RUMAFRICA Magazine

RUMAFRICA FASHION

RUMAFRICA FASHION

JE UNAFAHAMU UPENDO WA MAMA UNAFUNUA UPENDO WA MUNGU?

Matangazo yametengezwa na Rumafrica +255 715 851 523

“Je, mke anaweza kumsahau mtoto wake anayenyonya hivi kwamba asimhurumie mwana wa tumbo lake? Hata hawa wanawake wanaweza kusahau, lakini mimi mwenyewe sitakusahau wewe.”—ISAYA 49:15.

MTOTO mchanga aliyezaliwa anatulia katika mikono ya mama yake wakati mama anapomnyonyesha. Mazingira hayo ni yenye wororo na upendo. Mama mmoja anayeitwa Pam anasema hivi: “Nilipomshika mtoto wangu kwa mara ya kwanza mikononi mwangu, nilihisi upendo mwingi na kuona kwamba nina daraka la kutunza uhai huo mpya.”

Ingawa ni jambo linaloonekana wazi, uchunguzi umethibitisha kwamba upendo wa mama unachangia sana ukuzi wa mtoto mchanga. Hati fulani iliyochapishwa na Mradi wa Shirika la Afya Ulimwenguni juu ya Afya ya Akili inasema hivi: “Uchunguzi umeonyesha kwamba watoto ambao wameachwa na kutenganishwa na mama zao wanakosa furaha na kufadhaika, na nyakati nyingine wanakuwa na wasiwasi.” Hati hiyohiyo inataja uchunguzi ambao unaonyesha kwamba kuna uwezekano mkubwa kwa watoto wanaoonyeshwa upendo na kutunzwa tangu utotoni kuwa na akili nyingi kuliko watoto ambao wanapuuzwa.

Kuhusu umuhimu wa upendo wa mama, Alan Schore, profesa wa magonjwa ya akili kwenye Shule ya Utabibu ya UCLA huko Marekani, anasema hivi: “Uhusiano wa kwanza wa mtoto, yaani, uhusiano wake pamoja na mama yake, unakuwa ndio kielelezo, kwa kuwa unafinyanga kabisa uwezo wa mtoto wa kuwa na mahusiano mengine ya kihisia baadaye.”

Inasikitisha kwamba mfadhaiko, magonjwa, au mikazo mingine huenda ikamfanya mama ampuuze au hata “kumsahau mtoto wake.” (Isaya 49:15) Lakini si jambo la kawaida kwa mama kumpuuza au “kumsahau mtoto wake.” Kwa kweli, inaelekea kwamba ni jambo la asili kwa akina mama kuwapenda watoto wao. Watafiti wamegundua kwamba wakati mama anapojifungua, homoni fulani (oxytocin) inaongezeka na kufanya tumbo la uzazi limsukume mtoto na baadaye inatokeza maziwa kwa ajili ya mtoto. Inaaminika kwamba homoni hiyohiyo, inayotokezwa na wanaume na wanawake, inamchochea mama amtendee mtoto wake kwa upendo na bila uchoyo.

Ni Nini Chanzo cha Upendo?
Wale wanaoamini fundisho la mageuzi wanafundisha kwamba upendo usio na uchoyo, kama ule uliopo kati ya mama na mtoto wake, ulijitokeza wenyewe tu na kuendelezwa kupitia uteuzi wa kiasili kwa sababu uliwafaidi wale waliouonyesha. Kwa mfano, gazeti moja (Mothering Magazine) kwenye Intaneti linasema hivi: “Sehemu ya kwanza ya ubongo wetu ambayo ilitokana na mageuzi pamoja na ile sehemu tuliyorithi kutoka kwa mababu zetu ambao ni viumbe wanaotambaa, ndiyo kiini cha hisia. Mfumo huo wa ubongo ndio unaowawezesha akina mama na watoto wao wachanga kuwa na uhusiano wa karibu sana.”

Hivyo, utafiti umefunua kwamba mfumo huo wa ubongo unachangia sana hisia zetu. Hata hivyo, je, unaona ni jambo la akili kufikiri kwamba upendo wa mama kwa mtoto wake ulitokana na mageuzi ya ubongo wa viumbe wenye kutambaa?

Fikiria uwezekano mwingine. Biblia inasema kwamba wanadamu waliumbwa kwa mfano wa Mungu, yaani, wakiwa na uwezo wa kuonyesha sifa za Mungu. (Mwanzo 1:27) Upendo ndio sifa kuu ya Mungu. Mtume Yohana aliandika hivi: “Yeye ambaye hapendi hajamjua Mungu.” Kwa nini? “Kwa sababu Mungu ni upendo.” (1 Yohana 4:8) Tafadhali ona kwamba andiko hilo la Biblia halisemi tu kwamba Mungu ana upendo. Badala yake, linasema Mungu ni upendo. Yeye ndiye Chanzo cha upendo.

Biblia inaeleza upendo kwa njia hii: “Upendo ni wenye ustahimilivu na wenye fadhili. Upendo hauna wivu, haujigambi, haujivuni, haujiendeshi bila adabu, hautafuti faida zake wenyewe, hauchokozeki. Hauweki hesabu ya ubaya. Haushangilii juu ya ukosefu wa uadilifu, bali hushangilia pamoja na kweli. Huhimili mambo yote, huamini mambo yote, hutumaini mambo yote, huvumilia mambo yote. Upendo haushindwi kamwe.” (1 Wakorintho 13:4-8) Je, linaonekana kuwa jambo linalopatana na akili kuamini kwamba sifa hiyo bora ilitokana na mageuzi?

Unahisi Jinsi Gani?
Ulipokuwa ukisoma maelezo kuhusu upendo katika fungu lililotangulia, je, moyo wako ulitamani sana mtu fulani akuonyeshe upendo kama huo? Ni jambo la asili kuwa na tamaa hiyo. Kwa nini? Kwa sababu “sisi ni uzao wa Mungu.” (Matendo 17:29) Tuliumbwa tukiwa na tamaa ya kupendwa na kuwapenda wengine. Na tunaweza kuwa na hakika kwamba Mungu anatupenda sana. (Yohana 3:16; 1 Petro 5:6, 7) Andiko lililotajwa mwanzoni mwa habari hii linaonyesha kwamba upendo wa Mungu kutuelekea una nguvu hata zaidi na unadumu zaidi kuliko ule wa mama kwa mtoto wake!

Hata hivyo, huenda ukajiuliza: ‘Ikiwa Mungu ni mwenye hekima, mwenye nguvu, na mwenye upendo, kwa nini hakomeshi mateso? Kwa nini anaruhusu watoto wafe, uonevu uendelee, na dunia iharibiwe kwa sababu ya pupa na usimamizi mbaya?’ Hayo ni maswali mazuri ambayo yanastahili kujibiwa kwa njia yenye kusadikisha.

Hata watu wanaoamini kwamba mambo ya Mungu hayawezi kujulikana wakisema nini, unaweza kupata majibu yenye kuridhisha kwa maswali hayo. Mamilioni ya watu katika nchi nyingi wamepata majibu hayo kwa kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Wachapishaji wa gazeti hili wanakualika kufanya vivyo hivyo. Ujuzi wako kumhusu Mungu unapoongezeka kwa kujifunza Neno lake na kuchunguza uumbaji, utaona kwamba hayuko mbali na kwamba unaweza kumjua. Inaelekea utasadikishwa kwamba Mungu “hayuko mbali sana na kila mmoja wetu.”—Matendo 17:27.

Comments