RUMAFRICA Magazine

RUMAFRICA FASHION

RUMAFRICA FASHION

KIJANA WA AJABU MWENYE UWEZO WA KUKARIRI BIBLIA NZIMA AIBUKA

Anthony Alli Ramadhani akirejea kifungu kutoka kichwani mwake wakati wa ibada
Ni siku ya Alhamisi wiki iliyopita ambapo ofisi za Gazeti Msemakweli zinapata Mgeni wa aina yake ambaye aliacha simulizi ambayo ni vigumu kuaminika, lakini ukweli unabaki pale pale kwamba Mgeni huyo ana uwezo wa ajabu wa kukariri Maandiko Matakatifu yaliyomo katika vitabu mbalimbali vya Biblia, na kuyasoma neno kwa neno kutoka kichwani mwake bila kukosea neno hata moja. 
Kijana huyo aliyejitambulisha kwa jina la Athony Alli Ramadhani (36) aliyeokoka mwaka 1996 katika Kanisa la Pentekoste Tabora mjini ni zao linalotokana na mama mkristo na baba Mwislamu, ambao hata hivyo walitengana wakati kijana huyo akiwa bado mdogo. 
Athony ambaye kwa sasa anaishi Jijini Dar es Salaam na ni mshirika wa Kanisa la kilokole la Ufufuo na Uzima lililoko Kawe, alilifika katika ofisi za Gazeti hili akiwa ni Biblia yake iliyochakaa ikionesha kwamba imekuwa ikinasomwa sana. 
Katika mahojiano na Gazeti hili alisema kuwa nia yake ni kuhakikisha kuwa anaikariri Biblia nzima kuanzia kitabu cha Mwanzo hadi Ufunuo wa Yohana na akaonesha kwa vitendo kudhihirisha kiu yake hiyo, kwa kusoma sura 15 za kitabu cha Mwanzo bila kukosea neno. 

Aidha kijana Athony alisema tayari amekariri sura nyingi za vitabu vya Zaburi na Hesabu lakini kiu yake ni kuimaliza Biblia nzima, kwani uwezo anao isipokuwa kinachomkwamisha ni muda na shughuli nyingi za kutafuata maisha bila kupata muda mzuri wa kupumzia na kusoma Biblia yake. 
“Baada ya kuokoka nilikuwa na kiu sana ya kumjua Mungu na kumtafuta Mungu kupitia neno lake, ndipo siku moja nikiwa nimelala Mungu alijibu maombi yangu na kunionesha maono yaliyonitaka nisome kwa bidii neno lake”,alisema Kijana Athony ambaye wakati wa mahojiano na agazeti hili, alikuwa akipokea simu nyingi kutoka kwa watu waliokuwa wakiulizia sehemu yalipo Maandiko fulani Matakati katika Biblia Takatifu na yeye kuwajibu haraka papo kwa hapo bila kukosea. 
“Nakumbuka siku moja mchana nilisikia sauti ambayo naamini ni ya Mungu ikinitaka nikalale. Nilitii na ndipo nikiwa usingizini nililetewa kitabu mbele yangu na tazama nilishuhudia maandishi ya moto yakipita katika kurasa zake. Baadaye nikasikia sauti ikiniambia kwamba napaswa kukariri maandiko hayo kisha ndoto hiyo ikakoma nikaamka”, alisema kijana Anthony. 
Alisema tangu wakati huo alianza kusoma Biblia na kujikuta kila akisoma maandiko yote anayosoma yanakaa kichwani na kwamba kamwe hayasauliki. 
“Hali ndivyo ilivyo ndugu Mwandishi. Nitaka niikariri Biblia nzima ila kwa sasa nafanya kazi ya bodaboda na nyingine ambazo zinachukuwa muda wangu mwingi. Nataka sana nipate mtu wa kunifadhili ili nikasome niwe mchungaji kabisa kwa vile najua Mungu ameshaniita, ila tatizo ni fedha.Akitokea mtu akanifadhili nitafurahi sana”, alisema Kijana huyo ambaye katika kanisa lake analosali anafahamika kama Mchungaji mshauri kutokana na huduma ya kuwapa ushauri wa kiroho Wakristo wapya na wenyeji. 
Alisema elimu yake ni ya darasa la nne inayomuwezesha kusoma vyema Biblia ya Kiswahili na kuandika, lakini angefurahi zaidi kama angepata ufadhili pia wa kusomweshwa lugha ya Kiingereza ili aikariri Biblia nzima ya Kiingereza kama anavyofanya kwa Biblia ya Kiswahili. 
Gazeti hili lilitaka kujua namna watu wanavyouchukulia uwezo wake mkubwa wa kukariri maandiko ya Biblia ambapo alisema anamshukuru Mungu kwamba Mchungaji wake Josephat Gwajima anamkubali na kumwelewa na kwamba siku moja alishawahi kumtambulisha mbele ya kanisa na akamuombea na kumtaka asonge mbele na kazi ya Injili. 
“Najua watu wengine wanakataa kipaji nilichopewa na Mungu na wanasema ni nguvu za giza zinazoniongoza kitu ambacho sio cha kweli. Tazama Mwandishi, Shetani hawezi kujifitini kiasi hiki kwa kunipa uwezo huu ili nieneze Injili ya Yesu Kristo. Ninachojua mimi ni kwamba aliyenipa uwezo huu ni Mungu mwenyewe kupitia Roho Mtakatifu kwa ajili ya kuujenga ufalme wake na sio wa Shetani”, alisema kijana Athony.
Limeandika Gazeti Msemakweli.

Comments