RUMAFRICA Magazine

RUMAFRICA FASHION

RUMAFRICA FASHION

EPUKENI MANUNG’UNIKO

“Endeleeni kufanya mambo yote bila kunung’unika.”—WAFILIPI 2:14.

1, 2. Ni shauri gani ambalo mtume Paulo aliwapa Wakristo huko Filipi na Korintho, na kwa nini?

AKIONGOZWA kwa roho, mtume Paulo aliliandikia barua kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza huko Filipi na kulisifu sana. Aliwasifu waamini wenzake wa jiji hilo kwa sababu ya ukarimu wao na bidii yao, naye akaeleza jinsi alivyofurahia matendo yao mema. Hata hivyo, Paulo aliwakumbusha ‘waendelee kufanya mambo yote bila kunung’unika.’ (Wafilipi 2:14) Kwa nini mtume huyo alitoa shauri hilo?

2 Paulo alijua matokeo ya kunung’unika. Miaka kadhaa mapema, alilikumbusha kutaniko la Korintho kwamba kunung’unika kunaweza kuwa hatari. Paulo alisema kwamba wakati Waisraeli walipokuwa nyikani walimkasirisha Yehova tena na tena. Jinsi gani? Kwa kutamani mambo mabaya, kwa kuabudu sanamu na kufanya uasherati, kwa kumjaribu Yehova, na kwa kunung’unika. Paulo aliwatia moyo Wakorintho wajifunze kutokana na mifano hiyo. Aliandika hivi: “Wala tusiwe wanung’unikaji, kama baadhi yao walivyonung’unika, na kuangamizwa na mwangamizaji.”—1 Wakorintho 10:6-11.

3. Kwa nini tunapendezwa na habari ya kunung’unika?

3 Sisi watumishi wa Yehova leo tunaonyesha roho kama ya kutaniko lililokuwa Filipi. Tuna bidii katika matendo mema, nasi tunapendana. (Yohana 13:34, 35) Hata hivyo, tunapofikiria madhara yaliyowapata watu wa Mungu zamani kwa sababu ya kunung’unika, tuna sababu nzuri ya kutii shauri hili: “Endeleeni kufanya mambo yote bila kunung’unika.” Acheni kwanza tufikirie mifano ya watu walionung’unika ambayo inatajwa katika Maandiko. Kisha, tutazungumzia mambo fulani tunayoweza kufanya ili kuepuka kusababisha madhara kwa kunung’unika.

Kusanyiko Lenye Uovu Linamnung’unikia Yehova

4. Waisraeli walinung’unikaje nyikani?

4 Neno la Kiebrania linalomaanisha ‘kunung’unika au kulalamika’ linatumiwa katika Biblia kuhusiana na mambo yaliyotukia wakati Waisraeli walipokuwa nyikani kwa miaka 40. Mara kwa mara, Waisraeli walionyesha kwamba hawakuridhika na hali yao maishani, nao wakanung’unika kwa sababu hiyo. Kwa mfano, majuma machache tu baada ya kukombolewa kutoka utumwani Misri, ‘kusanyiko zima la wana wa Israeli lilianza kunung’unika juu ya Musa na Haruni.’ Waisraeli walilalamika kuhusu chakula, wakisema: “Laiti tungekufa kwa mkono wa Yehova katika nchi ya Misri tulipokuwa tukiketi kando ya vyungu vya nyama, tulipokuwa tukila mkate na kushiba, kwa sababu ninyi mmetutoa na kutuleta nyikani ili kuliua kutaniko lote kwa njaa.”—Kutoka 16:1-3.

5. Waisraeli waliponung’unika, walikuwa wakimnung’unikia nani hasa?

5 Lakini, Yehova alikuwa amewapa Waisraeli vitu walivyohitaji nyikani. Aliwapa chakula na maji kwa upendo. Waisraeli hawakukabili kamwe hatari ya kufa kwa njaa nyikani. Lakini, kwa sababu ya kutoridhika, walijifanya kwamba wanaumia sana, nao wakaanza kunung’unika. Ingawa walimlalamikia Musa na Haruni, machoni pa Yehova walikuwa wananung’unika hasa dhidi ya Mungu mwenyewe. Musa aliwaambia Waisraeli hivi: “Yehova amesikia manung’uniko yenu mnayonung’unika juu yake. Na sisi ni nani? Manung’uniko yenu si juu yetu, bali ni juu ya Yehova.”—Kutoka 16:4-8.

6, 7. Kama inavyoonyeshwa kwenye Hesabu 14:1-3, mtazamo wa Waisraeli ulibadilikaje?

6 Muda mfupi baadaye, Waisraeli walilalamika tena. Musa aliwatuma watu 12 kuipeleleza Nchi ya Ahadi. Kumi kati yao walirudi na ripoti mbaya. Ikawaje? “Wana wote wa Israeli wakaanza kunung’unika juu ya Musa na Haruni, na kusanyiko lote likaanza kusema dhidi yao: ‘Laiti tungalikufa katika nchi ya Misri, au laiti tungalikufa katika nyika hii! Na kwa nini Yehova anatuleta kwenye nchi hii [Kanaani] ili tuanguke kwa upanga? Wake zetu na watoto wetu wadogo watakuwa nyara. Je, si afadhali kwetu turudi Misri?’”—Hesabu 14:1-3.

7 Mtazamo wa Waisraeli ulikuwa umebadilika kama nini! Mwanzoni, walipowekwa huru kutoka Misri na kukombolewa kupitia Bahari Nyekundu, uthamini wao uliwachochea kumwimbia Yehova sifa. (Kutoka 15:1-21) Lakini kwa sababu ya matatizo ya nyikani na kuwaogopa Wakanaani, watu wa Mungu walipoteza uthamini wao na kuonyesha mtazamo wa kutoridhika. Badala ya kumshukuru Mungu kwa uhuru aliowapa, walimlaumu kwa sababu walidhani kwamba wamekosa vitu fulani. Hivyo, kunung’unika kulionyesha kwamba hawakuthamini maandalizi ya Yehova. Haishangazi kwamba Yehova alisema hivi: “Kusanyiko hili lenye uovu litaendelea kuwa na manung’uniko haya ambayo linaendeleza juu yangu mpaka wakati gani?”—Hesabu 14:27; 21:5.

Manung’uniko Katika Karne ya Kwanza

8, 9. Toa mifano ya watu walionung’unika ambayo inatajwa katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo.

8 Mifano hiyo kuhusu manung’uniko ilihusisha vikundi vya watu ambao yaonekana walionyesha waziwazi kwamba hawakuridhika. Hata hivyo, wakati Yesu Kristo alipokuwa Yerusalemu kwa ajili ya Sherehe ya Vibanda mwaka wa 32 W.K., “umati ulikuwa ukinong’onezana mambo mengi juu yake.” (Yohana 7:12, 13, 32) Walikuwa wakinong’onezana kumhusu Yesu, wengine wakisema kwamba yeye ni mtu mwema na wengine wakisema yeye si mwema.

9 Pindi nyingine, Yesu na wanafunzi wake walikaribishwa katika nyumba ya yule mkusanya-kodi aliyeitwa Lawi, au Mathayo. “Mafarisayo na waandishi wao wakaanza kuwanung’unikia wanafunzi wake, wakisema: ‘Kwa nini mnakula na kunywa pamoja na wakusanya-kodi na watenda-dhambi?’” (Luka 5:27-30) Baadaye, huko Galilaya, “Wayahudi wakaanza kumnung’unikia [Yesu] kwa sababu alisema: ‘Mimi ndio mkate ambao ulishuka kutoka mbinguni.’” Hata baadhi ya wafuasi wa Yesu waliudhika kwa sababu ya mambo aliyosema, nao wakaanza kunung’unika.—Yohana 6:41, 60, 61.

10, 11. Kwa nini Wayahudi wenye kusema Kigiriki walinung’unika, na wazee Wakristo wanaweza kufaidikaje kutokana na jinsi malalamiko hayo yalivyoshughulikiwa?

10 Muda mfupi baada ya Pentekoste 33 W.K., kulikuwa na kisa fulani cha kunung’unika ambacho kilikuwa na matokeo mazuri. Wanafunzi wengi wapya kutoka nchi za nje ya Israeli walikuwa wakifurahia ukarimu wa waamini wenzao huko Yudea. Lakini matatizo fulani yalizuka kuhusiana na ugawaji wa maandalizi yaliyokuwepo. Simulizi linasema hivi: “Wayahudi wenye kusema Kigiriki walianza kunung’unika juu ya Wayahudi wenye kusema Kiebrania, kwa sababu wajane wao walikuwa hawaangaliwi katika ugawaji wa kila siku.”—Matendo 6:1.

11 Wanung’unikaji hao walikuwa tofauti na Waisraeli nyikani. Wayahudi wenye kusema Kigiriki hawakulalamika kwa ubinafsi kuhusu matatizo yao wenyewe. Badala yake, walisema kwamba wajane fulani hawakuwa wakitimiziwa mahitaji yao. Isitoshe, wanung’unikaji hao hawakuzusha fujo wala hawakulalamika kwa sauti dhidi ya Yehova. Waliwaeleza mitume malalamiko yao, nao mitume wakapanga hatua ichukuliwe haraka kwa sababu malalamiko hayo yalifaa. Huo ni mfano bora sana ambao mitume waliwawekea wazee Wakristo leo! Wachungaji hao wa kiroho huepuka ‘kuziba masikio yao ili wasikie kilio cha kulalamika cha mtu wa hali ya chini.’—Methali 21:13; Matendo 6:2-6.

Jihadhari na Madhara ya Kunung’unika

12, 13. (a) Toa mfano unaoonyesha madhara ya kunung’unika. (b) Ni nini kinachoweza kumfanya mtu anung’unike?

12 Mifano mingi ya Kimaandiko ambayo tumezungumzia inaonyesha kwamba manung’uniko yaliwaathiri sana watu wa Mungu wa kale. Basi, tunapaswa kufikiria kwa uzito madhara ambayo yanaweza kutokea leo kwa kunung’unika. Hebu fikiria mfano huu. Vyuma vingi vinaweza kushika kutu. Mtu asipochukua hatua mapema wakati anapogundua kwamba chuma kimeshika kutu, chuma hicho kinaweza kuliwa na kutu mpaka kisiwe na faida yoyote. Magari mengi sana yameharibika, si kwa sababu ya matatizo ya injini, bali kwa sababu vyuma vyake vimeliwa na kutu kabisa hivi kwamba ni hatari kutumia magari hayo. Tunaweza kutumiaje mfano huo kuhusiana na kunung’unika?

13 Kama vile vyuma fulani hushika kutu, wanadamu wasio wakamilifu wana mwelekeo wa kulalamika. Tunapaswa kuwa chonjo kugundua dalili yoyote ya kutaka kulalamika. Kama vile unyevu na hewa yenye chumvi hufanya chuma kishike kutu haraka, taabu zinaweza kutufanya tutake sana kunung’unika. Mkazo unaweza kufanya tuudhike sana tunaposumbuliwa kidogo. Kadiri hali zinavyozidi kuwa mbaya katika siku hizi za mwisho za mfumo huu, mambo yanayoweza kufanya tulalamike huenda yataongezeka. (2 Timotheo 3:1-5) Hivyo, huenda mtumishi mmoja wa Yehova akaanza kunung’unika kuhusu mtumishi mwenzake. Huenda akanung’unika kwa sababu ndogo, kama vile udhaifu wa mwingine, uwezo wake, au mapendeleo yake ya utumishi.

14, 15. Kwa nini tunapaswa kuchukua hatua dhidi ya mwelekeo wa kulalamika?

14 Hata tuwe tumekasirishwa na jambo gani, tusipodhibiti mwelekeo wetu wa kutaka kulalamika, tunaweza kusitawisha mtazamo wa kutoridhika na vilevile tabia ya kunung’unika. Naam, kunung’unika kunaweza kutudhoofisha kabisa kiroho. Waisraeli waliponung’unika kuhusu maisha yao nyikani, walimlaumu hata Yehova. (Kutoka 16:8) Acheni tuepuke kufanya hivyo!

15 Uwezekano wa chuma kuharibiwa na kutu unaweza kupunguzwa kwa kukipaka rangi ya kuzuia kutu na kurekebisha haraka sehemu zilizoliwa. Vivyo hivyo, tukigundua kwamba tuna mwelekeo wa kulalamika, tunaweza kuudhibiti kwa kusali na kuchukua hatua haraka kujirekebisha. Tunaweza kufanyaje hivyo?

Ona Mambo Kama Yehova

16. Tunaweza kushindaje mwelekeo wa kulalamika?

16 Tunaponung’unika tunakazia fikira shida zetu, tunajifikiria wenyewe, na kusahau baraka tunazopata tukiwa Mashahidi wa Yehova. Ili kushinda mwelekeo wa kulalamika, tunahitaji kujikumbusha baraka hizo. Kwa mfano, kila mmoja wetu ana pendeleo zuri la kutambulishwa kwa jina la Yehova. (Isaya 43:10) Tunaweza kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja naye, nasi tunaweza kuzungumza na “Msikiaji wa sala” wakati wowote ule. (Zaburi 65:2; Yakobo 4:8) Maisha yetu yana kusudi kwa sababu tunaelewa suala la enzi kuu ya ulimwengu wote na tunakumbuka kwamba tuna pendeleo la kudumisha utimilifu wetu kwa Mungu. (Methali 27:11) Tunaweza kuhubiri habari njema ya Ufalme kwa ukawaida. (Mathayo 24:14) Imani katika dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo hutuwezesha kuwa na dhamiri safi. (Yohana 3:16) Hizo ni baraka tunazopata haidhuru tuna matatizo gani.

17. Kwa nini tunapaswa kujitahidi kuona mambo kama Yehova, hata ikiwa tuna sababu nzuri ya kulalamika?

17 Acheni tujitahidi kuona mambo kama Yehova, bali si kulingana na maoni yetu. Mtunga-zaburi Daudi aliimba hivi: “Nijulishe njia zako, Ee Yehova; nifundishe mapito yako mwenyewe.” (Zaburi 25:4) Ikiwa tuna sababu nzuri ya kulalamika, Yehova anaiona. Anaweza kusuluhisha jambo hilo sasa hivi. Basi, kwa nini nyakati nyingine yeye huruhusu shida ziendelee? Huenda ni kwa sababu anataka kutusaidia tusitawishe sifa nzuri, kama vile subira, uvumilivu, imani, na ustahimilivu.—Yakobo 1:2-4.

18, 19. Toa mfano kuonyesha faida zinazoweza kutokea tunapovumilia hali ngumu bila kulalamika.

18 Kuvumilia hali ngumu bila kulalamika hutusaidia kuboresha utu wetu na vilevile kuwavutia wale wanaotazama mwenendo wetu. Katika mwaka wa 2003, kikundi fulani cha Mashahidi wa Yehova kilisafiri kwa basi kutoka Ujerumani ili kuhudhuria kusanyiko Hungaria. Dereva wa basi hilo hakuwa Shahidi, naye hakufurahia wazo la kwamba angekuwa na Mashahidi hao kwa siku kumi. Hata hivyo, baada ya safari, maoni yake yalibadilika kabisa. Kwa nini?

19 Wakati wa safari hiyo, kulikuwa na matatizo fulani. Lakini Mashahidi hawakulalamika. Dereva huyo alisema kwamba hicho ndicho kikundi bora zaidi cha abiria ambacho amewahi kuhudumia! Hata aliahidi kwamba wakati ambapo Mashahidi watamtembelea nyumbani kwake, atawakaribisha na kuwasikiliza kwa makini. Naam, abiria hao walimvutia mtu huyo sana kwa “kufanya mambo yote bila kunung’unika”!

Msamaha Huendeleza Umoja

20. Kwa nini tunapaswa kusameheana?

20 Namna gani ikiwa tuna sababu ya kulalamika kuhusu mwamini mwenzetu? Ikiwa ni jambo zito, tunapaswa kutumia kanuni zinazotajwa katika maneno ya Yesu kwenye Mathayo 18:15-17. Hata hivyo, nyakati nyingine si lazima tufanye hivyo kwa kuwa mara nyingi watu hutukosea katika mambo madogo. Kwa nini tusione hali hiyo kuwa nafasi ya kusamehe? Paulo aliandika hivi: “Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwingine. Kama vile Yehova alivyowasamehe ninyi kwa hiari, nanyi fanyeni vivyo hivyo pia. Lakini, zaidi ya mambo haya yote, jivikeni upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha muungano.” (Wakolosai 3:13, 14) Je, tuko tayari kusamehe? Yehova ana sababu ya kulalamika juu yetu. Lakini, yeye huendelea kutuhurumia na kutusamehe.

21. Wale wanaosikiliza manung’uniko wanaweza kuathiriwaje?

21 Hata tuwe tumekosewa kwa njia gani, kunung’unika hakutatatua matatizo. Neno la Kiebrania linalomaanisha “kunung’unika” linaweza pia kumaanisha “kulalamika kwa hasira.” Yaelekea sisi huhisi vibaya tunapokuwa karibu na mtu mwenye tabia ya kunung’unika, nasi hujitahidi juu chini kumwepuka. Tukinung’unika, au kulalamika kwa hasira, wale wanaosikiliza wanaweza kuhisi vibaya pia. Wanaweza kuhisi vibaya sana na hata kutuepuka! Mtu anaweza kutusikiliza tunaponung’unika, lakini hatavutiwa nasi.

22. Msichana mmoja alisema nini kuhusu Mashahidi wa Yehova?

22 Kusamehe huendeleza umoja, na watu wa Yehova wanathamini sana umoja. (Zaburi 133:1-3) Katika nchi moja ya Ulaya, msichana mmoja Mkatoliki mwenye umri wa miaka 17 aliiandikia ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova ili kueleza jinsi anavyovutiwa nao. Alisema hivi: “Hilo ndilo tengenezo moja tu ninalojua ambalo washiriki wake hawagawanywi na chuki, pupa, ubaguzi, ubinafsi, wala utengano.”

23. Tutazungumzia nini katika makala inayofuata?

23 Kuthamini baraka zote za kiroho tunazopata tukiwa waabudu wa Mungu wa kweli, Yehova, kutatusaidia kuendeleza umoja na kuepuka kunung’unika dhidi ya wengine katika mambo ya kibinafsi. Makala inayofuata itaonyesha jinsi sifa za kiroho zinavyoweza kutuzuia tusihusike katika aina fulani hatari ya kunung’unika, yaani, kunung’unika kuhusu sehemu ya kidunia ya tengenezo la Yehova.

Je, Unakumbuka?

• Kunung’unika kunahusisha nini?

• Ni mfano gani unaoweza kuonyesha madhara ya kunung’unika?

• Ni mambo gani yanayoweza kutusaidia kushinda mwelekeo wa kunung’unika?

• Kuwa tayari kusamehe kunaweza kutusaidiaje kuepuka kunung’unika?

Waisraeli walinung’unika dhidi ya Yehova mwenyewe!

Je, wewe hujitahidi kuona mambo kama Yehova?