RUMAFRICA Magazine

RUMAFRICA FASHION

RUMAFRICA FASHION

MAPARACHICHI NA MAPAPAI: WAFALME WA MATUNDA …


MATUNDA AGHALI KUZIDI YOTE UZUNGUNI NDIYO PIA YENYE THAMANI KIAFYA

Afrika imejaaliwa mimea, madini, rutuba na hali ya hewa safi.
Takribani vyakula vyote tunavyohitaji wanadamu hupatikana bara hili. Lakini pamoja na hayo uhai wetu mfupi kuzidi wengine duniani. Kufuatana na orodha ya wastani wa maisha iliyotolewa na shirika la Ujasusi Marekani (CIA)na Umoja wa Mataifa mwaka 2011- nchi zinazoongoza kwa maisha marefu ni Japani na chini kabisa ni Afrika.
Wajapani wanaishi hadi miaka 90 kuendelea , Ulaya, Marekani na China kati ya 75 hadi 90; nchi za bara Asia (mathalan India) miaka 65 kuendelea; mwisho ni Afrika yenye taifa la Angola mkiani (miaka 40). Tanzania imewekwa na wastani wa miaka 50 hadi 53.
Msingi wa sababu zinazowafanya watu wasiishi muda mrefu ni maendeleo ya uchumi-jamii na siasa.
Lakini kiini cha wewe kuishi (mbali na elimu, makazi bora na furaha moyoni )ni CHAKULA BORA NA NAMNA UNAVYOKILA.

Wajapani mathalan wanasifika kwa kula vyema- hawali misosi mikubwa mikubwa kama sisi. Ulaji wao ni mdogo mdogo, wa mara kwa mara- hawajazi sana matumbo. Halafu kuna vitu wanavyokula ambavyo husaidia sana kukarabati na kuhifadhi mwili. Mfano mzuri ni mimea ya baharini. Kuna mmea uitwao Kombu ambao unauchemsha na kuyatumia maji yake kwa kupikia mchuzi, chai, nk. Moja ya faida ya “Kombu” ni kukinga na kuuponyesha mwili kutokana na maradhi; pili, kuongeza nguvu za nywele, ngozi na maisha kijumla. Ndiyo maana nadra sana kumwona Mjapani asiyekua na nywele nyingi, hata akiwa mzee- huwaoni wana mvi. Mvi ni dalili ya ukosefu wa madini mwilini.
Wana afya.
Mbegu mbichi kama hizi za Maboga zina faida kubwa sana mwilini : mafuta asilia yasiyodhuru moyo-kama nyama, kinga maradhi, ujenzi na kukarabati ngozi, mifupa, kucha, nywele, kuupa mwili nguvu za rijali nk.

Wenzetu nchi zilizoendelea wanathamini sana matunda na mboga mboga. Si ajabu leo wanaishi maisha marefu kutuzidi.
Sisi tumevijaza vyote hivi, TELE, lakini hatuvithamini.
Zamani nikiwa mtoto ilikuwa kawaida mapishi kuwa na mboga za majani na saladi (kachumbari) leo kutokana na kuingizwa kwa utamaduni wa “vyakula vya haraka “ (“junk”) na “ladha” –vyenye CHUMVI NA MAFUTA MAFUTA MENGI YA KUKAANGA kama chips, nyama choma nk, hatuli sana mboga mbichi mbichi za majani. Na zikipikwa zinachemshwa hadi zinageuka nyani.
Mchanganyiko wa matango na brokoli, nilioutayarisha kwa “mvuke” – yaani kubandika sufuria yenye hizo mboga juu ya nyingine inayochemka chini yake. Upishi huu “barabara” hufanya mboga zisiunguzwe au kuiva sana- zinabakia imara.


WANGAPI TUNAKULA MATUNDA KWA WINGI AFRIKA?
Kiafya unatakiwa ule matunda aina tano kwa siku kupata faida zake zote mwilini.
Faida za matunda hazihesabaki. Na hayatakiwi yaliwe pamoja na chakula- bali kabla- AU KATI KATI YA MILO MIKUBWA. baadaye. Tabia yetu wengi kuchanganya matunda na milo mikubwa kama wali, ugali, chapati na kadhalika – hausaidii – ni afadhali hata usile kabisa.
Ndizi mbivu toka visiwa vya Caribbean – huwa za aina moja tu. Hii ni kama ndizi tunayoita “mchare” kule Uchaggani.

Matunda humeng’enywa kwa vimeng’enyo tofauti na vyakula mama (wanga, protini, nk). Kati ya faida kuu za matunda ni:
1. Zuia maradhi , rutubisha na kinga mwili
2. Sukari , nguvu na mafuta asilia
3. Madini na Vitamin mbalimbali yanayosaidia kujenga, kukarabati na hata kuzuia bakteria na maadui wakubwa wakubwa wa miili yetu mathalan “free radicals”- tunaweza kulinganisha “free radicals” na majivu yanayobakia baada ya moto kuwaka. Hutolewa mwilini kama taka au kuingia mwilini kutokana na uchafu wa mazingira, mioshi ya sigara na magari, taka taka za mashine za kisasa – tena siku hizi wengi tunalala na simu za mkononi zikiwa zimewashwa, tunazibeba kwa wingi. Taka au majivu haya ndiyo kiini kikuu cha maradhi ya kisasa (nchi zilizoendelea) mathalan saratani.
Ukipita maduka ya Uzunguni utakuta vyakula mbalimbali vinauzwa toka Afrika. Matunda haya yanayothaminiwa sana Majuu, huuzwa bei aghali sana.
Hapa London ambapo kila aina ya chakula ulimwenguni hupatikana bei za matunda ziko hivi, kiwastan:
1. Kichani kimoja cha ndizi kisukari (mara nyingi toka visiwa vya Ngazija au Mauritius) ni £2-£3. Kama shilingi 6-7,000. Ona chini ilivyo mbaya ukilinganisha na zinazopatikana Arusha, Mbeya au Kilimanjaro…
2. Parachichi – hupimwa kufuatana na uzito. Kuna vijiparichichi vidogo vyeusi ambavyo vimejazana katika maduka makubwa makubwa (supamaketi) vijiparachichi koko- si vizuri hata kidogo- halafu aghali- mara nyingi si vitamu au vimeharibika ndani. Maparachichi makubwa makubwa toka Afrika nan chi za joto (tropics) hupatikana maduka ya pembe za chaki, kwa Wahindi au sokoni. Bei yake moja kiwastani ni £1.50- £2 kuendelea. Takriban 5,000.
3. Maembe kiwastani ni kama maparachichi – ila miaka ya karibuni yameanza kupungua bei na hupatikana kirahisi (kufuatana na msimu). Maembe haya( kama mananasi ) hutoka Ivory Coast, Costa Rica na Brazil.
4. Papai-pia hupimwa kwa uzito. Makubwa hayapatikani kabisa katika supamaketi za Kizungu. Ukilitaka uende mitaa tunaoishi wageni, ya wafanyakazi , Wahindi na Waturuki. Haya yanatoka Brazil – bei yake ni £5 (Shilingi 12,000) kuendelea.
5. Tikiti Maji- haya yako aina nne. Ya kijani nje, rangi ya chungwa ndani “Cantaloupe” yenye vitamin kibao huzwa wastani wa £1; ilhali manjano (toka Brazil) na kijani nje(toka Hispania ) wastani £2; aghali kuzidi yote ni tikiti maji lenyewe- kijani nje, jekundu ndani (“water-melon”);
£2.50 (Shs 6,000) kuendelea. Faida zake ki-afya hazisemeki.
6. Cherries na Strawberries. Matunda ya Kizungu. Kabla sijaja Majuu sikufaham Cherries, lakini Strawberry hupatikana maduka ya Kizungu Afrika.
Mcheri…tunda lenye faida nyingi ikiwemo kusaidia maradhi ya Jongo.

Cherry ambalo hupendwa sana na ndege, lina faida nyingi sana miongoni kusaidia kupambana na maradhi yanayosakama damu au mzungunguko wa maji mwilini kama Jongo. Jongo ni ugonjwa unatokana na aidha kurithi, kunywa sana pombe, nyama nyekundu, mayai, kutofanya mazoezi. Hujionyesha kwa maumivu makali katika goti moja au kidole gumba cha mguu. Cherry safi sana. Vichache katika kasha huanzia £2 (Shilingi 5,000).
Strawberry- Stroberi kiwastani huwa aghali. Msimu yanapopungua bei ni wakati wa baridi (Desemba-Machi) yanaposhuka toka shilingi 7,000 hadi 5,000. Bei hizi hufuatana na wapi unaishi, maduka makubw ana madogo , nk
Kawaida sehemu tunazoishi Watanzania , kama mitaa ya Mashariki ya London kuna unafuu wa bei za vyakula na matunda shauri wakazi wengi hapa pia ni Wahindi wenye maduka ya bei nafuu kuliko ya yale makubwa makubwa ya Kizungu.
7. Matunda yote yenye mbegu dani (Berries) kama Cranberries, Blue Berries, Blackberries- siku hizi hupatikana katika juisi zinazotengenezwa bila sukari nyingi. Nadhani tatizo kubwa la nchi Afrika ni kutengeneza juisi za matunda zilizojaa maji na sukari zaidi kuliko matunda. Huu ni udanganyifu na uroho wa wafanyabiashara wetu. Shirikisho la Ulaya limekuwa makini miaka ya karibuni kuzuia tabia hiyo Uzunguni na kuweka mikakati mikali.
Stroberi (Strawberry) – tunda linalopatikana zadi Uzunguni- ambalo lina Vitamin C kwa wingi.

Kifupi haya ndiyo matunda ya aghali rahisi hapa London.
Bei rahisi ni ndizi mbivu (toka visiwa vya Carribbean – na zingatia Matoke ya Uganda ni aghali sana- kichani kimoja kinaanzia shilingi elfu saba!), matufaha (matunda rasmi ya Kizungu), machungwa na machenza, Kiwi (yale matunda ya kijani toka New Zealand), zabibu, mapea (pears ), mapera, nk
Sasa tuongelee faida za matunda nliyoyachagua kwa leo yaani Mapapai na Maparachichi.
Ni muhimu kuzingatia kwamba matunda yanatakiwa kuliwa yakiwa katika kitengo kimoja- yaani chachu (“acid”), asidi au alkali (“alkaline”). Matunda hayo ya chachu ni maembe, mananasi, machungwa, zabibu, Kiwi, nk; ambapo alkali ni matikiti maji, ndizi mbivu, tufaha, mapea, Strawberry nk.
Matunda chachu (“asidi”) yanatakiwa yaliwe pamoja…

Mapapai na Maparachichi yanaangukia katika mkondo wa “alkali” na moja ya matunda yaliyowekwa katika Vyakula Vyenye Nguvu kuliko vyote (Superfoods) . Matunda hayo ni Machungwa , Kiwi, Papai, Parachichi. Vyakula hivi via faida sana mwilini.
Mfano wa matunda yenye “alkali” yanayotakiwa kuliwa pamoja.

Faida zake ni zifuatazo.
1. Kinga maradhi na kinga magonjwa (Anti-Oxidant) ambazo husaidia kukinga na kupambana na takataka zinazotolewa na mwili au zinazotoka katika mazingira machafu.
2. Vitamin C. Vitamin hii ni muhimu sana mwilini. Ukosefu wa Vitamin C husababisha uchovu, kukosa usingizi, uvivu, kutokuwa na hamu ya kula. Kwa siku mtu mzima unatakiwa upate gramu 40 za Vitamin C. Kwa wavuta sigara zidisha mara mbili. Ukila matunda yenye Vitamin C unapata kinga ya majeraha mwilini (vidonda pona haraka), huboresha wajihi, haiba na “nafsi” ya ngozi, mifupa, meno na mzunguko mzima wa damu mwilini- hivyo kusaidia usingizi ( na kwa watoto kusaidia kukua vizuri).
3. Papai lina “papain” inayosaidia kuukinga mwili na kulainisha tumbo- ndiyo maana kama umevimbiwa au huendi haja kubwa sawasawa (“constipation”) ukila papai husaidia sana.
4. Mapapai na Maparachichi yana “Beta Carotene”(itokanayo na Vitamin A) inayopatikana pia katika nyanya, karote, maembe, mchicha (ambao haukupikwa hadi ukanyong’onyea), mbegu mbegu (mbichi si za kukaanga au kuwekwa chumvi- hadi zikakongoroka) kama hizi pichani chini karanga, mlozi, korosho, nk.
Faida zake ni pamoja na kusaidia mizunguko ya umajimaji na damu mwilini, ngozi na nywele (safi sana kwa kina dada wanaojipenda), kupunguza mafuta katika damu (cholestoral) na “presha” – mambo yanayoua sana watu weusi duniani leo. Ukiwa upungufu wa “Beta Karotene” macho hayaoni vizuri, unaugua upesi upesi hasa maradhi ya mapafu (mafua, kikohozi,nk). Kwa wanawake waja wazito ni rahisi kupoteza watoto au kuzaa watoto ambao hawako sawasawa.
5. Maparachichi yanayo mafuta asilia. Mafuta haya ni mazuri SANA kuliko yale tunayoyapata katika nyama au vitu vilivyokaangwa, maana yanausaidia na haya haribu mwili. Makisio yake ni kalori 400 kwa parachichi moja. Hiyo ni nguvu kubwa sana. Ndiyo maana Parachichi (na Papai) huhesabiwa kama mfalme wa matunda.
Lazima izingatiwe kuwa chakula, mmea au tunda lolote lenye rangi nzito iliyokolea kama parachichi huwa na faida MARIDHAWA mwilini.
Hivyo, kuanzia leo kama hukua ukithamini matunda haya mawili- kayatafute. Kuna watu wazima wanaosema eti matunda ni chakula cha watoto. Wanakosea. Mtu mzima anahitaji kuendelea kuukarabati mwili wake. Kwetu Afrika ni ya bei nafuu- wapo wengi wanaofika Ulaya na Marekani wanashindwa kuyala shauri bei yake si mchezo. Halafu wala si matamu kama ya nyumbani Afrika…
MATUNDA OYEE!