| Mchungaji Florian Katunzi akiongoza maombi wakati wa kongamano aliloliandaa na kanisa analosimamia la EAGT City Centre jijini Dar es salaam. |
Kongamano la siku nane la maombi na
maombezi lililomalizikia hivi karibuni Jijini Dar es Salaam, limewaponya na
kuwafungua watu wengi waliokuwa wakiteswa na Shetani kwa kuwatoa katika
‘majeneza’ ya magonjwa na matatizo sugu
yaliyokuwa yakiwasumbua, akiwemo kijana Rashid Selemani (25) aliyenusurika
kutolewa kafara na wachimbaji
madini Wilayani Nachingwea mkoani Lindi.
Umati
wa watu ulishuhudia kijana huyo akitambaa kama nyoka wakati akiombewa
uponyaji, ambapo baada ya kuponywa alitoa ushuhuda wake jinsi yeye na
wenzake kumi walivyoshauriwa kwenda kwa
mganga wa kienyeji na kuchemshwa katika sufuria ili kufanikisha upatikanaji wa
madini.
Alisema
yeye na wenzake hao walikuwa wachimbaji madini ya dhahabu katika mgodi
mmoja mkoani humo, ambapo ‘mabosi’ wao waliwashauri kwenda kwa mganga wa
kienyeji ili kupata dawa, bila kujua nia ya mabosi hao ilikuwa kuwatoa kafara.
“Tupofika kwa mganga tulilazwa katika
chumba chenye joka kubwa lililotuchanja chale tatu katika miguu ya kulia na baadaye tulichemshwa katika sufuria kubwa
la maji ya moto na kupatiwa dawa”, alisema kijana Sulemani na kuongeza kuwa
baada ya kurudi katika mgodi wa dhahabu, walijikuta wakipata ajali mbaya ya
kuangukiwa na kifusi.
Alisema anamshukuru Mungu kwamba
wafanyakazi wenzao waliwaokoa yeye na wenzake wawili waliokuwa wamefukiwa
pamoja, ambapo katika harakati za uokoaji alijeruhiwa mguuni na kumsababishia
jeraha linalomfanya atembee akichechemea.
Kijana
Selemani ambaye wakati akiombewa uponyaji alikuwa akipiga kelele na kutembea kama nyoka kutokana na
mapepo yaliyokuwa yamempagaa, alisema baada ya kunusurika kutolewa kafara alikimbilia Jijini Dar es Salaam maeneo ya
Mwembeyanga.
Alisema siku moja alikutana na wanawake
waliokuwa wakisukana na akawauliza
sehemu lililopo kanisa la kilokole.
Kijana Selemani alisema wanawake hao walimwelekeza kwenda kwenye viwanja vya
Sabasaba na ndipo alipofika katika Ukumbi wa PTA na kushiriki katika kongamano
la Maombi na mombezi lililokuwa likiendeshwa na Mchungaji Florian Katunzi wa
Kanisa la EAGT City Centre.
Uponyaji wa kijana Selemani na ushuhuda
wake ni sehemu ya miujiza mikuu ya uponyaji iliyorindima katika siku nane za
kongamano hilo lililowatoa wengi kutoka katika ‘majeneza’ ya mateso ya shetani.
Katika siku ya mwisho ya kongamano hilo
lililovuta maelfu ya watu katika ukumbi wa PTA ulioko katika viwanja vya
Maonesho ya Kimataifa ya Biashara vya Mwalimu Nyerere maarufu kama Sabasaba,
ujumbe uliotolewa na Mchungaji Katunzi ulihusiana na Injili ya Luka 7:11-17.
Injili hiyo inazungumzia jinsi Yesu Kristo
Bwana wa uhai alivyomfufua mtoto wa mama mjane aliyekuwa amekufa katika
mji na
Naini, kwa kuwaambia watu waliokuwa wamebeba jeneza wakielekea kumzika
waliweke chini, kisha akaligusa na kuiambia maiti iamke na
ikatii mara moja.
“Ujumbe wa leo ni maombi ndani mwa maombi,
ambapo kila pando asilolipanda Baba Yetu wa Mbinguni litang’olewa”, alisisitiza
Mchungaji Katunzi katika mahubiri yake.
Mchungaji Katunzi aliendesha maombezi
mazito ya kuwatoa watu kutoka katika majeneza ya utasa, magonjwa, mapepo,
umasikini, kudharauliwa, matatizo ya ndoa, majini, wachawi na matatizo mengine
mengi.
Wengi walioondolewa katika majeneza hayo
kupitia maombezi hayo, walidondoshwa na nguvu za Mungu na kukimbizwa
katika chumba maalum kupatiwa huduma za kiroho na timu maalum ya
maombezi ya watendakazi wa Kanisa la EAGT City Centre.
Mara baada ya kumalizika kwa kongamano hilo
la Maombi na Maombezi, Mchungaji Katunzi aliliambia gazeti Msemakweli kuwa yuko
katika maandalizi ya kongamamo jingine la siku nne la Maombi na Maombezi
litakalofahamika kama Anza mwaka na Bwana 2013.
Alisema kongamano hilo litaanza Desemba 29,
2012 na kumalizika Junuari 1, 2013
katika ukumbi wa PTA, likiwa maalum kwa ajili ya kuwaingiza Watanzania mwaka
2013 kwa ujumbe wa baraka za kifamilia, utakaojikita zaidi katika masuala ya
uchumi na elimu.
Limeandika Msemakweli.
Comments