RUMAFRICA Magazine

RUMAFRICA FASHION

RUMAFRICA FASHION

WANAHABARI WATIMULIWA KWA BUNDUKI KESI YA LEMA, MAHAKAMA YALIONYA JESHI LA POLISI ARUSHA:

 Wakati askari polisi saba watatoa ushahidi mahakamani katika kesi ya uchochezi inayomkabili Mbunge wa Arusha Mjini (Chadema), Godbless Lema, Mahakama imetoa onyo kwa askari Polisi na Magereza wanaowasumbua waandishi wa habari na wananchi.

Onyo hilo lilitolewa na Hakimu Mkazi Mfa- widhi wa Mahakama ya Mkoa wa Arusha, Augustino Rwezile baada ya askari Magereza kuwafukuza kwa mbio huku wakiwa na silaha waandishi wa habari waliotaka kuchukua kumbukumbu za Lema kufikishwa mahakamani.

Pia, aliwaonya Polisi ambao wamekuwa wakilalamikiwa kwa kuwazuia wananchi wanapokwenda kusikiliza kesi ya mbunge wao. 

Waandishi wa habari jana waliwahi asubuhi kusikiliza kesi ya Lema na kutaka kumpiga picha wakati akifikishwa mahakamani, lakini walipata wakati mgumu baada ya kukimbizwa na askari Magereza wenye silaha ambao hawakutaka mtu yeyote kupiga picha ya mtuhumiwa huyo.

Waandishi hao, Lilian Joel (Uhuru) na Janet Mushi (Mtanzania) waliokolewa na Hakimu Mkazi, Nestory Baro ambaye walimshika huku wakipiga kelele kuomba msaada hatua ambayo ilizua tafrani mahakamani.

Hata hivyo, baada ya tukio hilo, waandishi hao walipelekwa na hakimu Baro kwa Hakimu Mkazi Mfawidhi, Rwezile ambaye alishuhudia pia tukio hilo.

Hakimu Rwezile aliwaita maofisa wa Polisi, waliokuwa mahakamani hapo na kuwaonya kuacha tabia ya kuwakamata na kuwabughudhi wananchi na wanahabari wanaofika mahakamani hapo kusikiliza kesi.

Hakimu Rwezile, pia alilitoa agizo hilo la kuwaonya askari Magereza na Polisi baada ya wakili wa Lema, John Mallya kuomba tamko la mahakama kutokana na wananchi kuzuiwa kuingia mahakamani, kukamatwa na kunyanyaswa waandishi wa habari.

Hakimu Rwezile alitoa agizo tena kwa askari Magereza na Polisi wanaofika mahakamani kuacha kuwasumbua wananchi na kueleza pamoja na wanahabari wana uhuru wa kufika mahakamani na kusikiliza kesi.

“Hakuna usiri mahakamani hatutarajii tena kuona misuguano hapa, tayari nimezungumza na waandishi na askari Magereza kuhusiana na suala hili, eneo hili lipo chini ya Mahakama hivyo watu wanapaswa kuingia na kutoka salama,” alisema 

Jana saa mbili asubuhi, Lema alifikishwa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mkoa wa Arusha kwa basi la Magereza, akiwa chini ya ulinzi mkali na haikuruhusiwa kumpiga picha.

Mbele ya Hakimu Rwezile, wakili wa Serikali, Fortunatus Mhalila alisoma maelezo ya awali ya kesi hiyo na kudai upelelezi umekamilika na upande wa Jamhuri una mashahidi saba.

Aliwataja mashahidi hao kuwa ni Ofisa Upelelezi wa Polisi Mkoa wa Arusha (RCO), SSP George Katabazi, Mkuu wa Upelelezi wa Polisi Wilaya ya Arusha (OSCID), ASP Damas Masawe, Mkaguzi wa Polisi, Adam Nyamiti, WP 6826 Ester Yohana na Ofisa wa Kitengo cha Upelelezi Makosa ya Mtandao Makao Makuu ya Polisi, Ezekiel Kway.

Alidai katika kesi hiyo, Lema anatuhumiwa kuhamamisisha watu kutenda kosa ikiwa ni kinyume na kifungu 390 (35) cha Kanuni za Adhabu, iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2002.

Mhalila alidai Lema kati ya Agosti Mosi hadi 26, alitengeneza na kusambaza ujumbe mfupi wa sauti kupitia WhatsApp kuhamasisha watu kutenda kosa, ikiwapo kuwataka kufanya maandamano kuanzia Septemba Mosi mwaka huu. Baada ya maelezo hayo, Hakimu Rwezile alimtaka Lema kueleza kama maelezo hayo ni sahihi au la.

Lema alikanusha kutuma ujumbe wa kuhamamisha uvunjaji wa sheria. Wakili Mallya alisema upande wa utetezi upo tayari kupangwa kwa siku ya kuanza kuwasikiliza mashahidi. Kutokana na maelezo hao, Hakimu Rwezile aliahirisha kesi hiyo hadi Desemba 2, ushahidi utakapoanza kutolewa.

Lema na mkewe, pia wana kesi nyingine ya kutoa lugha ya uchochezi dhidi ya Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mrisho Gambo ambayo nayo iliahirishwa hadi Desemba 21 kutokana na mtuhumiwa wa pili, Neema Lema (33) kutokuwapo mahakamani.

Wakili Mallya alisema Neema ameitwa jijini Dar es Salaam katika kesi nyingine. Baada ya maelezo hayo, Hakimu Rwezile aliahirisha kesi hiyo na Lema kurejeshwa magereza hadi leo, Mahakama Kuu Kanda ya Arusha itakapoanza kusikiliza maombi ya dhamana.