RUMAFRICA Magazine

RUMAFRICA FASHION

RUMAFRICA FASHION

MHE MWANJELWA AWATAKA WAKUFUNZI WA VYUO VYA KILIMO NCHINI KUTOFANYA KAZI KWA MAZOEA

Na Mathias Canal, Mtwara

Wakufunzi wa Vyuo vya Kilimo kote nchini wametakiwa kutofanya kazi kwa mazoea badala yake kufanya kazi kwa Weledi, Ubunifu na Maarifa ili kuongeza tija katika majukumu yao ya kufundisha wanafunzi ambapo baadae wanazalisha wataalamu mbalimbali katika sekta ya Kilimo.

Kauli hiyo imetolewa juzi 22 Disemba 2017 na Naibu Waziri wa Wizara ya Kilimo Mhe Mary Mwanjelwa wakati akizungumza na Wakuu wa Idara na Wafanyakazi wa Chuo cha Kilimo (MATI) Kilichopo katika kijiji cha Naliendele katika Halmashauri ya Wilaya ya Mtwara Mjini.

Alisema kuwa watendaji hao wanapaswa kuwa wabunifu katika nyanja mbalimbali zitakazowawezesha kuwa na kipato cha ziada kwa kufuata sheria, taratibu na kanuni.

Alisema kuwa kufanya hivyo kutawanufaisha kuwa na kipato kitakachowawezesha kuendesha chuo pasina kutegemea serikali kwa kina jambo ambalo litapunguza malalamiko dhidi ya serikali kufanya kila kitu.

Aidha, alisisitiza viongozi wa vyuo vyote vya Kilimo nchini kutumia vyombo mbalimbali vya Habari sambamba na mitandao ya kijamii ili kutangaza maudhui ya vyuo na kozi zinazofundishwa ili kurahisisha wanafunzi kupata wepesi katika uchaguzi wa vyuo vya kusoma.

Katika ziara hiyo Naibu Waziri wa Kilimo Mhe Mary Mwanjelwa alitembelea na kujionea miundombinu ya Taasisi na kazi za mafunzo ikiwa ni pamoja na kuangalia shughuli za uzalishaji wa mazao mbalimbali.

Kwa upande wake Kaimu Mkuu wa Chuo cha Kilimo Mtwara Ndg Elias L. Maijo alimpongeza Naibu Waziri huyo wa Wizara ya Kilimo kwa kuaminiwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe Dkt John Pombe Magufuli na hatimaye kuteuliwa kumsaidia katika majukumu yake ambapo pia ameahidi kutekeleza maelekezo yote yaliyotolewa.

MWISHO.







Comments