RUMAFRICA Magazine

RUMAFRICA FASHION

RUMAFRICA FASHION

AJALI YA LORI NA HIACE YAUA WATU 9 NA KUJERUHI 18, IRINGA

 
IRINGA: Watu tisa wamefariki dunia na wengine 18 kujeruhiwa kufuatia ajali mbaya ya gari iliyotokea eneo la Ifunda mkoani Iringa jana Desemba 5, 2016 baada ya lori kugongana na gari dogo la abiria aina ya Toyota Hiace.
Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Amina Masenza amesema dereva wa lori lililopata ajali lililokuwa likitokea Mbeya kuelekea Dar es Salaam, alishindwa kufunga breki na kuigonga Hiace iliyokuwa imeegeshwa pembezoni mwa barabara.

“Lori limeharibika kabisa na Hiace pia imeharibika vibaya,” alisema RC Masenza.

“Lori hilo liliposhindwa kufunga breki liliigonga Hiace ambayo ilikuwa na abiria na kwenda mbele na kisha kugonga watembea kwa miguu.” 

RC Masenza alisema katika ajali hiyo iliyotokea jana jioni, madereva wa magari hayo wote wamejeruhiwa na wamelazwa Hospitali ya Mkoa wa Iringa pamoja na majeruhi wengine.

“Dereva mmoja yupo chumba cha upasuaji kwa kuwa mguu wake umevunjika na mwingine yupo wodini,”alisema RC Masenza.