RUMAFRICA Magazine

RUMAFRICA FASHION

RUMAFRICA FASHION

85% YA WAKUU WA MIKOA HAWARUDI

Rais Dk. John Pombe Magufuli

DAR ES SALAAM: Huku Rais Dk. John Pombe Magufuli akitarajiwa kutangaza uteuzi wa Wakuu wa Mikoa na Wilaya wakati wowote kuanzia sasa, uchunguzi unaonesha kuwa asilimia 85 ya viongozi wa sasa hawatarejea kwenye nafasi zao.

Uchunguzi huo uliozingatia vigezo mbalimbali, unaonesha kuwa licha ya wengi kupoteza kazi, lakini pia baadhi ya wakuu wa wilaya watapanda vyeo na kukabidhiwa mikoa.
Moja ya sababu itakayowaondoa viongozi hao ni kutokwenda na kasi ya rais katika utekelezaji wa majukumu yao ikiwa ni pamoja na uwezo wao wa kutatua kero za wananchi. Katika kundi hili, wapo wakubwa ambao wameshindwa kuondoa ugonjwa sugu wa kipindupindu, ambao unatoweka na kurejea kila baada ya muda mfupi.

Aidha, baa la njaa kwa baadhi ya mikoa na wilaya, linaonekana kuwa tatizo linaloweza kusababisha viongozi wake kushindwa kurejea ofisini, kwani suala hilo linaonekana kama ni uzembe, kwa vile sehemu kubwa ya nchi ina rutuba inayofaa kwa kilimo, isipokuwa wakulima wanakosa hamasa au bei kubwa ya pembejeo, kitu ambacho kingeweza kudhibitiwa.

“Suala la umri pia linaweza kuwa changamoto nyingine inayowakabili viongozi hao, kwani baadhi yao wanaonekana hawaendani na nyakati, lakini wako ambao muda wao wa kustaafu umewadia, hawa nao wana asilimia kubwa ya kutorudi,” alisema mchambuzi mmoja wa masuala ya siasa, aliyekataa kutajwa jina.

Katika kundi la viongozi hao ambao hawatarejea vyeo vyao, wapo pia ambao walisababisha Chama Cha Mapinduzi (CCM) kutopata ushindi mkubwa katika maeneo yao, wakati wa uchaguzi mkuu uliopita, ambao ulikuwa na ushindani mkubwa, kitu kinachotafsiriwa kama kukosa ubunifu au kukubalika kwa wakubwa hao katika maeneo hayo.

Wakati akihutubia taifa kupitia kwa wazee wa Jiji la Dar es Salaam hivi karibuni, Rais Magufuli alisema viongozi hao watapimwa na kuchaguliwa kwa utendaji wao wa kazi, akimtaja Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Paul Makonda kama mmoja wa viongozi ambao wanaweza kuwa na uhakika wa kuwepo katika safu mpya itakayoteuliwa.

Comments