RUMAFRICA Magazine

RUMAFRICA FASHION

RUMAFRICA FASHION

SERIKALI YAWATAKA WAAJIRI KUHAKIKISHA MITAMBO NA VIFAA VYA KAZI VINAFANYIWA UKAGUZI MARA KWA MARA.

Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Vijana), Mhe. Antony Mavunde akitoa hotuba yake wakati wa mkutano na waandishi wa habari ulioandaliwa na Wakala wa Usalama na Afya Mahali Pa Kazi (OSHA) kuhusu maandalizi ya maadhimisho ya siku ya Usalama na Afya mahali pa kazi uliofanyika Aprili 25, 2017 Dodoma.
Baadhi ya Watumishi wa Wakala wa Usalama na Afya Mahali Pa Kazi (OSHA) wakimsikiliza Naibu wake Ofisi ya Waziri Mkuu Mhe. Antony Mavunde (hayupo pichani) wakati wa Mkutano wa waandishi wa habari ulioandaliwa na Ofisi hiyo ikiwa ni maandalizi ya ya maadhimisho ya siku ya Usalama na Afya mahali pa kazi uliofanyika Mjini Dodoma.
Kaimu Mtendaji Mkuu OSHA Bi. Khadija Mwenda akizungumza wakati wa mkutano na Waandishi wa habari juu ya maandalizi ya maadhimisho ya Siku ya Usalama na Afya mahali pa Kazi uliofanyika Mjini Dodoma Aprili 25, 2017.
Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Vijana, Ajira na Wenye Ulemavu) Bw.Peter Kalonga akichangia hoja wakati wa Mkutano na waandishi wa habari juu ya maandalizi ya maadhimisho ya Siku ya Usalama na Afya mahali pa Kazi uliofanyika Mjini Dodoma Aprili 25, 2017.
Naibu Waziri Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Vijana), Mhe. Antony Mavunde akisalimiana na Mwakilishi wa TUCTA Bw.Ramadhani Mwenda mara baada ya mkutano wa waandishi wa habari Aprili, 25, 2017 Dodoma
Naibu wake Ofisi ya Waziri Mkuu (Kazi, Ajira na Vijana), Mhe. Antony Mavunde (katikati waliokaa) akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya Watendaji wa Wakala wa Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA)mara baada ya kumaliza mkutano na waandishi wa habari Aprili 25, 2017 Mjini Dodoma. (PICHA NA OFISI YA WAZIRI MKUU-DODOMA)

Serikali imewataka waajiri wote na wadau kwa ujumla kuhakikisha kuwa sehemu za kazi, mitambo na vifaa vya kufanyia kazi vinafanyiwa ukaguzi mara kwa mara ili kuhakikisha kuwa havileti madhara kwa wafanyakazi. 

Hayo yamesemwa na Naibu Waziri, Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulikia masuala ya Kazi, Ajira na Vijana Mhe. Antony Mavunde wakati wa mkutano na waandishi wa habari leo mjini Dodoma kuhusu maandalizi ya maadhimisho ya siku ya Usalama na Afya mahali pa kazi. 

“Kwa upande wa Serikali jukumu letu kubwa ni kuweka na kusimamia sera ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi, kutunga na kusimamia Sheria za Usalama na Afya Mahali pa Kazi, na kuweka viwango mbalimbali vya usalama na afya sehemu za kazi” alisisitiza Mavunde. 

Mavunde alisema kuwa kwa sasa kanuni ya kuripoti ajali na magonjwa imekamilika na kuanza kutumika tangu mwezi Septemba, mwaka 2016. 

Ambapo ameshauri wafanyakazi kuwasaidia waajiri wao kusimamia mifumo iliyopo, kujilinda wao binafsi ili wasiumie ama wasipate magonjwa yatokanayo na kazi sambamba na kutumia ipasavyo vifaa vyote vya kujikinga wawapo kazini. 

Mavunde alisema kuwa serikali inaendelea kuboresha mfumo wa ukusanyaji takwimu za ajali na magonjwa yatokanayo na kazi, hivyo bado kuna changamoto ya kupata taarifa kuhusu ajali na magonjwa yatokanayo na kazi hii inatokana na waajiri wengi kutoripoti taarifa hizo kama sheria inavyoelekeza. 

kwa mantiki hiyo Serikali inaandaa mfumo ambao utaongea na mifumo mingine ili kupata taarifa za ajali na magonjwa. 

Aliongeza kuwa “Serikali kupitia Wakala wa Usalama na Afya Mahala pa Kazi (OSHA) imejipanga kuhakikisha kuwa Usalama na afya za wafanyakazi hao zinalindwa kwa kuhakikisha kuwa waajiri wanazingatia taratibu zote za Usalama na Afya kwa mujibu wa sheria na 5 ya Mwaka 2003, ili kulinda nguvu kazi ya taifa hili”. 

Aidha, tarehe 28 Aprili ya kila mwaka, Tanzania inaungana na mataifa mengine duniani kuadhimisha siku ya Usalama na Afya Mahali pa kazi ili kuwakumbuka wahanga wa majanga yanayotokea sehemu za kazi. 

Madhumuni makubwa ya kuadhimisha siku hii ni kuendesha kampeni ya Kimataifa ya kuboresha usalama na afya kazini na kuhamasisha utengenezaji ajira zenye staha. Kwa kuhamasisha waajiri na wafanyakazi na umma kwa ujumla kuchukua hatua za makusudi ili kuhakikisha kuwa suala la ajali na magonjwa yatokanayo na kazi yanapungua au kutotokea kabisa sehemu za kazi. 

Maadhimisho ya mwaka huu yanatarajia kufanyika Moshi Mkoani Kilimanjaro kwa kujumuisha shughuli hizo kuanzia tarehe 25 hadi tarehe 27 ambapo yatatanguliwa na kongamano la wadau wa Usalama na Afya.