RUMAFRICA Magazine

RUMAFRICA FASHION

RUMAFRICA FASHION

SOMO: JIFUNZE KUSAMEHE - MWALIMU CHRISTOPHER MWAKASEGE


Mwalimu Christopher Mwakasege

JIFUNZE KUSAMEHE NA KUSAHAU

Tuna uhakika ya kwamba, Roho Mtakatifu anakuongoza kusoma somo hili kwa makusudi kamili.

Maneno yaliyomo humu ni ya kukusaidia wewe na Wakristo wote, ili tuweze kuishi maisha ya "amani na watu wote, na huo utakatifu, ambao hapana mtu atakayemwona Bwana asipokuwa nao."(Waebrania 12:14).
Kusamehe na kusahau ni tatizo kubwa ambalo limewazuia wakristo wengi wasipokee majibu ya maombi yao toka kwa Mungu. Ninaamini kuwa maneno yaliyomo humu yatakusaidia katika kupokea majibu ya maombi mengi ambayo hujayapokea.


Ni maombi yetu kwa Mungu, katika Jina la Yesu Kristo ya kwamba, Roho Mtakatifu ayachukue mafundisho haya na kuyaandika katika moyo wako, na akusaidie kuyatenda.
Na unaposoma itakuwa ni vizuri ukiwa na Biblia yako karibu, ili usome mistari yote tuliyoiandika. Somo hili tutajifunza kwa wiki sita mfululizo. Somo la wiki inayofuata litakuwa linajenga juu ya somo la wiki linalotangulia hasa baada ya wiki ya kwanza.
Mungu akusaidie unapofuatilia somo hili mpendwa wa mungu

KUTOKUSAMEHE NI KIKWAZO
" Nanyi, kila msimamapo na kusali, sameheni mkiwa na neno juu ya mtu; ili na Baba yenu aliye mbinguni awasamehe na ninyi makosa yenu. Lakini kama ninyi hamsamehi, wala Baba yenu aliye mbinguni hatawasamehe ninyi makosa yenu" (Marko 11:25,26).


Kutokusamehe ni kikwazo na kizuizi kikubwa ambacho kinasimama kati ya mtu na majibu ya maombi yake. Watu wengi wanapenda imani zao zikue, lakini kwa sababu ya kutokusamehe imani zao zinakuwa hazina matunda.
Tatizo si kwamba watu hawapendi kusamehe. Ingawa watu wanapenda kusameheana, lililo wazi ni kuwa walio wengi hawajui namna ya kusamehe kule kunakokubalika na Bwana. Watu wengi wanajifunza katika biblia juu ya imani, maombi, utakatifu na mambo mengine ya kiroho. Lakini ni watu wachache wanaojifunza kutoka katika biblia namna ya kusamehe.Kati ya vizuizi vya mtu kupokea jibu la maombi yake kutoka kwa Mungu, ni tatizo la kutokujua jinsi ya kusamehe.
Bwana Yesu alipowambia wanafunzi wake juu ya kusamehe alitaka waone uhusiano ulipo kati ya sala na kusamehe. Kwa maneno mengine alitaka wafahamu kuwa kujibiwa kwa maombi na sala na dua kunategemea sana uhusiano walionao na watu wengine.Kabla Yesu hajasema juu ya kusamehe alizungumza maneno muhimu sana juu ya maombi. Yesu alisema hivi:

" Mwamini Mungu. Amini, nawaambia, yeyote atakayeuambia mlima huu, ng'oka ukatupwe baharini, wala asione shaka moyoni mwake, ila aamini kwamba hayo asemayo yametukia, yatakuwa yake. Kwa sababu hiyo nawaambia, Yoyote myaombayo mkisali, aminini ya kwamba mnayapokea, nayo yatakuwa yenu." (Marko11:22 - 24)

Haya ni maagizo muhimu sana kwa kila mkristo, kwa ajili ya maisha ya ushindi kila siku. Na watu wengi wamekuwa wakiitumia mistari hii, ili kupata mahitaji yao ya kiroho na ya kimwili.
Mafanikio yako katika kutumia mistari hiyo na ahadi hizo za Bwana Yesu, yatategemea sana jinsi wewe unavyofuata maagizo ya Yesu juu ya matumizi ya mistari hiyo.
Kuna mtindo uliozuka katikati ya watu wa Mungu, wa kuifanya biblia kuwa kama duka. Wanafungua biblia, wanachagua mistari wanayotaka na ahadi wanazotaka, wanaondoka nazo, huku wakiiacha mistari mingine kwenye biblia.

Lakini wanapoitumia hiyo mistari ya ahadi wanazotaka, na kuona hakuna matokeo yoyote, wanaona kama kwamba neno la Mungu limepungua nguvu.Hiyo si kweli. Neno la Mungu halijapungua nguvu zake wala halitakujapungua nguvu zake. Neno la Mungu hudumu milele.Kwa hiyo ni vizuri kusoma na kutafakari ahadi za Mungu juu ya maombi, lakini pia ni muhimu sana kuhakikisha kuwa unafuata maagizo yote ya utumiaji wa ahadi hizo.Kwa hiyo walio wengi. Maombi yao juu ya magonjwa, ndoa zao, wokovu wa ndugu zao na kadhalika, yamefungwa kwa kutotimiza maagizo haya ya Bwana Yesu.

"NINYI KILA MSIMAMAPO NA KUSALI, SAMEHENI, mkiwa na neno juu ya mtu; ili na Baba yenu aliye mbinguni awasamehe na ninyi makosa yenu. Lakini kama ninyi hamsamehi, wala Baba yenu aliye mbinguni hatawasamehe ninyi makosa yenu" (Marko 11;25, 26).

Maombi yako hayajibiwi mara nyingi kwa sababu ya wewe kutosamehe wengine. Kwa maneno mengine Yesu alitaka tufahamu kuwa, tusipojifunza kusamehe wengine waliotukosea, tutabaki na dhambi mbele za Mungu.
Maana yake nini basi?
Maana yake, kutokusamehe kunahesabiwa kuwa ni kosa mbele za Mungu, na ni dhambi inayotutenga na uso wa Mungu, ili tusijibiwe maombi yetu toka kwa Mungu.
Kutokusamehe ni uasi Dhambi ni uasi (1 Yohana 3:4) Dhambi ni kuasi maagizo ya Mungu.

Kama Mungu ameagiza kwa kinywa cha Kristo kuwa kabla hatujaomba lo lote, ni lazima tusamehe kwanza; inakuwaje basi, wewe unataka ujibiwe maombi yako kabla hujamsamehe mwenzako?
Na kwa kutokusamehe umeasi agizo la Mungu, na kufuatana na waraka wa kwanza wa Yohana 3:4umehesabiwa kuwa umetenda dhambi.Kwa hiyo unahitajiwa utubu juu ya kutokusamehe!
Tuna uhakika kuwa wewe unayesoma hayo umewahi kuisema 'Sala ya Bwana' iliyoandikwa katika kitabu cha Mathayo, Sura ya 6:9-15.
Hatujui kama unaelewa uzito wa maneno yaliyomo katika sala hiyo. Walio wengi wanaisema kwa sababu wameikariri, lakini si kwamba wameielewa maana yake.
Katika sala hiyo, kuna maneno yanayohusu mambo ya kusamehe:
"Utusamehe deni zetu (makosa yetu) kama sisi nasi tuwasamehevyo wadeni wetu (walio tukosea). (Mathayo6:12)

Tafakari hili neno 'kama'
Utusamehe makosa yetu, kama sisi nasi tunavyowasamehe waliotukosea.Hii ina maana ya kwamba kipimo kile unachokipimia katika kuwasamehe wengine ndivyo na Mungu atakavyotumia kipimo hicho hicho kukusamehe wewe mambo uliyomkosea.Sasa elewa kwamba hakuna kusamehe kukubwa, wala kusamehe kudogo. Kutokusamehe ni kutokusamehe. Na kusamehe ni kusamehe. Mizani yake inapima kitu kizima, haipimi msamaha kidogo kidogo.

Yesu alilifafanua jambo hili aliposema:-
"Kwa maana mkiwasamehe watu makosa yao, na Baba yenu wa mbinguni atawasamehe ninyi. Bali msiposamehe watu makosa yao, wala Baba yenu hatawasamehe ninyi makosa yenu." (Mathayo 6:14,15).

Je, unaweza kusamehe bila kusahau?
Tulipokuwa tunaongea na mama mmoja juu ya kumsamehe mume wake, ili ugonjwa wake upone, alituambia; "Mimi nilikwishamsamehe siku nyingi."
Tukamuuliza; "Una uhakika?"
Akasema, "Ndiyo, la sivyo ningekuwa nimekwishatengana naye"
Tukamuuliza tena: "Kuna wakati wo wote huwa unawaza kuwa isingekuwa ni watoto mliozaa naye, ungeomba talaka au ungeondoka tu?
Akasema; Ndiyo, tena mara nyingi."
Tukamwambia: "Kusamehe kwako kuko wapi wakati bado unayahesabu makosa ya mume wako, kiasi ambacho ndoa imeshikiliwa na watoto badala ya kushikiliwa na makusudi ya Mungu?"
Yule mama akashangaa.

Kuna watu wengine wanasema wamesamehe wakati, bado kuna fundo na shina la uchungu katika mioyo yao. Kwa kinywa wanasema, wamesamehe, lakini moyoni bado hawajasamehe.
Na kuwatambua watu wa namna hiyo ni rahisi sana.
Mtu huyo huyo akimkosea tena, utamsikia akilalamika akisema;
"Mtu huyu nilimsamehe lile kosa la kwanza, tena amerudia. Kumbe mambo yalikuwa hayajaisha, ndiyo maana hata siku fulani alisema maneno fulani, ndiyo maana hata juzi alimgombeza mtoto wangu ......"
Utaona mtu huyo akiyakumbuka yote mabaya ya nyuma ambayo mwenzake alimtendea. Wengine hata hudiriki kusema kuwa: "Nitamsamehe lakini sitasahau"
Sasa, hiyo siyo lugha ya watu wa Mungu, waliookolewa na kununuliwa kwa damu ya thamani ya Yesu Kristo.


Hiyo ni lugha ya watu wasiomjua Mungu, watu wa ulimwengu huu. Na Biblia inatuambia kwamba sisi siyo wa ulimwengu huu. (Yohana 17:16).
Weka hilo katika roho yako. Wewe si wa ulimwengu huu, kwa hiyo lugha na maneno ya ulimwengu huu hayakuhusu. Zungumza lugha ya watu watakatifu wa ufalme wa Mungu ambao ndiyo wa uzao wako.
Utawezaje kusema kuwa umemsamehe mwenzako wakati bado una uchungu naye moyoni mwako? Utasemaje umemsamehe wakati kila wakati unalikumbuka na kulisema kwa watu kosa alilokufanyia?
Utasema huko ni kusamehe ambako Mungu anataka ufanye, ili na yeye akusamehe.
La hasha!
Kusamehe bila kusahau kosa ulilokosewa ni kusamehe kusikokamilika wala kukubaliwa mbele za Mungu. Kusema umesamehe huku bado una uchungu moyoni mwako, ni unafiki ulio wazi mbele ya Mungu.

Je! hujawahi kusoma mistari ifuatayo:
"Mmesikia watu wa kale walivyoambiwa, Usiue; na mtu akiua, itampasa hukumu. Bali mimi nawaambieni, kila amwoneaye ndugu yake hasira itampasa hukumu, na mtu akimfyolea ndugu yake itampasa baraza; na mtu akimwapiza itampasa jehanamu ya moto."(Mathayo 5:21, 22)
Unaweza kuona jinsi Yesu Kristo alivyofananisha hasira hiyo iliyojaa moyoni mwako juu ya ndugu yako na uuaji. Na adhabu zake zinafanana.Sasa, utakuwa unajiuliza, inawezekana kwa vipi mtu kusahau mabaya aliyotendewa?Basi nakuhakikishia kuwa inawezekana kabisa! Kwa kuwa yote yanawezekana kwake aaminiye. Na imani huja kwa kusikia neno la Mungu (Warumi 10:17) Tatizo lako ni kwamba unaona kusamehe na kusahau ni vitu viwili tofauti, kwa hiyo unavitenganisha. Huwezi ukatenganisha kusamehe na kusahau. Kwa kuwa huwezi kusamehe bila kusahau; na huwezi kusahau bila kusamehe.

Ufanyeje basi, uweze kusamehe na kusahau ili na Mungu naye akusamehe na kusahau makosa yako?
Ili tuweze kufahamu namna ya kusamehe na kusahau, ni muhimu tuielewe tabia ya Mungu juu ya jambo hili.

Comments