RUMAFRICA Magazine

RUMAFRICA FASHION

RUMAFRICA FASHION

KWA TAHARIFA YAKO: UNAJUA KIJITONYAMA UPENDO GROUP WALIKOANZIA UIMBAJI?
Haya mdau wetu wa Gospel Kitaa kama tulivyokuahidi kwamba kuanzia alhamisi ya leo tutakuwa tunakuletea kipengele cha habari kiitwacho ''KWA TAHARIFA YAKO'' taarifa utakayoipata yawezekana ni mpya kwako au ya zamani, kama unaijua unaweza kuongeza jambo ambalo GK haikufanikiwa kulijua kwa kuweka comment yako chini kabisa ya habari husika(angalizo iwe ni kwa ajili ya kuujenga ufalme wa Mungu).



Kundi la Kijitonyama Upendo Group.

KWA TAHARIFA YAKO;-- Siku ya leo tunaanza na kundi lililojipatia umaarufu sana nchini tangu mwanzo wa miaka ya 2000 hadi sasa,nazungumzia kundi la Kijitonyama Upendo Group a.k.a Spiritual Voice. Kama hujui kundi hili limetokea wapi, Ni kwamba kundi hili waimbaji wake walikuwa ni wanakwaya wa kwaya ya Uinjilisti Kijitonyama walioimba pambio la Hakuna Mungu Kama Wewe, wanaopatikana katika kanisa la Kiinjili la Kilutheri Kijitonyama.

Waimbaji wa Upendo group ndio walikuwa waimbaji tegemewa katika kwaya hiyo kabla hawajajitoa, ninaposema tegemewa nina maana waimbaji wanne wa kundi hilo walikuwa masolo au waanzilishi wa nyimbo za kwaya hiyo, waimbaji hao ni Joshua Mlelwa na mkewe Lilian Mlelwa, Albert Mpale Mafwenga pamoja na mkewe Eluinjuka Mafwenga pamoja na mwanadada Esther Castory hawa walikuwa waimbaji tegemewa wa kwaya ya Kijitonyama Uinjilisti pamoja na wenzao wengine.

Walijitoa kwenye kwaya hiyo kama GK inakumbuka vyema mwishoni mwa mwaka 1999 wakati huo wakiwa tayari walisharekodi album yao ya ''Mungu Anakupenda'' wakiwa bado ndani ya kwaya kisha kuamua kutoka katika kwaya hiyo na kuendelea na kundi lao la Upendo Group ili kueneza injili kwa mapana zaidi, ila huku nyuma kwenye kwaya waliacha shida kidogo ya waimba solo hali iliyolazimu walimu waliokuwepo kuamua kutunga nyimbo zisizokuwa na mwimbishaji(solo) jambo ambalo walifanikiwa baada ya muda kupita.



Joshua Mlelwa akiwaongoza wenzake wakati huo akiwa ndani ya kundi hilo pamoja na mkewe, wa kwanza kushoto.

Ikumbukwe kwamba waimbaji wa Upendo group kanda yao ya mwisho kushiriki na kwaya ilikuwa ''IKO WAPI IMANI'' kwa wale walio na kanda hiyo kama unajua vyema sauti zao utawasikia baadhi yao humo, bila kusahau toleo ambalo GK inalipenda liitwalo ''YESU NI UPENDO'' pia humo utawasikia, au kwa wale waliotazama nyimbo za maombolezo za kifo cha Baba wa Taifa mwalimu Nyerere kuna wimbo unaitwa ''KILIO'' kilio ah kilio ah Tanzaniaa tunalia tunalia ulioanzishwa na Joshua na mwimbaji mwingine wa kwaya hiyo.

Kijitonyama Upendo Group walipotoka hakika walifanikiwa kuliteka soko la muziki wa injili na kubadilisha upepo kabisa, nikisema kwamba kundi hili ndio lililochangia kwakiasi kikubwa matumizi ya kuimba kwa kutumia CD hapana shaka utakubaliana nami(ingawa kwa sasa wameacha na kuanza kupiga live), uchezaji, nyimbo zao, ziliwafanya wapate umaarufu na kuzifanya mpaka kwaya kuanza kucheza kwa bidii pamoja na kuimba ili wafanane na kundi hili, jambo ambalo naweza kusema kwamba hakika Upendo Group walifanikiwa kubadilisha upepo wa uimbaji ingawa wenyewe wameacha kutumia CD lakini makundi mengine mpaka leo hawataki kuacha.

Kundi hili lilifanya makundi mengine kuibuka lakini hayajadumu na kubaki historia ingawa kundi hilo liko imara mpaka leo kumtangaza Kristo.Kundi hili ni la kwanza kwa makundi ya gospel nchini kufanya maonyesho mengi nje ya nchi kama Ujerumani,Uingereza, Marekani na nchi nyingine za Scandnavia, Pia moja ya mafanikio ni kwamba limefanyika baraka kwa watu wengi ikiwa ni pamoja na kuwa chanzo cha mamia ya watu kurejea kwa Kristo, maendeleo mengine wanamiliki kiwanja cha ekari 10 pamoja na studio ya video iitwayo Kijitonyama Upendo Group(KUG) production ambayo imefanikiwa kurekodi waimbaji wenye majina kama Rose Muhando.

Kundi hili baada ya kutoka na ''Mungu Anakupenda'' ulioanzishwa na mke wa Joshua aitwaye Lilian ambaye kama Upendo wamealikwa sehemu kama hayupo huyo dada unaona kama kundi halijafika, kutokana na kumudu vyema nafasi yake ya utumishi shambani mwa Bwana, matoleo yao yaliyofuata ni pamoja na Ingia zizini, Bam-Bam,Maisha yako,Jina lako li hai,Mungu wa ushindi pamoja na matoleo ya video ambayo wamejirekodi kupitia production yao ya KUG.

Lakini pia kwasasa waimbaji wawili ambao walikuwa tegemewa ndani ya kundi hilo bwana Joshua Mlelwa pamoja na mkewe Lilian wamejitoa katika kundi la Upendo Group, kwasasa wanafanya huduma peke yao na tayari wametoa toleo lao huku wimbo wao wa ''NI WEWE'' ukiwa unafanya vyema katika tasnia ya muziki wa injili nchini. Lakini kundi la Kijitonyama Upendo Group lipo palepale na huduma bado inaendelea.

WIKI IJAYO NITAKUFAHAMISHA KAMA HUJUI NINI KILITOKEA ZAIDI KWA UPANDE WA KWAYA YA KIJITONYAMA UINJILISTI BAADA YA WENZAO KUONDOKA NDANI YA KUNDI.


HAPA ANGALIA BAADHI YA PICHA ZA ZAMANI WAKATI WAIMBAJI HAO WAPO NDANI YA UINJILISTI KIJITONYAMA. PICHA KUTOKA MAKTABA YA K-JUNIOR BLOG.



Hapa unaweza kumuona Lilian wa kwanza kushoto ndani ya joho enzi hizo akiwa na Uinjilisti Kijitonyama.




Hapa unaweza kumuona Esther mbele mwenye nyekundu nyuma yake yupo Lilian wakiwa na waimbaji wenzao wa Kijitonyama Uinjilisti enzi hizo huko walimu wao bwana Mushi mwenye miwani pamojana na Emanuel Shedo (MC FOMA FOMA) wakicharaza magitaa.




Hapa unaweza kumuona Eluinjuka wa kwanza kulia akipiga macho kuelekea kamera, hapa enzi hizo ndani ya kwaya ya Uinjilisti Kijitonyama.

KWA LEO HIYO NI KWA TAHARIFA YAKO KAMA ULIKUWA HUJUI!

Comments