RUMAFRICA Magazine

RUMAFRICA FASHION

RUMAFRICA FASHION

FAHAMU NJIA ZA KUPATA MARAFIKI NA KUDUMISHA URAFIKI


Je, unafahamu jinsi ya kupata marafiki na kudumisha urafiki?

Hapana shaka wewe msomaji wangu una marafiki. Je, unaridhika na idadi ya marafiki ulionao? Kama hauridhiki, je, unajua namna ya kupata marafiki wapya na kudumisha urafiki na wale ulionao? Kama hujui usiwe na wasiwasi bali endelea kusoma makala hii.

Katika utafiti mdogo niliofanya kabla ya kuandika makala hii niligundua kuwa karibuni kila mtu ana zaidi ya rafiki mmoja. Wapo wachache walioniambia kuwa ingawa kuna watu wengi waliozoeana nao lakini hawana hakika kama wote ni marafiki zao. Hata wale waliosema wana marafiki wengi, walikiri kuwa hawaamini kama wote ni marafiki wa kweli. Mwisho nimeamua niandike kwa ujumla tu kuhusu namna ya kupata marafiki ili wale wasio nao waweze kuwapata na wale wanaofikiria wana marafiki wachache waweze kuongeza wengine.

Hata hivyo, kabla sijaendelea hebu tujiulize swali jingine. Je inafaa mtu kuwa na marafiki wangapi? Watu wengi niliowauliza swali hili walisema ni vyema kuwa na marafiki wengi. Kuna wengine walisema kuwa ni vyema kuwa na marafiki wachache wa kweli kuliko kuwa na utitiri wa marafiki. Rafiki yangu mmoja aliniambia inafaa kuwa na rafiki katika kila sekta muhimu ya maisha kama vile kuwa na rafiki mwalimu, daktari, mwanasheria, askari na mfanyabiashara.

Wale waliopendelea kuwa na marafiki wengi walisisitiza kuwa kadri unavyokuwa na marafiki wengi ndivyo kadri utavyokuwa na maisha mazuri zaidi. Kwani hata unapokuwa na shida au unapopatwa na maafa utakuwa na marafiki wengi watakaopata imani ya kukusaidia.

Kwa hakika kuwa na marafiki wengi ni vyema zaidi. Kila mara ninaposimulia kuhusu suala la kuwa na marafiki wengi huwa nakumbuka habari za mahali fulani ambako watu maarufu, hata kama hawakuwa na ndugu na marafiki wengi, walipendelea msiba unapotokea nyumbani kwao wahudhurie watu wengi ili msiba uonekane mkubwa. Hivyo, msiba ulipotokea nyumbani kwa mtu maarufu asiye na ndugu, jamaa na marafiki wengi walikodisha kikundi chenye watu wengi na walio mabingwa wa kulia na kuomboleza kwenye msiba. Wanapofika huwekwa mahali pa faragha wakapatiwa maelezo kuhsu jina, wasifu na tabia ya mtu aliyefariki na nasaba yake na mfiwa. Vile vile hufahamishwa jina na sifa za mtu aliyefiwa. Mbinu hii ilikuwa ikisaidia kuonyesha kuwa mfiwa ama ukoo mkubwa na ndugu na marafiki wengi. Hata hivyo, wakati mwingine kama kulitokea makosa katika kuwapatia maelezo waombolezaji waliweza kulia wakisema “Maskini ndugu yetu aliyekuwa mfadhili wetu umetutoka sasa nani atatusaidia tutakapopatwa na shida waliomboleza hivyo wakati aliye fariki alikuwa ni mtoto wa miaka miwili tu, watu wakabaki wakiwatazama huku wameshangaa.



Mambo yanayotusaidia kupata marafiki

Inatupasa tukumbuke kuwa suala la kupata marafiki sio jambo la bahati, kuwa na fedha nyingi au haiba kubwa. Kuna watu wenye fedha na hadhi kubwa lakini hawana marafiki. Kuna useni kuwa “Urafiki hujengeka kati ya watu kutokana na mambo kadhaa yanayoweza kutokea baina yao” Yafuatayo ni baadhi ya mambo ambayo yakizingatiwa huweza kumsaidia mtu kupata marafiki na kuimarisha upendo kwa wale alionao.

1. Kujenga mawasiliano na hali ya kukutana mara kwa mara

Urafiki huibuka kati ya watu wanaowasiliana na kuweza kututana mara kwa mara. Utafiti umeonyesha kuwa watu wanaoishi katika makazi yaliyo karibu karibu wana uwezo wa kujenga urafiki zaidi. Hususani imebainika kuwa wale wanaoishi katika maghorofa au katika nyumba zilizo katika makambi kama ya majeshi au nyumba za Shirika la Nyumba huwa wanaunda urafiki mara nyingi zaidi kuliko wanaokaa katika makazi yaliyo mbali mbali. Kwa muhtasari, kadri unavyoishi karibu na mtu mwingine ndivyo kadri mnavyokuwa na mawasiliano na kuonana mara kwa mara jambo ambalo hufanya iwe rahisi kwa yeye kutokea kuwa rafiki yako na pengine hata kuwa rafiki wa kweli. Vile vile watu wanaopata fursa ya kuwa pamoja kwa muda mrefu katika shughuli kama vile shuleni au mafunzoni au kazini huweza kujenga urafiki iwapo wahusika wataamua kuwa marafiki. Watu wengi wamepata marafiki wa kudumu na wake au waume kutokana na wale waliokutana nao shuleni au kazini. Licha ya kuwa karibu kutokana na makazi, elimu na kazi, watu hujumuika pia katika shughuli za kijamii kama vile burudani au maafa ambazo pia hutoa fursa ya kujenga urafiki. Katika mikutano hii inayokutanisha na watu fulani mara kwa mara chukua anwani za wale wenye mwalekeo wa kuwa marafiki na hatimaye anzisha mawasiliano yanayoweza kujenga urafiki.

2. Kuwa mwenye kuthubutu

Kuna watu ambao katika maisha ya kawaida huwa wanaitwa watu wenye uchakalamu yaani wanapokuwa kwenye kundi la watu ni lazima watafanya mambo ambayo yatamfanya kila mtu atambue kuwepo kwao. Kwa upande fulani mwenendo huu huweza kuchukuliwa kama tabia mbaya lakini kwa upande mwingine ndiyo inayomwezesha mtu kupata marafiki. . Anza kwa kujitambulisha wewe na kisha muombe akufahamisha yeye ni nani. Baadaye anzisha maongezi yatakayowafanya mfahamiane na kukutana mara kwa mara mahali hapo na hatimaye majumbani mwenu.

Kila itakapotokea nafasi ya wewe kuweza kumsaidia mtu yeyote uliyekutana naye katika namna hii itumie ili uonekane kuwa ni rafiki. Msaada huo sio lazima uwe wa kitu unaweza kuwa msaada wa ushauri au mawazo.

3. Kuwa msikivu na mtu anayesogeleka

Kila mtu hupenda kusikilizwa. Mtu huwaona ni rafiki wale watu wanaomuonyesha wanamfurahia na kumjali. Ili uweze kupata marafiki huna budi kuwa na uwezo wa kuwafanya watu wote unaokutana nao na kuongea nao wajihisi unawafurahia na unawajali. Wataalamu wa saikolojia husema kuwa “Katika miezi miwili unaweza kupata marafiki wengi kwa kuwaonyesha watu kuwa unawathamini na unawajali kuliko idadi utakayopata katika miaka miwili kwa kujaribu kuwafanya watu wakuthani na kukujali wewe”. Wataalamu hao wanasisitiza dhana hii kwa kusema, “Unawezaje kufanya watu wakupende au wawe na mvuto kwako iwapo wewe hutawaonyesha kuwa unawathani na kuwajali. Hivi ni vitu ambavyo huashiria kuwa unawapenda”

4. Kuwa na maongezi ya kusisimua

Pamoja na kuwa msikivu na unayesogeleka bado kuna sifa nyingine muhimu ambayo inabidi uwenayo ili uwe na mvuto kwa watu ambao wangeweza kuwa marafiki watarajiwa. Kila unapokuwa na maongezi na mtu mmoja au kundi la watu hakikisha una jambo la kusisimua litakalowapendeza na kuwachangamsha. Katika mikusanyiko ya watu hufurahi sana kama miongoni mwao huwepo mtu anayewaeleza mambo ya kupendeza na kuwavutia.

5. Fanya watu wakufahamu

Kadri watu wanavyokufahamu na kuelewa tabia na hisia zako ndivyo kadri unavyojiongezea fursa za kuweza kupata marafiki. Kama unataka watu wakukubali na kukupenda huna budi kuwapatia nafasi ya kufahamu jinsi unavyojisikia jinsi unavyofikiri na unavyotenda shughuli zako. Inabidi ukubali ukweli kuwa watu wanavyojua fikra na hisia zako kuna wale watakaokukubali na wengine kutokukupenda. Hii ni kanuni ya maisha ambayo haiwezi kubadilika. Aidha, kumbuka kadri utakavyojitahidi kuzuia watu wasikuchukie ndivyo kadri utakavyokuwa unazuia watu wasikupende.

6. Dhibiti hasira zako

Jambo moja lenye utata na ambalo huweza kuathiri na hata kuharibu mahusiano na urafiki ni hasira. Hata hivyo wanasaikolojia wamethibitisha kuwa mtu anaweza kumuonyesha rafiki yake kuwa amechukia na bado wakaendeleza urafiki wao. Wahenga waliwahi kusema “Muungwana hakasiriki kwa mashavu” Hata kama umekasirika epuka kuwakaripia marafiki zako watarajiwa au wale marafiki halisi. Katika mazingira ambayo unalazimika kumkasirikia rafiki yako zungumza naye kwa upole na utulivu kwa kuwa maneno makali mara nyingi huumiza.

Hitimisho

Kadri utakavyoweza kuzikusanya juhudi zako ukaweza kuanzisha mahusiano na watu unawaona wanafaa ndivyo kadri utakavyokuwa umo katika mstari wa kuelekea kwenye mafanikio ya kuwa na marafiki wengi.