RUMAFRICA Magazine

RUMAFRICA FASHION

RUMAFRICA FASHION

MKE WA KOMBA AMWANGUKIA JPM KUHUSU MAFAO YA MUMEWE

DAR ES SALAAM: Ikiwa imetimia miaka miwili tangu kifo cha aliyekuwa kada maarufu wa Chama cha Mapinduzi CCM, Kapteni John Komba, Mke wake Salome Komba ameibuka na kumuomba mwenyekiti wa Chama hicho Rais Dk John Magufuli amsaidie ili aweze kulipwa ‘Mafao’ na ‘Stahiki’ za mume wake.

Akiongea kupitia kipindi cha Maisha Mseto cha Times Fm mapema jana (Jumanne, Feb 28, 2017) asubuhi, Salome alidai kuwa wanaidai CCM mafao ya Sh75 milioni kama jasho la mume wake alivyokitumikia CCM lakini hadi sasa wamelipwa Sh4.5 milioni.

“Namuomba Mwenyekiti wa CCM anisaidie niweze kupata mafao ya marehemu, alikuwa anaipenda sana CCM na mpaka anafariki alikuwa ameanza kuwahamasisha wasanii kuhusiana na kampeni,” amesema na kuongeza:

“Niliongea na Katibu Mkuu, nikamweleza nadai Sh75 milioni ila nimepewa Sh4.5 milioni na ni mwaka wa pili sasa hivi tangu mume wangu afariki, hivyo naomba nisaidiwe nipate jasho lake kwa sababu ni haki yake kwa jinsi alivyojitoa kwenye chama, na amefariki akiwa ndani ya CCM.”