RUMAFRICA Magazine

RUMAFRICA FASHION

RUMAFRICA FASHION

BILA WACHUNGAJI NCHI HAINA PA KUKIMBILIA-KAMANDA KOVA


Huku likiendelea kulaumiwa kwa utendaji usiokidhi matumizi ya nguvu kupita kiasi, Jeshi la Polisi nchini limefungua na kueleza kuwa bila msaada wa watumishi wa Mungu juhudi zao za kukabiliana na uhalifu nchini hazitazaa matunda yoyote.

Akizungumza na chazo kimoja cha blog hii katika mahojiano maalumu  wiki  iliyopita, Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova,  alisema nchi inaelekea katika hali ya hatari,  hivyo  wameamua kukutana na wachungaji ili washirikiane nao katika kuirejesha  kwenye utulivu.


Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Suleiman Kova

“Tumeamua kuwashirikisha watumishi ili wamlilie Mungu wao aliye hai, awezekurejesha amani ambayo imeanza kuyumbayumba. Kweli bila hao nchi yetu hatujui itaelekea wapi, tunaimani kubwa kwamba wana kitu cha ziada juu ya nchi,” alisema Kamanda Kova.

Kamanda Kova aliweka wazi kuwa, kwa kutambua umuhimu wa watumishi wa Mungu aliye hai wiki iliyopita walilifanya kikao maalumu nao jijini hapa, ili kuwasihi wamsihi  Kristo alikumbuke taifa la Tanzania na kulirejesha katika amani.

Mkuu huyo wa Jeshi la Polisi,aliweka bayana kuwa, lengo la kikao hicho na watumishi hao wa Mungu ni kupanga mikakati ya kufanya kazi pamoja kwa kile alichodai kuwa kwa nguvu pekee za Jeshi hilo, hakuna chochote kitakachowezekana na nchi inaweza kuwa katika matatizo makubwa.

“Lengo la Jeshi la Polisi, kukutana na wachungaji lilikuwa ni nzuri tu, unajua sisi tunafanya doria ya kuzuia uhalifu kwa njia ya mwili, lakini wachungaji wanafanya doria kwa njia ya rohoni, kwa hiyo wao wana nafasi kubwa ya kuleta mafanikio makubwa nakukomesha hali iliyopo katika taifa kwa sasa, ambayo siyo nzuri,” alisema Kamanda.   
Sambamba na hilo,  alisema watumishi wa Mungu wanauwezo mkubwa wa kuwafundisha watu maadili mema, kwa kuwa kauli yao katika jamii inasikilizwa zaidi.

 

“Lazima nchi iwe na amani kwa kutumia mbinu zozote, unafikiri ndugu mwandishi mambo yakiharibika tutakimbilia wapi, hakuna pa kukimbilia mambo yakiharibika katika taifa letu, kwa hiyo lazima tushirikiane na wachungaji kukomesha uhalifu,” alisema Kamanda Kova.

Kamanda Kova aliwataka watanzania kuacha tabia ya kuleta vurugu katika taifa,  huku wakijichukulia sheria mkononi  na kusababisha madhara makubwa katika taifa, hali inayopelekea mvurugano kutokea hata wananchi wasiokuwa na hatia kupoteza maisha.

Kadhalika anawasihi wachungaji kote nchini kuwa na uchungu na taifa hili, washirikiane na Jeshi hilo bega kwa bega kurejesha amani ya taifa ambalo ni mfano hata katika nchi mbalimbali duniani na likikifahamika kama kisiwa cha amani.

Aliongeza kuwa Jeshi la polisi lilikiri mbele ya wachungaji hao kuwa kutumia nguvu na risasi, si suluhu na haitakuwa njia ya kutatua tatizo bali ni kuongeza matatizo zaidi, hivyo likaomba ushirikiano kwa taasisi mbalimbali za kidini hapa nchini kukemea vitendo vibaya vinavyoweza kuliweka taifa pabaya

Source: Gospelvisiontz

Comments