RUMAFRICA Magazine

RUMAFRICA FASHION

RUMAFRICA FASHION

Dereva Aliyesababisha Vifo vya Wanafunzi Wawili Akamatwa

KAMISHNA wa Polisi Kanda Maalum Dar es Salaam, Simon Sirro, amethibitisha kutokea kwa vifo vya wanafunzi wawili, Itlamu Athumani (mwanafunzi wa kidato cha kwanza Shule ya Sekondari Msimbazi) na Sakina Hamis (mwanafunzi kidato cha kwanza Mchikichini) na tayari wamemkamata dereva huyo aliyesababisha ajali hiyo kwa uzembe.

Akizungumza na wanahabari jijini Dar es Salaam leo Mei 3, Sirro amesema jeshi la polisi limepokea taarifa ya tukio la ajali hiyo eneo la Super Doll Barabara ya Nyerere na alisema mtuhumiwa atafikishwa mahakamani.

Ajali hiyo ilikuwa ni kati ya lori aina ya Scania lenye namba za usajili T 273 CEV lililogongana na basi moja aina ya Echer lenye namba za usajili T376 lililokuwa likitokea Gongo la Mboto.

Alieleza kuwa katika ajali hiyo majeruhi wengine ni takribani 24 ambapo wanawake majeruhi ni tisa na wanaume 21 ambao baadhi yao wametibiwa katika Hospitali ya Wilaya ya Temeke na kuruhusiwa.

Amefafanua kuwa chanzo cha ajali hiyo ni uzembe wa dereva wa lori la Scania ambako ni mali ya kampuni ya Mikoani Traders lililoingia barabara ya pili bila kuchukua tahadhari kuelekea kwenye maegesho ya ofisi yao na kusababisha ajali hiyo.

Katika hatua nyingine Sirro amesema kuwa wamekamata risasi tisa mnamo Aprili 29 maeneo ya Minazikinda Wilaya ya Kigamboni zikiwa zimetelekezwa kwenye makaravati ambapo ufuatiliaji unaendelea ili kubaini risasi hizo zilitelekezwa na watu gani na nani mmiliki halali wa risasi hizo.

Na Denis Mtima