Rais John Magufuli, leo amejumuika na waumini wa kanisa linaloongozwa na Mchungaji Antony Lusekelo maarufu kama mzee wa Upako, lililopo Ubungo Kibangu jijini Dar es Salaam.
Rais Magufuli, ambaye ni Mkatoliki, alishiriki ibada hiyo kwa nusu saa na kupewa nafasi ya kutoa machache, ambapo alimsifu Mzee wa Upako kwa huduma yake ya maombezi na kuahidi kuijenga barabara ya Kibangu inayoungana na ile ya Nelson Mandela.
Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano Ikulu, Grayson Msigwa amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kufafanua kuwa kilichompeleka hasa ni kuikagua barabara hiyo inayotokezea jeshini, aliyodai kuwa tayari fedha zake za ujenzi zimeshawekwa kwenye bajeti ya mwaka huu.
Hii ni mara ya pili kwa Rais Magufuli kusali katika makanisa tofauti na dhehebu lake, kwani mapema mwaka huu, alihudhuria ibada katika kanisa la KKKT usharika wa Azania Front.