RUMAFRICA Magazine

RUMAFRICA FASHION

RUMAFRICA FASHION

SIKU MWALIMU NYERERE ALIPOFANYA MAAMUZI MAGUMU

ILIKUWA mwaka 1955 mwalimu Julius Kambarage Nyerere aliamua kufanya maamuzi magumu ya kuamua kuachana na kazi yake ya ualimu kwenye Shule ya Sekondari Pugu iliyokuwa ikimpa kipato cha kujikimu na kuendesha maisha yake.

Alifanya maamuzi hayo ya kuachana na kazi yake hiyo na kuingia rasmi kwenye shughuli za kisiasa kupitia chama cha Tanganyika African National Union(TANU), ambazo kwa wakati huo hazikuwa na malipo zaidi ya kujitolea na wakati mwingine zilipelekea mtu kutiwa hatiani na kubambikiwa kesi.

Barua iliyoandikwa na Mwalimu Nyerere baada ya kufanyiwa tafsiri kutoka lugha ya Kiingereza kwenda lugha ya Kiswahili.


Mpendwa Padri,

Nimelifikiria chaguo ulilonipa, kati ya kazi yangu shuleni na uanachama wangu katika T.A.N.U na nimefikia uamuzi kwamba lazima nijiuzulu katika nafasi yangu shuleni.

Lakini sasa najikuta nimekabiliwa na chaguo kama hilo. Kwa vile TANU inaingiliana na kazi yangu shuleni, suala hilo ni la kibinafsi na hivi karibuni au baadaye nitalazimika kupunguza shughuli zangu katika TANU au kuchagua kati ya TANU na shule. Katika hali hiyo chaguo lingekuwa la kweli; na kama ningegundua kwamba nisingeweza kuyafanya mambo yote hayo mawili kikamilifu ni dhahiri kwamba ningeiacha shule na kwenda kushughulika na TANU. Lakini iwapo kujiuzulu kutoka TANU kutanifanya niendelee na kazi yangu, suala hilo linakuwa ni la uamuzi wa kikanuni. Ni nani nchini Tanganyika yuko huru kujiunga na kuiongoza TANU? Kinadharia ni watu wote wasiokuwa waajiriwa wa serikali. Katika hali halisi nafahamu kwamba waajiriwa wa serikali za mitaa hawako huru, au ni kwamba hawana uhuru kuliko walimu wa mamlaka za kidini. Na kama uhuru wa walimu hao wa kidini utatiliwa mashaka, hali ingekuwa ya mashaka kwani sioni sababu yoyote kwa nini kila mwajiri asitoe masharti kama hayo kwa waajiriwa wake; na uwezekano huo ungekuwa wa kusikitisha. Kwa hiyo, ni lazima nijiuzulu kama njia ya kupinga hali hiyo.

Ninasikitika kwamba shughuli zangu katika TANU ni dhahiri zimeathiri utendaji wangu wa kufundisha; ninasikitika kuhusu matatizo ambayo yatajitokeza kwako na kwa wenzangu kwa muda kutokana na kujiuzulu kwangu; ninasikitika pia kwa matokeo ya kiuchumi ambayo yataikumba familia yangu.

Ningekuwa katika nafasi yako, Padri, ningefanya kama ulivyofanya wewe; tumaini langu pekee ni kwamba utaona inawezekana kwamba ungekuwa katika nafasi niliyo nayo mimi ungechukua hatua kama ambayo nimeichukua.

Nakushukuru wewe na Mapadri wengine kutokana na kushirikiana nami siku zote. Nitazihitaji sala zenu zaidi kuliko ilivyokuwa hapo nyuma. Endelea, Padri, kuniombea.

Mwanao mpendwa katika Kristo,



Julius Nyerere.

Nakala ya barua halisi iliyoandikwa na Mwalimu Nyerere


Baada ya kuandika barua hiyo rasmi Mwalimu Nyerere alijiunga na chama cha TANU.

Mwalimu Nyerere kutokana na uzalendo wake mkubwa kwa taifa hili aliamua kujitoa mhanga na kupoteza malipo yake ya ualimu na kuingia katika mapambano ya kudai uhuru ambako hatma yake Desemba 9, 1961 alifanikisha nchi yetu kuwa huru na tangu wakati huo tupo huru mpaka leo.

Picha mbali mbali za Mwalimu Nyerere enzi za uhai wake.





Uzalendo huu wa Nyerere ni wa kuigwa na mfano kwa viongozi wengine ambao siku zote wanapaswa kuweka kwanza maslahi ya taifa mbele, haijalishi wataumia kiasi gani. Ametufundisha jambo kubwa na muhimu rejea kwenye barua yake aliyoiandika nanukuu “ninasikitika pia kwa matokeo ya kiuchumi ambayo yataikumba familia yangu.” Katufundisha kwamba ukidhamiria kuitumikia nchi yako kwa uadilifu hutaogopa wewe au familia yako kuteseka na njaa, lazima ujitoe bila kujali ni kiasi gani utaumizwa na maamuzi yako, Taifa kwanza.

(picha zote za Mwalimu Nyerere ni zile zilizopigwa enzi za uhai wake wakati akiitumikia nchi yake kwa uadilifu mkubwa)

Imeandaliwa na;

Leonard Msigwa/GPL/MTANDAO.