RUMAFRICA Magazine

RUMAFRICA FASHION

RUMAFRICA FASHION

MATUKIO KATIKA PICHA MIAKA SABA YA KANISA LA KISWAHILI LA READING NCHINI UINGEREZA




Balozi wa Tanzania nchini Uingereza mheshimiwa Peter Kallaghe aliwaongoza watanzania katika ibada ya kumshukuru Mungu kutimiza miaka 7 ya kanisa la kiswahili la Imani lililopo katika mji wa Reading nchini humo linaloongozwa na mchungaji Tumaini Kallage.

Ibada hiyo ambayo pia ilihudhuriwa na wachungaji kutoka huduma nyingine kama mtume Matthew Jutta wa Word changers ministry ya London, ilifanyika katika kanisa la Katoliki la Mtakatifu Andrew lililopo jirani na hospitali ya Royal Berkshire ambapo ndipo kanisa hilo hufanyia ibada zake kila jumapili ya tatu na ya nne kila mwezi kuanzia saa nane mchana. Viongozi wengine waliohudhuria ni pamoja na mchungaji kiongozi wa kanisa la Kilutheri jijini London Moses Shonga, Mchungaji Magreth wa Kenya sambamba na waimbaji wa kwaya ya Furaha London, Glory of God ministry International ya Reading walioongoza kipindi cha sifa, wenyeji Imani kwaya pamoja na kwaya ya watoto ya kanisani hapo.

Sambamba na kumshukuru Mungu, ibada hiyo ilitumika kumshukuru Mungu kwa matendo makuu aliyowatendea waumini hao kwa mwaka 2015, shukrani kwa Mungu kwa kuiwezesha Tanzania kumpata Rais John Magufuli sambamba na kumuombea afya njema na ulinzi. Pia kulifanyika ibada ya ubatizo kwa watoto.


Aidha mtume Jutta aliweza kuwabariki waumini waliofika kanisani hapo kwa kutoa neno la mahubiri la kuwataka waumini hao kutokuwaza ama kuambatana na watu wanaowaza kushindwa ama wasiwasi maishani mwao kwakuwa na wao wataingia katika mtego huo zaidi amewataka mwaka 2016 ukatumike kuwaza mafanikio na kuhakikisha malengo yao kutimia. Pia alitumia wasaa huo kupongeza juhudi zinazofanywa na Rais wa Tanzania katika kipindi kifupi alichokaa madarakani kwa kupasua majipu ama kupambana na kero ambazo watanzania wamekuwa wakizipigia kelele siku zote, na kuwataka watanzania kurudi nyumbani endapo maisha ya Uingereza yamewashinda kwakuwa mazingira ya nyumbani yameanza kukaa vizuri.


Aidha mara baada ya ibada, kanisa hilo lilitoa zawadi mbalimbali kwa watumishi na waumini ambao wamehusika kwa namna moja ama nyingine katika kuhakikisha huduma hiyo inasonga mbele. Kwa upande wake balozi Kallaghe aliwapongeza viongozi wa kanisa hilo na watanzania kwa ujumla waliofika kanisani hapo kwa umoja na kuliombea amani taifa lao. Pia balozi Kallaghe aliwataka waumini hao kuendelea kuiombea serikali na Rais Magufuli ili kazi aliyoianza basi ikazidi kuzaa matunda na kuineemesha Tanzania. Kwa upande mwingine balozi Kallaghe aliwaambia waumini hao ni kwa jinsi gani mataifa mengine ulimwenguni ikiwemo Uingereza jinsi wanavyoshangazwa na utendaji wenye nia ya mabadiliko unaofanywa na Rais Magufuli.

-
BONYEZA HAPA KUONA MATUKIO ZAIDI

Comments