RUMAFRICA Magazine

RUMAFRICA FASHION

RUMAFRICA FASHION

MPENDE JIRANI YAKO KAMA WEWE MWENYEWE

“[Amri] ya pili ni hii, ‘Mpende jirani yako kama wewe mwenyewe.’”—MT. 22:39.


UNGEJIBUJE?

Ni nani kwa kweli aliye jirani yetu?
Kwa nini unaamini kwamba tunaweza na tunapaswa kumpenda jirani yetu?
Kulingana na 1 Wakorintho 13:4-8, upendo unaweza kuonyeshwa kwa njia gani mbalimbali?

PINDI moja, Farisayo alimjaribu Yesu kwa kumuuliza hivi: “Mwalimu, amri iliyo kuu katika ile Sheria ni gani?” Kama ilivyotajwa katika makala iliyotangulia, Yesu alijibu kwamba “amri iliyo kuu na ya kwanza” ni hii: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.” Yesu akaongezea hivi: “Ya pili, kama hiyo, ni hii, ‘Mpende jirani yako kama wewe mwenyewe.’”—Mt. 22:34-39.

2 Yesu alisema kwamba ni lazima tumpende jirani yetu kama tunavyojipenda wenyewe. Hivyo, tunapaswa kujiuliza hivi: Ni nani kwa kweli aliye jirani yetu? Tunawezaje kuonyesha kwamba tunampenda jirani?


Mkurugenzi wa Rumafrica Rulea Sanga (kulia) na Mh. Lazaro Nyarandu-Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii - Tanzania

NI NANI KWA KWELI ALIYE JIRANI YETU?

3 Huenda tukafikiri kwamba jirani ni mtu anayeishi karibu nasi ambaye ni rafiki wa karibu anayetusaidia. (Met. 27:10) Hata hivyo, ona alivyosema Yesu alipoulizwa hivi na mtu aliyejiona kuwa mwadilifu: “Ni nani kwa kweli aliye jirani yangu?” Yesu alimjibu kwa kusimulia mfano wa Msamaria mwema. (Soma Luka 10:29-37.) Tungetarajia kwamba kuhani Mwisraeli na Mlawi wangetenda kama majirani wema walipomwona mtu aliyekuwa ameibiwa, akapigwa, na kuachwa karibu kufa. Hata hivyo, walipita bila kumsaidia kwa njia yoyote. Mtu huyo alisaidiwa na Msamaria—na Wasamaria waliheshimu Sheria ya Musa lakini walidharauliwa na Wayahudi.—Yoh. 4:9.

4 Ili kumsaidia mtu huyo apone, Msamaria huyo alimwaga mafuta na divai juu ya majeraha yake. Alimpa mtunza-nyumba ya wageni dinari mbili ambazo ni sawa na mshahara wa siku mbili hivi ili amtunze mtu huyo. (Mt. 20:2) Hivyo, ni rahisi kuona ni nani aliyethibitika kuwa jirani wa kweli wa mtu huyo aliyejeruhiwa. Kwa kweli, mfano wa Yesu unatufundisha kwamba tunapaswa kumpenda na kumhurumia jirani yetu.
Watumishi wa Yehova hawasiti kuwaonyesha upendo jirani zao upendo (Tazama fungu la 5)

5 Mara nyingi si rahisi kupata watu wenye huruma kama Msamaria huyo. Ni vigumu hata zaidi katika ‘siku hizi za mwisho’ zilizo hatari kwa sababu watu wengi hawana upendo wa asili, ni wakali, na hawapendi wema. (2 Tim. 3:1-3) Kwa mfano, huenda hali za hatari zikatokea wakati wa msiba wa asili. Fikiria kilichotukia wakati kimbunga kinachoitwa Sandy kilipopiga jiji la New York City mwishoni mwa Oktoba 2012. Katika sehemu moja ya jiji iliyoathiriwa sana, wezi waliwaibia wakazi wa eneo hilo ambao tayari walikuwa wakiteseka kwa sababu ya kukosa umeme na mahitaji mengine ya lazima. Katika eneo hilohilo, Mashahidi wa Yehova walifanya mpango ili kuwasaidia waamini wenzao na watu wengine pia. Wakristo hutoa misaada kama hiyo kwa sababu wanawapenda jirani zao. Kuna njia gani nyingine za kuonyesha kwamba tunawapenda jirani zetu?


JINSI TUNAVYOWEZA KUONYESHA UPENDO KWA JIRANI
6 Wasaidie watu kiroho. Tunafanya hivyo kwa kujitahidi kuwapa ‘faraja inayotia moyo kutokana na Maandiko.’ (Rom. 15:4) Kwa kweli, tunaonyesha kwamba tunawapenda jirani zetu katika kazi yetu ya kuhubiri tunapowaambia kweli za Biblia. (Mt. 24:14) Tuna pendeleo kubwa sana la kutangaza ujumbe wa Ufalme kutoka kwa “Mungu anayetoa tumaini”!—Rom. 15:13.

7 Fuata ile Kanuni Bora. Yesu alitaja kanuni hiyo aliposema hivi katika Mahubiri yake ya Mlimani: “Mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima mwatendee wao pia vivyo hivyo; hii, kwa kweli, ndiyo maana ya Sheria na Manabii.” (Mt. 7:12) Tunapowatendea wengine kama Yesu alivyoshauri, tunatimiza kusudi la “Sheria” (kuanzia kitabu cha Mwanzo hadi Kumbukumbu la Torati) na “Manabii” (vitabu vya unabii vya Maandiko ya Kiebrania). Vitabu hivyo vinaonyesha wazi kwamba Mungu huwabariki wale wanaowapenda wengine. Kwa mfano, Yehova alisema hivi kupitia Isaya: ‘Shikeni haki, na mfanye yaliyo ya uadilifu. Mwenye furaha ni yule mwanadamu ambaye hufanya jambo hili.’ (Isa. 56:1, 2) Yehova hutubariki kwa sababu tunawatendea jirani zetu kwa upendo na uadilifu.

8 Wapende adui zako. Yesu alisema hivi: “Ninyi mlisikia kwamba ilisemwa, ‘Mpende jirani yako na kumchukia adui yako.’ Hata hivyo, mimi ninawaambia ninyi: Endeleeni kuwapenda adui zenu na kusali kwa ajili ya wale wanaowatesa ninyi; ili mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni.” (Mt. 5:43-45) Mtume Paulo alirudia jambo hilo alipoandika hivi: “Ikiwa adui yako ana njaa, mlishe; ikiwa ana kiu, mpe kitu anywe.” (Rom. 12:20; Met. 25:21) Kulingana na Sheria ya Musa, mtu alipaswa kumsaidia adui kumfungua punda wake aliyeangushwa na mzigo. (Kut. 23:5) Kwa kufanya kazi pamoja kwa njia hiyo, huenda wale waliokuwa maadui wakawa marafiki wakubwa. Kwa kuwa tunawapenda watu tukiwa Wakristo, adui zetu wengi wamebadili maoni yao kutuhusu. Tukiwapenda adui zetu, hata wale wanaotutesa vikali, tutapata shangwe kama nini kuona baadhi yao wakikubali Ukristo wa kweli!

9 “Fuatilieni amani pamoja na watu wote.” (Ebr. 12:14) Bila shaka, watu hao wanatia ndani ndugu zetu kwa kuwa Yesu alisema hivi: “Ikiwa unaleta zawadi yako kwenye madhabahu na hapo ukumbuke kwamba ndugu yako ana jambo fulani juu yako, acha zawadi yako hapo mbele ya madhabahu, na uende zako; kwanza fanya amani yako pamoja na ndugu yako, na ndipo, ukiisha kurudi, itoe zawadi yako.” (Mt. 5:23, 24) Mungu atatubariki tukimpenda ndugu yetu na kufanya amani haraka pamoja naye.

10 Usitafute-tafute makosa ya wengine. Yesu alisema hivi: “Acheni kuhukumu ili msihukumiwe; kwa maana kwa hukumu mnayohukumu, mtahukumiwa; na kwa kipimo mnachopimia, watawapimia ninyi. Basi, kwa nini unautazama unyasi ulio katika jicho la ndugu yako, lakini hulifikirii boriti lililo katika jicho lako mwenyewe? Au unawezaje kumwambia ndugu yako, ‘Niruhusu niutoe unyasi ulio katika jicho lako’; wakati, tazama! boriti limo katika jicho lako mwenyewe? Mnafiki! Kwanza toa boriti lililo katika jicho lako mwenyewe, na ndipo utakapoona waziwazi jinsi ya kuutoa unyasi ulio katika jicho la ndugu yako.” (Mt. 7:1-5) Yesu anakazia kwa njia yenye nguvu kwamba hatupaswi kuchambua makosa madogo ya wengine kwa kuwa huenda sisi wenyewe tunafanya makosa makubwa zaidi!

NJIA YA PEKEE YA KUONYESHA UPENDO KWA JIRANI
11 Tunataka kuwapenda jirani zetu kwa njia ya pekee. Tunahubiri habari njema ya Ufalme kama Yesu alivyofanya. (Luka 8:1) Yesu aliwaagiza wafuasi wake ‘wafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.’ (Mt. 28:19, 20) Tunatimiza agizo hilo kwa kujitahidi kuwasaidia jirani zetu kutoka katika barabara pana na kubwa inayoongoza kwenye uharibifu na kutembea kwenye barabara yenye nafasi ndogo inayoongoza kwenye uzima. (Mt. 7:13, 14) Bila shaka Yehova anabariki jitihada hizo.

12 Tunawasaidia watu kutambua uhitaji wao wa kiroho kama Yesu alivyofanya. (Mt. 5:3) Tunatosheleza mahitaji ya kiroho ya wale wanaoitikia vizuri kwa kuwahubiria “habari njema ya Mungu.” (Rom. 1:1) Wale wanaokubali ujumbe wa Ufalme wanapatanishwa na Mungu kupitia Yesu Kristo. (2 Kor. 5:18, 19) Kwa kweli, tunawaonyesha jirani zetu upendo kwa njia muhimu sana tunapohubiri habari njema.

13 Tunapofanya marudio na kuongoza mafunzo ya Biblia kwa ustadi, tunawasaidia watu kuishi kupatana na viwango vya uadilifu vya Mungu na hilo hutuletea uradhi. Kufanya hivyo kunaweza kumsaidia mwanafunzi wa Biblia afanye mabadiliko makubwa katika maisha yake. (1 Kor. 6:9-11) Kwa kweli, inatia moyo sana kuona jinsi Mungu anavyowasaidia watu wenye “mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele” kufanya mabadiliko yanayohitajika na kuwa na uhusiano wa karibu pamoja naye. (Mdo. 13:48) Wengi waliokuwa wamekata tamaa hupata shangwe, na badala ya kuwa na mahangaiko yasiyo ya lazima, wanamtumaini Baba yetu wa mbinguni. Inapendeza kama nini kuona wapya wakifanya maendeleo ya kiroho! Je, si kweli kwamba ni baraka kuwaonyesha jirani zetu upendo kwa njia ya pekee tukiwa wahubiri wa Ufalme?

UFAFANUZI ULIOONGOZWA NA ROHO TAKATIFU KUHUSU UPENDO

14 Tukimpenda jirani yetu kama Paulo alivyoeleza, tutampendeza Mungu, tutaepuka matatizo mengi, tutapata furaha, naye atatubariki. (Soma 1 Wakorintho 13:4-8.) Acheni tuchunguze kwa ufupi alichosema Paulo kuhusu upendo na kuona jinsi tunavyoweza kufuata shauri hilo tunaposhughulika na jirani yetu.

15 “Upendo ni wenye ustahimilivu na wenye fadhili.” Kama Mungu anavyoonyesha ustahimilivu na fadhili anaposhughulika na wanadamu wasio wakamilifu, sisi pia tunahitaji kuwa na ustahimilivu na fadhili wengine wanapotukosea na kutenda bila kufikiri au heshima. “Upendo hauna wivu,” hivyo tukiwa na upendo wa kweli hatutatamani mali au mapendeleo ya wengine kutanikoni. Zaidi ya hayo, ikiwa tuna upendo, hatutajigamba au kujivuna kwa kiburi. Kwa kweli, “macho yenye majivuno na moyo wa kiburi, taa ya waovu, ni dhambi.”—Met. 21:4.

16 Upendo utatuchochea kumtendea jirani yetu kwa njia ya adabu. Hatutamdanganya, kumwibia, au kufanya lolote ambalo litavunja sheria na kanuni za Yehova. Upendo utatusaidia pia kuhangaikia faida za wengine badala kuhangaikia tu faida zetu wenyewe.—Flp. 2:4.

17 Upendo wa kweli hauchokozeki kwa urahisi na “hauweki hesabu ya ubaya,” kana kwamba tunaandika katika kitabu wengine wanapotutendea kwa njia isiyo ya upendo. (1 The. 5:15) Hatutampendeza Mungu ikiwa tutakuwa na kinyongo moyoni. Kuwa na kinyongo ni kama kuchochea moto utakaotudhuru na kudhuru wengine. (Law. 19:18) Upendo unatufanya tushangilie pamoja na kweli, lakini utatuzuia ‘kushangilia juu ya ukosefu wa uadilifu,’ hata ikiwa mtu anayetuchukia anateseka au kutendewa isivyo haki.—Soma Methali 24:17, 18.

18 Paulo anaendelea kufafanua upendo kwa kusema kwamba upendo “huhimili mambo yote.” Mtu akitukosea na kutuomba msamaha, upendo utatuchochea kumsamehe. Upendo “huamini mambo yote” katika Neno la Mungu na kutuchochea kuthamini chakula cha kiroho tunachopokea. Upendo “hutumaini mambo yote” yaliyoandikwa katika Biblia na kutuchochea kuwaambia wengine sababu ya tumani letu. (1 Pet. 3:15) Tunapojaribiwa, tunasali na kutumaini kwamba hatimaye hali zitakuwa nzuri. Upendo “huvumilia mambo yote,” iwe ni dhambi tulizotendewa, na pia mateso au majaribu mengine. Zaidi ya yote, “upendo haushindwi kamwe.” Wanadamu watiifu wataonyesha sifa hiyo kwa umilele wote.

ENDELEA KUMPENDA JIRANI YAKO KAMA WEWE MWENYEWE
19 Tukifuata shauri la Biblia, tunaweza kuendelea kumpenda jirani yetu. Tunapaswa kuwapenda watu wote, si wa kabila letu tu. Tunahitaji pia kukumbuka maneno haya ya Yesu: “Mpende jirani yako kama wewe mwenyewe.” (Mt. 22:39) Mungu na Kristo wanatutazamia tumpende jirani yetu. Ikiwa ni vigumu kumpenda jirani yetu kwa sababu fulani, acheni tusali ili Mungu atuongoze kupitia roho takatifu. Tukifanya hivyo, Yehova atatubariki na kutusaidia kutenda kwa njia ya upendo.—Rom. 8:26, 27.

20 Amri ya kumpenda jirani yetu kama sisi wenyewe inaitwa “sheria ya kifalme.” (Yak. 2:8) Baada ya kutaja baadhi ya amri za Sheria ya Musa, Paulo alisema hivi: “Amri nyingine yoyote iliyoko, zimejumlishwa katika neno hili, yaani, ‘Mpende jirani yako kama wewe mwenyewe.’ Upendo haumfanyii uovu jirani ya mtu; kwa hiyo upendo ndio utimizo wa sheria.” (Rom. 13:8-10) Hivyo, tunapaswa kuendelea kumpenda jirani yetu.

21 Tunapotafakari kwa nini tunapaswa kumpenda jirani yetu, ni vizuri kukumbuka maneno ya Yesu kwamba Baba yake “hulichomoza jua lake juu ya watu waovu na wema na hunyesha mvua juu ya watu waadilifu na wasio waadilifu.” (Mt. 5:43-45) Tunahitaji kumpenda jirani yetu awe ni mwadilifu au si mwadilifu. Kama ilivyotajwa mwanzoni, njia muhimu ya kuonyesha upendo huo ni kuhubiri ujumbe wa Ufalme. Jirani yetu atapata baraka nyingi ikiwa atakubali na kuthamini kikweli habari njema.

22 Tuna sababu nyingi za kumpenda Yehova bila masharti. Pia, kuna njia nyingi tunazoweza kuonyesha kwamba tunampenda jirani yetu. Tunapompenda Mungu na jirani yetu, tunaonyesha kwamba tunatii maneno ya Yesu kuhusu mambo hayo muhimu. Zaidi ya yote, tunampendeza Yehova, Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo.

[Maswali ya Funzo]
1, 2. (a)Yesu alisema ni amri gani ya pili iliyo kuu katika Sheria? (b) Tutachunguza maswali gani?

3, 4. (a) Yesu alisimulia mfano gani ili kujibu swali: “Ni nani kwa kweli aliye jirani yangu”? (b) Msamaria alimsaidiaje mtu aliyekuwa ameibiwa, akapigwa, na kuachwa karibu kufa? (Tazama picha kwenye ukurasa huu.)

5. Watumishi wa Yehova walionyeshaje kwamba wanawapenda jirani zao wakati wa msiba wa asili uliotokea hivi karibuni?

6. Kazi yetu ya kuhubiri inahusianaje na kumpenda jirani?

7. Ile Kanuni Bora ni ipi, na tunabarikiwa jinsi gani tunapoifuata?

8. Kwa nini tunapaswa kuwapenda adui zetu, na huenda matokeo yakawa nini?

9. Yesu alisema nini kuhusu kufanya amani na ndugu yetu?

10. Kwa nini hatupaswi kutafuta-tafuta makosa ya wengine?

11, 12. Tunawaonyesha jirani zetu upendo kwa njia gani ya pekee?

13. Unahisije kuhusu kushiriki katika kazi yetu ya kuhubiri kuhusu Ufalme?

14. Kulingana na 1 Wakorintho 13:4-8, upendo unaweza kuonyeshwa kwa njia gani mbalimbali?

15. (a) Kwa nini tunapaswa kuwa wenye ustahimilivu na wenye fadhili? (b) Kwa nini tunapaswa kuepuka kuwa na wivu na kujigamba?

16, 17. Tunawezaje kutenda kulingana na 1 Wakorintho 13:5 na 6?

18. Tunajifunza nini kuhusu upendo katika 1 Wakorintho 13:7 na 8? 19, 20. Ni shauri gani la Biblia linalopaswa kutuchochea kuendelea

Comments