RUMAFRICA Magazine

RUMAFRICA FASHION

RUMAFRICA FASHION

RAIS MAGUFULI ASALI IBADA YA JUMAPILI ARUSHA MJINI ATOA NENO



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli leo tarehe 08 Mei, 2016 ameungana na waumini wa Parokia ya Toleo la Bwana iliyopo katika Jimbo Katoliki la Arusha kusali ibada ya Jumapili, ambapo katika salamu zake amewaomba watanzania kuendelea kuiombea nchi yao ili kazi anayoifanya ya kukabiliana na matatizo yanayowakabili watanzania wanyonge ifanyike kwa mafanikio.
Dkt. Magufuli amesema hayo alipokaribishwa na Mwenyekiti wa Parokia hiyo Bw. Philemon Mushi kuwasalimu waumini wa kanisa hilo, mara baada ya kumalizika kwa ibada ya Jumapili ya kupaa kwa Bwana.
"Niko pamoja na nyinyi ndugu zangu watanzania na wana Arusha wote, napenda kuwaahidi tena sitawaangusha, nitasimama mbele kuwatetea masikini, siku zote nitakuwa upande wenu, siku zote nitatembea na nyinyi, nasema kwa dhati kabisa na nataka muamini hilo kwamba sitawaangusha" amesema Rais Magufuli huku akishangiliwa na waumini walioshiriki ibada hiyo.
Rais Magufuli amewahakikishia watanzania wote kuwa atahakikisha ahadi zote alizoziahidi anazitekeleza na amewaomba watanzania wote kuungana na kushikamana ili kufanikisha juhudi za kuijenga Tanzania bora.


"Ninajua kuongoza ni kazi kubwa, inajua kuongoza Taifa lililo masikini kama Tanzania inahitaji mkono wa Mungu, kwa hiyo niwaombe sana ndugu zangu Wakristo na watanzania kwa ujumla, muendelee kuliombea Taifa hili, kuniombea mimi, na pia kujiombea sisi wote ili amani tuliyonayo katika nchi yetu iendelee kudumu katika maisha yote


"lakini siku zote katika matendo yetu kila tunapofanya tumtangulize Mungu kwa sababu Mungu ndio kila kitu, lakini tutambue kwamba siku moja tutakufa, kwa hiyo ni vyema katika matendo yetu tutakapokuwa hapa duniani tujitahidi sana kufanya matendo mazuri kwa ajili ya watu na hasa watu wanyonge, ambao kwa kweli watanzania waliowanyonge wanapata shida sana" Amebainisha Rais Magufuli.


Pia Dkt. Magufuli amewasihi watanzania wote kuachana na ushabiki wa vyama vya siasa na badala yake waungane katika ujenzi wa Taifa na kukabiliana na kero zinazowaumiza.


Gerson Msigwa
Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano, IKULU
Arusha


08 Mei, 2016