini hayakuwa yamekaribia au kuwa jirani na kibanda anachoishi), yamekuja baadaye, yaani yamenikuta.

Mwandishi: Kwani eneo hili ulipewa na nani?

Rasta Magoda: Eneo hili nililipata kutoka kiwanda cha jirani lakini sipendi kukitaja jina moja kwa moja.

Mwandishi: Hujawahi kupata usumbufu wowote kutoka serikalini au mtu yeyote kuhusu kuishi hapa?

Rasta Magoda: Usumbufu ambao nimewahi kupata ni kutoka kwa mwenyekiti wa serikali ya mtaa kipindi fulani hivi, alikuwa hataki niishi hapa, lakini baadaye nilikwenda kwa mtendaji nikazungumza naye vizuri na kumuomba aniachie hapa maana ni sehemu naitumia kujiingizia kipato na kupata riziki, akaniruhusu kuishi hapa.

Mwandishi: Kwa hiyo umeoa huku unaishi hapahapa?

Rasta: Ndiyo.

Mtoto wa Rasta Magoda akiwa katika pozi.
Mwandishi: Swali kwa mama, wewe ni mwenyeji wa wapi na ulichukuliaje siku ya kwanza ulipoletwa na mumeo kuja kuishi hapa?

Amina: Mimi ni mwenyeji wa Kasulu, Kigoma, nilipachukulia kawaida tu, maana niliamua mwenyewe kuja kuishi na mume wangu na pia hali yake nilikuwa naifahamu.

Mwandishi: Siyo kwamba alikushawishi kwa namna yoyote na ukajikuta upo hapa?

Amina: Hapana, niliamua mwenyewe.

Mwandishi: Ndugu zenu huwa wanawatembelea mkiwa katika eneo hili?

Amina: (Akicheka), ndiyo kwa nini wasije?

Mwandishi: Inawezekana wakawa wanaogopa kutokana na eneo lote kuzungukwa na makaburi?

Amina: Hapana. Hapa hii ni sehemu salama kabisa na hata wakija huwa tunawaondoa wasiwasi.

Mwandishi: Watoto wenu hawa wote wawili mmewapata mkiwa hapahapa?

Amina: Ndiyo, tulikuwa hapahapa, huyu mkubwa anaitwa Chris na mdogo Robert.

Mwandishi: kwa upande wa malezi kwa watoto unakutana na changamoto gani kama mama, tukiangalia pia katika eneo hili hakuna hata watoto wengine wanaoweza kucheza nao, kuna shida gani mnakutana nayo.

Amina: Hakuna changamoto yoyote, kama ni watoto kucheza mimi nacheza nao na kwetu malezi ni mazuri tu.

Mwandishi: Hakuna wakati watoto mnawakuta wakiwa juu ya makaburi wakicheza wakati mwingine?

Amina: Hapana, watoto wanachezea hapahapa katika maeneo ya nyumba tu.

Mwandishi: Tukirudi kwa rasta, mnategemea kuishi hapa mpaka lini?

Rasta Magoda: Mpaka pale Mungu atakaponisaidia kupata kipato kizuri na kujimudu vizuri kimaisha.

Itaendelea Toleo lijalo.